Monday 4 October 2010


LEO ikiwa ni siku ya Mitihani ya Taifa ya Kidato cha nne kwa Tanzania nzima, wanafunzi wengi walikua na maandalizi ya mwisho kwa mitihani hiyo,pichani baadhi ya wanafunzi wakiwa katika matayarisho hayo katika bustani ya Jamhuri,kama walivyokutwa na mpigapicha Abdallah Masangu.

KIDATU CHA NNE WAAZA MITIHANI LEO.

Kidato cha nne waanza mitihani leo



Na Mwandishi wetu
4 OCTOBER 2010
MITIHANI ya kidato cha nne inafanyika nchini kote leo huku Baraza la Mitihani la Taifa, NECTA, likiwaondoa watahiniwa 1,376 wa kujitegemea na 1,487 wa skuli.

Wanafunzi hawatafanya mitihani kutokana na kubainika kuwa na kasoro kadhaa zikiwemo kutokuwa na matokeo sahihi ya mtihani wa kidato cha pili.

Taarifa ya NECTA pia imesema watahiniwa 2,124 walioomba kusajiliwa kama watahiniwa wa skuli wamesajiliwa kama watahiniwa wa kujitegemea baaa ya kubainika kuwa hawana sifa za kuwa watahiniwa wa skuli.

Uongozi wa Shirika la Magazeti ya Serikali na wafanyakazi wanawatakiwa wanafunzi wote mitihani mema.

REDIO JAMII TANZANIA KUKUTANA LEO.

Redio jamii Tanzania kukutana Micheweni leo

Na Mwandishi wetu
4 OCTOBER 2010

REDIO jamii kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania, zinakutana Micheweni kisiwani Pemba leo kwa mafunzo ya kuimarisha utendaji wa vituo hivyo nchini.

Taarifa iliyotolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Said Shaaban, imesema kuwa mafunzo hayo yametayarishwa kwa ushirikiano baina ya Wizara hiyo na Shirika la UNESCO.

Said Shaaban ameeleza kuwa Mgeni rasmi katika ufunguzi wa mafunzo hayo atakuwa Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna.

Katibu huyo ameeleza kuwa lengo la mafunzo hayo ni kutekeleza mpango wa kuimarisha vituo vya redio jamii nchini, ambazo zina mchango mkubwa wa kuwaletea maendeleo wananchi wa jamii husika.

Zanzibar hadi sasa ina redio jamii moja iliyo Micheweni, ambayo imewekwa makusudi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), ili kuharakisha maendeleo ya wananchi wa kijiji hicho, ikiwa ni hatua za utekelezaji Mkakati wa Kukuza uchumi na kuondosha umasikini Zanzibar (MKUZA).

Micheweni ni eneo ambalo lilikuwa katika hali mbaya zaidi kiuchumi Zanzibar, ambapo hatua mbalimbali zimechukuliwa na SMZ kuondosha hali hiyo, ambapo sasa ugumu wa maisha umeanza kupungua kwa kuweko miundombinu muhimu kwa wananchi kufanya kazi na kujikomboa.

Wakati wa ufunguzi wa Redio Jamii ya Micheweni, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume, aliahidi maeneo mengine ya Zanzibar yatakuwa na redio kama hizo ili kuharakisha maendeleo yao.

148/= ZