Thursday 30 September 2010

DK. SHEIN : MSIDANGANYIKE.

Dk. Shein: Msidanganyike



Chagueni CCM kwa maendeleo


Aahidi maendeleo zaidi Kaskazini Unguja

Na Mwanajuma Abdi

MGOMBEA Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohammed Shein, amesema chama hicho ndicho chenye uwezo mkubwa wa kuwaletea maendeleo wasidanganyike na vyama vingine vinavyotoa ahadi zisizotekelezeka.

Alisema Serikali ya CCM imesambaza huduma za afya, elimu, maji na imetandika miuondombinu ya barabara na nishati ya umeme kwa wananchi wake, katika kuwafikishia maendeleo ya kweli.

Kauli hiyo ameitoa jana, Bumbwini Makoba Wilaya ya Kaskazini 'B', Unguja, katika mkutano wa kampeni za uchaguzi mkuu utaofanyika Oktoba 31 mwaka huu, ambapo aliwanadi wagombea wa ubunge, uwakilishi na udiwani wa majimbo matatu ya Kitope, Bumbwini na Donge.

Aliwataka wananchi wasidanganyike na ahadi za vyama vyengine, hivyo aliwasihi wasikilize sera za kila vyama ili wajuwe nani anatoa hadi za ukweli na zinazotekelezeka kama za CCM, ambapo aliwaomba kura zao wawapigie wagombea wa Chama hicho kuanzia Urais wa Zanzibar, Tanzania, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani.

Dk. Shein, ambae ni Makamu wa Rais wa Tanzania, alieleza CCM ni nambari 'one' na ndio chama makini katika kutekeleza ilani na sera zake zinazoahidiwa wakati wa kampeni, ambazo ni muongozo wa katika Serikali kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi bila ya ubaguzi.

Alieleza CCM ni chama pekee chenye historia kubwa ya nchi kutokana kuunganisha vyama vya ASP na TANU, ambapo mwaka 1963 ilani ya Chama cha Afro Shirazi Party ilinadiwa na jambo hilo linaendelea kunadi sera na ilani za Chama Cha Mapinduzi kwa sasa baada ya kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi.

Aliongeza kusema kwamba, Chama hicho ndicho pekee chenye uwezo wa kulinda na kuyaenzi Mapinduzi matukufu ya Zanzibar Januari 1964 na pia kina uwezo na jukumu la kudumisha amani na utulivu kwa kuleta umoja na mshikamano nchini.

Aliwahakikishia wananchi wa majimbo ya Kitope, Bumbwini na Donge kwamba maendeleo makubwa yatafanywa huko pindi akipata ridhaa ya kuongoza Zanzibar katika huduma za maji safi na salama kwa kupitia mradi mkubwa wa ACRA unaofadhiliwa na jumuiya mbali mbali katika ambapo shehia 18 watafaidika na huduma hiyo utaotumia zaidi ya shilingi bilioni 1.8.

Alisema mradi huo pia utakwenda sambamba na ujenzi wa vyoo vya kisasa kwa nyumba 533, ambapo katika kijiji cha Bumbwini nyumba 200 zitafaidika pamoja na hupatiwa huduma bora kwa wafugaji, kilimo cha mboga mboga na hivi sasa wananchi 100 wameshapatiwa mafunzo ya kilimo hicho na mpunga wa umwagiliaji maji kwa kulima ekari moja na kuweza kupata mavuno ya magunia 30.

Alifahamisha kuwa, mapinduzi ya kilimo yatafanyika katika kuwakomboa wakulima kwa kuwapatia nyenzo na kuwajengea uwezo katika kuzalisha mazao ya matunda na minazi kutokana na mengi yao kuparama na kusababisha kutozaa tena kutokana na kukatwa kwa makuti na mengine kuzeeka kwa kufikisha miaka 100.

Alieleza pia kutajengwa barabara ya Bumbwini Makoba hadi Kiongwe mpaka pwani, Bumbwini hadi Mwangapwani kutokana hiyo ni miji ya kihistoria lazima watu waje kujifunza na waone maendeleo.

Alizitaja barabara nyengine atazojenga ni Kitope - Kichwele - Pangani itakuwa na urefu wa kilomita nne, barabara ya Donge Mtambile hadi Muwanda kilomita tatu pamoja na daraja ya Zingwezingwe litajenga kwa kisasa, ambapo umeme pia vijiji vyote vilivyokuwa haujawahi kufika katika Jimbo la Kitope kama Mchungwani na Mbaleni.

Dk. Shein alisema ataimarisha huduma ya afya katika majimbo hayo na kuwapeleka madaktari bingwa wa kuchunguza maradhi mbali mbali pamoja na kuwapatia gari la wagonjwa 'Ambulance' kituo cha Afya cha Misufini ili kukuza huduma za mama na mtoto.

Mgombea huyo aliyekuwa na mkewe Mama Mwanamwema Shein, aliahidi kukuza elimu kuanzia msingi hadi vyuo vikuu, ambapo katika kijiji cha Muwanda kutajenga skuli ya sekondari ya kisasa pamoja na nyumba za walimu tatu, ambapo alitoa wito kwa wazazi kuwahimiza vijana kusoma ili waweze kupata nafasi ya kusoma elimu ya juu katika vyuo vikuu vya Zanzibar.

Alifafanua kuwa, wataanzisha Diploma ya sayansi ili walimu kuweza kusomesha pamoja na watu wengine wataohitaji kupata masomo ya uongozi bora, ili nchi ipige hatua za maendeleo kwa haraka kwani bila ya kuwa na vijana wasomi hatuwezi kupiga hatua kwa kasi kubwa.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhan Ferouz alisema mafanikio makubwa yamefanywa wilaya ya Kaskazini 'B', Unguja pamoja na kusambazwa matrekta kwa ajili ya kuimarisha kilimo chini ya Utawala wa Rais wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume, hivyo aliwaomba wananchi wakipigie kura ili maendeleo zaidi yapelekwe huko.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini, Haji Juma Haji, aliwakumbusha wananchi kuwa wasiharibu kura zao kwa vyama vyengine visivyoweza kushinda kwa vile kura zao hazitotosha ni bora wakawapigia wagombea wa CCM wanaowania nafasi mbali mbali za Urais wa Zanzibar Dk. Ali Mohammed Shein, Rais wa Tanzania, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani.

KAMPENI ZA KISTAARABU ZAENDELEA KILA KONA ZANZIBAR.

Kampeni za kistaarabu zaendelea kila kona Zanzibar



 Polisi wataka kudumishwa amani, utulivu


Na Mwantanga Ame

HUKU kampeni za kuwania madaraka kwa vyama za siasa zikiwa zimeshika kasi, Makamanda wa jeshi la Polisi wameeleza kuwa zinaendelea vyema bila kuripotiwa uvunjifu wa amani.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Muandishi wa habari hizi, Makamanda wa Mikoa Mitano ya Unguja na Pemba, walieleza kuwa vyama vyote vinavyoshiriki uchaguzi mkuu wa mwaka huu vimekuwa vikiendesha kampeni hizo kwa ustaarabu mkubwa.

Kamanda wa Polis Mkoa wa Kaskazini Unguja Masoud Mselem Mtulia, alisema hali katika Mkoa huo shuari baada ya wagombea wa vyama kwa ngazi ya kitaifa na majimbo kuendesha kampeni zao bila ya kutokea kwa vitendo vya kuhatarisha amani.

Alisema matatizo yalijitokeza baada ya kuanza kwa kampeni katika Mkoa huo ni kuwapo kwa baadhi ya wahuni wasiofahamika kuchana picha za wagombea.

Nae Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Aziz Juma, alisema hadi sasa kampeni za vyama katika wilaya zake zinaendelea vyema na hakuna matatizo yliowahi kuripotiwa ya uvunjifu wa amani.

Huku kukiwepo tuhuma za misafara ya wafuasi wa CCM na CUF kurushiwa mawe katika eneo la Bububu wiki iliyopita, wairudi kwenye mikutano ya kampeni huko Kaskazini Unguja.

Kamanda wa Mkoa wa kaskazini Pemba Yahya Bugi, alisema kampeni za Mkoa huo zimeenda kwa amani pamoja na kujitokeza kwa matatizo madogo madogo yakiwemo ya baadhi ya watu wasiojulikana kuchaniana picha za wagombea.

Alisema asilimia kubwa ya picha ambazo zimekuwa zikichanwa zimekuwa zikihusishwa wagombea wa nafasi ya Urais kwa chama cha CCM na CUF.

Alisema jeshi hilo limekuwa likikabiliwa na tatizo la kukosa ushahidi wa kutosha jambo ambalo linasababisha kutowatambua wahusika na kuwafikisha katika vyombo vya sheria.

Huko Mkoa wa Kusini Pemba, Kamanda wa Mkoa huo, Hassan Nassir, alisema hakuna matukio maovu yaliyoripotiwa kwenye kampeni za siasa zinazoendelea katika mkoa huo.

Naye Kamanda wa Mkoa wa Kusini Unguja, Agustino Ollomo, alisema hali ya kampeni katika mkoa wake sio mbaya inaendelea vyema na wanachama wa vyama wamekuwa wakitumia viwanja mbali mbali bila ya bughudha kufanya kampeni zao.

Hata hivyo, Makamanda hao wamewataka wananchi kuhakikisha wanaendeleza amani ya nchi wakati wakisubiri kushiriki katika uchaguzi Mkuu ujao unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31, mwaka huu.

Wakati huo huo Kamishna Msaidizi wa Opereshini katika Jeshi la Polisi Zanzibar Hamdani Omar Makame, amevitaka vyama vya siasa kuchukua tahadhari ya kujizuia kuanzisha kwa vurugu baada ya kujionesha kuwapo kwa viashiria vya aina hiyo.

Tahadhari hiyo ameitoa huku kukiwa baadhi ya watu wameashaanza kuanzisha mtindo wa kurushiana mawe wanaporudi katika mikutano ya kampeni.

MAWASILIANO HUHARAKISHA MAENDELEO --- MWAKILISHI UNIFEM

Mawasiliano huharakisha maendeleo - Mwakilishi UNIFEM



Na Sheikha Haji

MWAKILISHI wa mfuko wa Umoja wa Mataifa wa kuwasaidia wanawake UNIFEM, Mohammed Buba amesema, ili wanawake waweze kupata maendeleo ya haraka, mawasiliano ya redio ni muhimu katika maisha yao ya kila siku.

Buba alisema mara nyingi wanawake wamekuwa wakikosa fursa ya kusikiliza taarifa mbalimbali zinazojiri ulimwenguni kote kutokana na mzigo wa kazi unaowakabili.

" Wanawake wakipatiwa nafasi ya kupata habari na kushiriki katika maendeleo wanaweza kupiga hatua kubwa kimaendeleo", alisema mwakilishi huyo.

Akitoa msaada wa redio 200 zinazotumia nguvu za jua kwa vikundi vya wanawake walio katika mradi wa kuwanyanyua wanawake kiuchumi WEZA, alisema iwapo watazitumia katika shughuli zao zitawasaidia kupata taarifa mbali mbali zikiwemo za kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Mradi wa redio jamii unalengo la kuviwezesha vikundi 60 vya mradi wa WEZA, vikiwemo 30 kwa Unguja na 30 kwa Pemba, kuandaa vipindi mbalimbali vinavyolenga kuwapatia elimu ya uchaguzi, haki na masuala ya kimaendeleo ambavyo vitarushwa hewani na kituo cha redio cha Zenj FM.

Wakitoa maoni yao juu ya mpango huo wanawake hao walisema, redio hizo zitawasaidia katika kuwaelimisha na kwamba kutokana na kujua umuhimu huo wataweza kuzitumia ipasavyo ili kuleta mabadiliko.

Walisema mara nyingi wamekuwa wakikosa fursa ya kusikiliza habari hususan wakati wa asubuhi na mchana kutokana na kuzongwa na mzigo wa kazi za mashambani na hivyo wanaporudi huharakia shughuli za nyumbani.

"Shughuli za nyumbani ni kikwazo kazi ni nyingi hivyo unasahau kabisa kushughulikia taarifa na vipindi muhimu", alisema mmoja wa waratibu wa vikundi hivyo.

Wakati huohuo, Afisa wa WEZA, Asha Abdi aliwataka wanawake hao kuitumia fursa hiyo kwa kubuni mbinu mbalimbali zikiwemo kutengeneza vipindi vitakavyokuwa na nguvu ya kuwaletea maendeleo.

Miongoni mwa mada zitakazojadiliwa kupitia vipindi hivyo kuelekea uchaguzi ni pamoja na sifa za kiongozi bora, sheria na haki za kupiga kura, sera za vyama na umuhimu wa wanawake kupiga kura.

Wednesday 29 September 2010

ZITTO KABWE : MAFUTA SI SUALA LA MUUNGANO.

29/9/2010



Zitto Kabwe: Mafuta si suala la Muungano


 Ahoji Zanzibar kutofaidika na madini ya Bara


Na Salum Vuai, Maelezo

MGOMBEA ubunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) katika jimbo la Kigoma Mjini Zitto Kabwe, amesema iwapo atarudi tena bungeni, atasimamia kwa nguvu zake zote ili suala la mafuta na gesi liondoshwe katika orodha ya mambo ya Muungano.

Kabwe alikuwa akijibu suala kuhusu Muungano katika mdahalo uliowakutanisha wagombea wa kundi la vijana uliofanyika katika hoteli ya Movenpick jijini Dar es Salaam na kurushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha ITV juzi usiku.

Katika mdahalo huo ulioshirikisha wagombea wa vyama vya CUF na CHADEMA kutoka majimbo ya mikoa mbalimbali chini ya uenyekiti wa Jenerali Ulimwengu, Kabwe alisema kimsingi anakubaliana na hoja kuwa iwapo Zanzibar kuna mafuta, basi hiyo ni mali yake na haijuzu kutiwa mkono na Serikali ya Muungano.

Alifahamisha kuwa, kwa vile Zanzibar haifaidiki na rasilimali za madini zinazopatikana Tanzania Bara, ni haki ya wananchi wa huko kudai mafuta yanayoaminika kuwepo visiwani yasiingizwe katika mambo ya Muungano.

"Suala la mafuta yanayokisiwa kuwepo Zanzibar, limezua mjadala mkubwa bungeni, mimi sioni mantiki ya kuwanyima Wazanzibari haki yao, kwani nao pia hawafaidiki na rasilimali za madini zilizoko Bara, nitajitahidi kuona mafuta yanaondoshwa kwenye mambo ya Muungano", alieleza msimamo wake.

Aidha alieleza kuwa mbali na suala hilo, zipo Wizara nyingi zilizo chini ya mwamvuli wa muungano wa Tanzania lakini haziihusu Zanzibar ingawa ina wabunge.

Hata hivyo, mgombea huyo alisema muungano wa Tanzania ni kitu cha thamani kubwa ambacho nchi nyingi duniani zinatamani kuwa na umoja kama huo lakini zimeshindwa.

Aliwasifia waasisi wa muungano huo hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na marehemu Abeid Amani Karume, akisema wameweka misingi imara ya udugu kati ya watu wa pande mbili hizo, ambayo inahitaji kuimarishwa kwa kutoruhusu mgawanyiko.

Ili kufikia azma hiyo, alishauri kuweko na haki sawa kwa wananchi wa nchi hizo kwa kutozusha mifarakano katika mambo yanayoweza kupatiwa ufumbuzi bila kusuguana.

Alifahamisha kuwa, muungano wa Tanzania uliasisiwa kama njia ya kuelekea umoja wa Afrika nzima ambao waasisi wake na viongozi wa zamani wa nchi mbalimbali wakiwemo Kwame Nkrumah wa Ghana na Gamal Abdelnasser wa Misri walikusudia kuunda.

"Pamoja na kasoro zinazojitokeza, lakini muungano wetu ni urithi mzuri tulioachiwa na waasisi wa taifa letu, hivyo changamoto zilizopo zitufunze namna bora ya kuuimarisha na kuuenzi na kwa kufanya hivyo, tutakuwa tunawaenzi waanzilishi wake", alifahamisha.

Nao wagombea wa CUF kutoka baadhi ya majimbo ya Morogoro na Dar es Salaam, walisisitiza msimamo wa chama chao kuunda serikali tatu iwapo watashinda katika nafasi ya uraisi wa Tanzania.

Walisema chama chao hakioni sababu ya kuendelea na mfumo wa serikali mbili, na kuelezea jambo hilo linaridhiwa na wananchi wengi wa Tanzania Bara, ambao wanaona njia hiyo tu ndiyo itakayosaidia kuondosha baadhi ya kero za muungano huo.

Mwenyekiti mwenza wa mjadala huo Jenerali Ulimwengu, alisema utaratibu huo utaendelea katika maeneo mbalimbali ili kuwapa wananchi fursa ya kufahamu kwa undani mwelekeo wa wagombea wao kabla kuingia katika uchaguzi mkuu Oktoba 31, mwaka huu.

Aliwapongeza wagombea walioshiriki kikao hicho kwa kusema hiyo ni miongoni mwa dalili za kukua kwa demokrasia nchini.

NAHODHA ASISITIZA UMOJA MIONGONI MWA WAISLAM.

Nahodha asisitiza umoja miongoni mwa Waislam

Na Abdulla Ali, Dar es Saalam

IMEELEZWA kuwa wakati umefika kwa Nchi za Kiislamu kuwekeza kwenye elimu ya Sayansi kwa lengo la kujiongezea uwezo na kukabiliana na ushindani wa mataifa Makubwa.

Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha alisema hayo alipokuwa akifungua semina ya Hijja na Umoja wa Kimataifa wa Umma wa Kiislamu iliyofanyika katika ukumbi wa Mayfair Plaza jijini Dar es Salaam.

Waziri Kiongozi alisema ukosefu wa elimu ya kutosha na umoja miongoni mwa waislamu ni miongoni mwa sababu zinazosababisha matatizo ya umasikini katika jamii hiyo.

Nahodha alisema kutokana na hali hiyo kuna haja ya kuimarisha umoja miongoni mwa waislamu, umoja ambao utapatikana kwa kueneza elimu na uhamasishaji wa dini.

Alisema Waislamu wakiungana wataweza kupambana na matatizo yao yakiwemo ya kiuchumi na kisiasa ,hivyo watajiongezea nguvu katika dunia.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Hijja na Kiongozi wa ujumbe wa Iran Sayyid Ali Qadhy Askary, alisema lengo lao ni kukutana na waislamu wenzao ili kubadilishana mawazo na kujifunza kutoka kwa waislamu wa kanda ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini.

Alisema ibada ya Hijja ina imarisha umoja wa waislamu wa Mataifa mbali mbali kwa kuwakutanisha sehemu moja na semina yao inazidi kuimarisha lengo hilo kwa kutoa fursa ya kuimarisha zaidi kutokana na mapendekezo yao.

Semina hiyo ya siku mbili imewajumuisha Mashekh,Maulama kutoka Iran,Tanzania, Kenya, Uganda na baadhi ya nchi za Kusini mwa Afrika, ambapo imefunguliwa na Rais Mstaafu wa Tanzania Ali Hassan Mwinyi na kufungwa na Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha.



WANAWAKE ZANZIBAR WASIFANYE MAKOSA -- MAMA SHEIN

Wanawake Zanzibar wasifanye makosa - Mama Shein



Mwandishi Maalum – Zanzibar

MKE wa mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi Mama Mwanamwema Shein amewataka wanawake visiwani Zanzibar wasifanye makosa katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu kwa kuchagua upinzani.

Mama Shein aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na akina mama wa vikundi mbalimbali vya kilimo cha mwani kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja na Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja katika ukumbi wa hoteli ya Bwawani.

Alisema wanawake wanapaswa kuhakikisha CCM inashinda kwa kishindo, kwani chama hicho tayari kimepanga mipango madhubuti ya kuendeleza akina mama katika Ilani yake ya Uchaguzi ya 2010-2015.

Alisema miongoni mwa mipango hiyo ni uanzishwaji wa Benki ya Wanawake Zanzibar ambayo itawawezesha wanawake kuweka na kukopa ili kuimarisha shughuli zao za kijamii na kiuchumi.

“Mikopo hiyo itatusaidia akina mama kuendeleza miradi yetu iwe ya kilimo cha mwani, migomba, kusomesha watoto, kujenga nyumba na miradi mingine mtakayoibuni,” alisema Mama Shein na kusisitiza wasisahau kulipa ili wengine wanufaike.

“Hivyo, mwaka huu tusikosee, tukikosea tutakuja kujuta. Tujipange tutafute kura nyingi kwa CCM ili mambo yetu haya akina mama yaweze kufanikiwa,” alisema Mama Shein.

Mama Mwanamwema alitumia fursa hiyo kuwahimiza akina mama visiwani hupa kutilia mkazo suala la kusomesha watoto wote wakiwemo wa kike na wa kiume kwa kuwa ndio wanaotegemewa kuwa viongozi wa baadae.

Alisititiza suala la akina mama kuimarisha mshikamano, amani na utulivu katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu kwani mara nyingi kupotea kwa amani waathirika wakubwa wanakuwa ni wanawake na watoto.

JK.: UMASIKINI KWA WAVUVI KUWA HISTORIA.

JK: Umasikini kwa wavuvi kuwa historia


RAIS Jakaya Mrisho Kikwete na Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu amesema kuwa endapo atachaguliwa tena ataanzisha mpango maalum wa kuwakopesha zana wavuvi katika maziwa ya Tanzania.

Aidha, Rais Kikwete amewatangazia majambazi wanaofanya uhalifu, kushambulia na hata kuua wavuvi katika maziwa ya Tanzania kuwa sasa kiama chao kimefika.

Rais Kikwete ameyatangaza hayo, alipofanya mikutano ya Kampeni kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu katika maeneo ya Busekera, wilaya ya Musoma, Mkoa wa Mara na Ukara, wilaya ya Ukerewe, Mkoa wa Mwanza.

Akizungumza na wananchi katika eneo la Busekera, Kata ya Bukumi, Jimbo la Uchaguzi la Musoma Vijijini Mkoani Mara, jioni ya jana, Rais Kikwete alitangaza ama ya Serikali yake kuwainua wavuvi kutoka kwenye umasikini.

Amesema kuwa katika kuinua hali hiyo ya wavuvi, Serikali yake, kama itachaguliwa tena, itaanzisha mpango maalum wa kuwakopesha zana wavuvi katika maziwa ya Tanzania kama ule wa MACEMP ambao unatumika kuwakopesha wavuvi wanaovua katika Bahari ya Hindi katika maeneo ya Pwani ya Tanzania.

“Endapo tutachaguliwa, tutaanzisha mpango wa kuwakopesha zana wavuvi katika maziwa ya Tanzania kwa kuwapokesha boti, injini, nyavu na zana zote muhimu ili kuinua kipato chao kwa kuvua samaki wengi zaidi,” amesema Rais Kikwete katika eneo hilo lililoko pwani ya Ziwa Victoria.

Akizungumza katika eneo la Bwisya la Kisiwa cha Ukara, kilichopo wilaya ya Ukerewe, Mkoa wa Mwanza, Rais Kikwete ametangaza kiama kwa majambazi ambao wamekuwa wanawashambulia wavuvi na wasafiri katika Ziwa Victoria kwa kusema kuwa sasa mwisho wao umefika.

“Nataka kuwahakikishieni ndugu zangu kuwa najua kuwa mmekuwa mnasumbuliwa na majambazi katika Ziwa Victoria. Tatizo hilo tumelipatia ufumbuzi na napenda kutangaza kiana cha majambazi, mwisho wao umefika,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:

“Tutaanzisha kikosi maalum cha kutoa ulinzi katika Ziwa Victoria katika maziwa yetu mengine. Vijana wako kwenye mafunzo na tutanunua boti za kisasa za ulinzi kukiwezesha kikosi hicho kufanya kazi vizuri. Mtalala, mtavua, mtaisha bila wasiwasi kutoka kwa majambazi na ujambazi.”

Rais Kikwete pia amesema kuwa endapo atachaguliwa tena kurudi madarakani, atahakikisha kuwa wananchi wanapata usafiri wa uhakika zaidi kwa kununua kivuko kipya kuchukua nafasi ya MV Nyerere ambacho kimechoka.

Rais Kikwete jana ameendelea na Kampeni katika maeneo ya Ukara na Nansio katika Wilaya ya Ukerewe, Kisesa na Nyanguge katika Wilaya ya Magu, na Lamadi na Bariadi katika Mkoa wa Shinyanga.

MAALIM SEIF AUSUSA MKUTANO KAMPENI

Maalim Seif aususa mkutano kampeni



Ni kwa kujitokeza wanachama ‘kiduchu’

KWA mara ya kwanza tokea kuanza kwa historia ya vyama vingi vya Siasa Tanzania , Katibu Mkuu wa CUF, Malim Seif Sharif Hamad, amekataa kuwahutubia wafuasi wa Chama hicho akatika Jimbo la Chake Chake Kisiwani Pemba kwa kutoridhishwa na mahudhurio.

Maalim, alikuwa mgeni Rasmi katika Mkutano huo uliofanyika katika Kiwanja cha Banda Taka , Jimbo la Chake Chake , kwaajili ya kuwanadi Wagombea Ubunge na Uwakilishi wa Jimbo hilo.

Katibu Mkuu huyo alisema ni vyema mkutano huo, ukapangwa siku nyengine tena iwe jioni na asubuhi kama ilivyokuwa ambapo alisimama jukwaani kwa muda wa dakika 10.

“Siridhiki na na wtu waliojitokeza na idadi ya watu wa Jimbo la Chake Chake , na muomba meneja wa Kampeni anipangie mkutano mwengine tena iwe jioni”, alieleza Maalim Seif.

Hata hivyo aliwanadi wagombea wa Ubunge , Uwakilishi , na Udiwani wa Wadi za Chake Chake na kuwataka wananchi kuwapa kura zao iliwaijenge Chake Chake mpya na baadae kuteremka katika jukwaa hilo.

Pamoja na kiroja hicho cha mwanzo kutokea katika mikutano ya Maalim Seif hapa Pemba , lakini baadhi ya wananchi walisikika wakisema kuwa uzembe ulifanyika katika kuutangaaza mkutano huo kwa viongozi husika wa CUF, ambao ulipaswa kutangazwa Pemba nzima ijapo kuwa ni wajimbo.

Hivyo pamoja na mgombea huyo kukataa kuhutubia Wafuasi wake , lakini Mjumbe wa Baraza kuu la Cuf, Taifa na mwakilishi wa Chama hicho alikuwa akimnadi Mgombea huyo wa Urais kwa tiketi ya CUF, kwa kuwataka Wananchi wa Pemba kumpa kura zao maalim Seif

MUZADALIFA YAHIMIZA MATUZO KWA WATOTO YATIMA

Muzdalifa yahimiza matunzo kwa watoto yatima


JUMUIA ya Muzdalifa, kwa kushirikiana na Taasisi ya kiislamu ya Insani Yrdim Vakfi (IHH) ya Uturuki imetoa shilingi 13,000,000 kusaidia watoto yatima katika mradi wa pamoja wa kuwajengea uwezo wa kimaisha watoto katika masuala ya elimu na uchumi.

Akikabidhi fedha hizo, Mwenyekeiti wa Jumuia hiyo Abdalla Khadhar amesema kuwa msaada huo ni muhimu kwa watoto mayatima katika kuendeleza maisha yao ya kila siku na kuwataka wazazi kuitumia vyema misaada inayotolewa kwa watoto wao.

Alisema misaada mbali mbali inayotolewa na wafadhili kwa ajili ya watoto mayatima inapaswa kuwafikia walengwa na wala isiwe miradi kuwaendeleza wazazi nazaidi ifikirie kutatua matatizo yanayowakabili watoto hao.

“Tunajuwa nyinyi walezi na wazazi wa watoto mayatima ndiyo mnaodhibiti fedha hizi kwa ajili ya watoto wenu lakini lazima matumizi yake yalenge kuwaondolea matatizo wanayokabili badala ya kuelekeza matumaini kwa mambo mengine,” alisema Maalim Abdalla.

Aidha aliwataka wazazi kuwa karibu na viongozi wa jumuia hiyo mara kwa mara ili kuwa na mikakati ya pamoja kuhusu mambo muhimu yanayowakuta watoto.

Nae Katibu Mtendaji wa Jumuia hiyo, Farouk Hamad amewahimiza wazazi na walezi wa watoto yatima waache tabia ya kuwatekeleza watoto wao na kuwapatia huduma bora za malazi, chakula na kuwatengenezea maisha mazuri ya baadae.

Alisema jumuia yake itaendelea kutafuta wafadhili zaidi wa nje na ndani ili kuhakikisha weartoto wanapata manufaa zaidi kutokana na misaada inayotolewa hivyo kuongeza kasi ya kutafuta wafadhili zaidi wa ndani na nje ya nchi.

Mapema Mkuu wa kitengo cha watoto yatima katika Jumuia hiyo, Amir Seif alisema kila mtoto aliweza kukabidhiwa shilingi laki moja 35 elfu kwa ajili ya kusaidia huduma mbali mbali.

REDEA YAIBUA KAULIMBIU NZITO.

RADEA yaibua kaulimbiu nzito




WAKATI Watanzania wakijiandaa kuingia katika uchaguzi mkuu Oktoba 31, mwaka huu, wananchi wa jimbo la Rahaleo wametakiwa kutumia fursa hiyo kuchagua viongozi wenye dira na dhamira ya kweli kuwaletea maendeleo bila kujali vyama wanavyotoka.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo Rahaleo jana, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo jimbo hilo (RADEA) Nabahani Said Washoto, alisema jimbo hilo linakabiliwa na changamoto nyingi ambazo viongozi waliopita wameshindwa kuzipatia ufumbuzi licha ya kutoa ahadi tamu kila wakati wa uchaguzi unapofika.

Washoto aliyataja baadhi ya matatizo makubwa waliyonayo wananchi wa jimbo hilo, kuwa ni pamoja na kero ya dawa za kulevya, ukosefu wa ajira kwa vijana pamoja na kutokufika mbali kielimu, uhaba wa maji safi na salama na nyengine ambazo alisema zimekuwa zikiwasumbua wananchi bila hatua za kuzimaliza kuchukuliwa.

Mwenyekiti huyo alifahamisha kuwa, uzoefu unaonesha wagombea wengi wanakuwa na kauli tamu za kuvutia wapiga kura, lakini wanapofanikiwa kuvipata viti vya mabaraza ya kutunga sheria, wanajisahau na kutumikia nafsi zao badala ya wananchi waliowapa ridhaa.

Kutokana na hali hiyo, Washoto alisema jumuiya yake inakusudia kufanya kongamano litakalowakutanisha wagombea wa nafasi za ubunge, uwakilishi na udiwani wa vyama vyote jimboni humo na wananchi ili kuwe na mjadala wa wazi utakaowawezesha wapiga kura kuwauliza masuala juu ya watakavyotumia nafasi zao kwa maslahi ya wananchi hao.

Alisema kongamano hilo limepangwa kufanyika wakati wowote kuanzia mwisho wa mwezi huu, likilenga kuwapima wagombea hao ili wananchi wajue ni wepi kati yao wenye uwezo na nia thabiti ya kumaliza matatizo yao na kuliletea maendeleo jimbo la Rahaleo.

Alifahamisha kuwa tayari walishakutana na wagombea wa vyama vyote katika nafasi hizo, na kuwaeleza dhamira ya kufanya kongamano hilo ambapo waliafiki na kupongeza hatua hiyo kwa kusema inafaa kuigwa na majimbo mengine.



“Sisi ni jumuiya isiyo ya kiserikali yenye madhumuni ya kuhamasisha maendeleo, tunataka wananchi wazinduke ili watakapochagua wasifanye makosa kama ya nyuma, kwani Rahaleo imekosa msukumo wa maendeleo, tunakusudia kubadilisha hali hiyo” alifafanua.

Washoto alieleza kuwa huu si wakati tena wa kukubali kulishwa maneno ya ‘halua’ ambayo lengo lake ni kuwanasa wapiga kura kwa maslahi ya wachache.

Alisisitiza kauli mbiu ya jumuiya hiyo isemayo ‘Mtu kwanza chama baadae’, akisema wapiga kura wanapaswa kuondokana na dhana ya kubeba vyama vyao hata kama wagombea wao hawana mwelekeo wa kuwasaidia.

Naye Katibu Mkuu wa jumuiya hiyo Kidawa Abdi Khatib, alizitaja baadhi ya sifa ya kiongozi bora kwa mujibu wa katiba ya RADEA, ambazo ni awe na ushirikiano na wanajimbo bila kujali tafauti zao.

Nyengine nia aweze kupima na kupambanua mambo yanayohusiana na maendeleo ya wanajimbo, pia awe na sifa ya utumishi zaidi na sio utashi wa ukubwa na madaraka, anaejalai utu na sio ubinafsi pamoja na kuwa muwajibikaji.

WATOTO VIJIJINI KUUNDIWA "JAMUHURI GARDEN " ZAO.

28/9/2010


Watoto vijijini kuundiwa ‘Jamhuri Garden’ zao



MENEJA wa uendeshaji wa bustani ya Jamhuri Ali Abdallah Ali, amesema wanakusudia kuwapelekea wananchi wa vijiji mbalimbali vya Unguja pembea kwa ajili ya kuwafurahisha watoto walioko huko.

Alisema hatua hiyo inalenga kuwapa fursa watoto wa vijijini ambao hawawezi kufika mjini kwa kufuata pembea zilizoko ‘Jamhuri Garden’, Forodhani au Kariakoo, ili nao wafurahi kama wenzao wa mjini.

Aidha alieleza kuwa kiingilio katika viwanja vitakavyowekwa pembea hizo huko vijijini, kitakuwa kidogo kulinganisha na shilingi 500 zinazotozwa kwa bustani ya Jamhuri.

“Kwa kuwa watoto wote wanahitaji muda na maeneo mazuri ya kupumzika na kucheza, tunaandaa mpango wa kuwasiliana na halmashauri za wilaya mbalimbali kuona namna ya kufanikisha upatikanaji wa viwanja ili tupeleke pembea kwa ajili ya watoto wetu”, alifafanua.

Hata hivyo, hakuweza kusema mpango huo utaanza lini na katika kiijiji gani.

Akizungumzia maendeleo ya bustani ya Jamhuri, Meneja huyo alisema tangu kuwekwa pembea, zaidi ya watu 1000 wengi wao wakiwa watoto, hufika bustanini hapo kila siku ya mwisho wa wiki kwa ajili ya kupanda pembea.

Naye Mstahiki Meya wa Manispaa ya Zanzibar Mahboob Juma Issa, alisema kuimarishwa kwa bustani hiyo kumesaidia kuwapa watoto faraja na kuwa na pahala salama pa kuchezea badala ya kuzurura barabarani na kucheza michezo ya hatari.

Aidha alisema upoteaji wa watoto umepungua sana katika siku za hivi karibuni, kwani wengi wao wakitafutwa huonekana wakicheza katika bustani hiyo jambo alilosema linapunguza wasiwasi wa wazazi na walezi.

DK. SHEIN: NITAJENGA MADARASA ZAIDI MSINGI.SEIKONDARI.

Jumatatu 27 Septemba



Dk. Shein: Nitajenga madarasa zaidi msingi, sekondari


l Wilaya ya kati kujengewa Kituo cha amali


l Barabara zilizobakia nazo kutengenezwa

lKukamilisha usambazaji maji, umeme Shehia zilizobakia

CHAMA cha Mapinduzi (CCM), kimeendelea kupokelewa na wananchi wengi zaidi, katika kampeni zake huku kikiahidi kuwapatia maendeleo makubwa yatayoweza kuleta mabadiliko ya maisha kwa wananchi wa wilaya ya kati Unguja jana, anaripoti MWANTANGA AME.

Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohammed Shein ameahidi hayo jana wakati akitoa sera za Chama cha mapinduzi kwa wananchi wa wilaya hiyo ikiwa ni muendelezo wa kampeni za Chama hicho kwa uchaguzi mkuu wa Oktoba 31, 2010.

Kampeni hizo jana zilifanyika katika Wilaya ya kati Unguja ambayo inayahusisha majimbo matatu likiwemo la Chwaka, Koani na Uzini, yakiwa na shehia 11.

Kampeni hizo zimeendelea kuonesha kuungwa mkono mgombea huyo baada ya makundi ya wanachama wa chama hicho na wananchi, kufurika katika kiwanja cha kampeni hizo Unguja Ukuu na kusababisha barabara ya Mkoa wa Kusini kuzidiwa kwa magari.

Akitoa sera za Chama hicho, Dk. Shein alisema wananchi na wanachama wa CCM wahakikishe wanakipa kura katika uchaguzi Mkuu ujao kwani ikiingia madarakani inakusudia kuendeleza barabara kadhaa za wilaya hiyo pamoja na kuinua sekta ya elimu, Kilimo, uvuvi na sekta ya Afya pamoja na huduma za jamii.

Akichambua mambo anayokusudia kuwamiminia wananchi wa wilaya hiyo, alisema ni pamoja na ujenzi wa barabara za Ukongoroni, Charawe, Ndijani, Jozani, Amani - Dunga, Koani-Jumbi, Kizimbani-Kiboje, Jendele-Cheju, na Njia nne Umbuji hadi Uroa, zitajengwa kwa kiwango cha lami.

Kuhusu sekta ya Afya, alisema Chama cha Mapinduzi kwa wilaya hiyo, inakusudia kuwaongezea ujenzi wa vituo vya afya kwa baadhi ya maeneo ambayo bado hayajawa na vituo hivyo yakiwemo ya kijiji cha Kikungwi kwa kuanzia.

Alisema katika sekta hiyo pia serikali ijayo ya awamu ya saba, itakuwa na mengi ya kuwatekelezea wananchi wa jimbo hilo katika kuandaa mpango mpya wa kuwa na Hospitali ya Wilaya na Mkoa kwa kuipatia vifaa muhimu.

Aidha kazi hiyo itaenda sambamba pamoja na kuweka vifaa vya uchunguzi katika hospitali hizo na kupambana na maradhi mazito yakiwemo ya ugonjwa wa Ukimwi, Malaria na Kifua Kikuu.

Upande wa sekta ya elimu, Dk. Shein aliahidi kuwa akiwa madarakani atahakikisha kunakuwa na mabadiliko katika sekta hiyo kwa kuongeza madarasa ya kusomea ili kupunguza idadi ya wanafunzi katika darasa moja kwa kufikia 40 badala ya hivi sasa kuwa katika idadi ya wanafunzi 60.

Akiendelea alisema katika Skuli hizo ambazo zitajengwa sambamba na nyumba tatu za walimu pia serikali hiyo itajenga skuli mbili za sekondari za wilaya ambazo zitajengwa katika kijiji cha Uzini na Koani, zitakuwa na vifaa vya maabara zitazokuwa za kisasa pamoja na vitabu vya kusomea kwa kila mwanafunzi.

Eneo jengine ambalo amelitaja ni la ujenzi wa Skuli za Amali pamoja na vituocha Elimu Mbadala ambavyo wananchi wa wilaya hiyo wataweza kuvitumia kwa kuongeza viwango vya elimu.





Ccccccccc

UGENI MKONO MARIDHIANO YA CCM, CUF :HAMADI

Ungeni mkono maridhiano ya CCM, CUF: Hamad

MGOMBEA uraisi wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF Maalim Seif Sharif Hamadi amewataka Wazanzibari kuunga mkono maridhiano baina yake, Katibu Mkuu wa CUF na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume ili kuishi kwa umoja na maelewano, anaripoti SHAIB KIFAYA.

Akizungumza katika mkutano wa kampeni wa CUF uliofanyika viwanja vya Kombawapya, Mgombea huyo alisema hatakuwa tayari kuona maridhiano hayo yanachezewa hali ambayo kamwe haitaashiria amani na utulivu.

Alisema jambo muhimu lililobaki hasa katika kuelekea katika uchaguzi mkuu ujao ni kuijenga Zanzibar mpya iliyojaa neema kwa maslahi ya taifa na wananchi wa jumla.

Akizungumzia kuhusu maendeleo ya Zanzibar, Maalim Seif alisema endapo atapewa fursa ya kukikalia kiti cha Urais wa Zanzibar atahakikisha kuwa wananchi wake wanaondokana na kero nyingi zinazowakabili chini ya utawala wa kisheria.

Kuhusu suala la ajira, alifahamisha kuwa Zanzibar mpya itafungua milango ya uwekezaji wa viwanda ili vijana waweze kujiajiri na kufungua masoko katika nchi za nchi kwa lengo la kukabiliana na umasikini nchini.

Aidha ameahidi kuwa serikali atakayoiongoza itakuwa na ushirikiano wa karibu sana na Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kuwahakikishia wananchi wa pande zote mbili maisha ya salama kwa kuondosha kero za Muungano huo.

Alisema ni vyema wananchi wakaishi kwa amani na maridhiano kupitia viongozi wao ambao ndio wanaowategemea kutatua matatizo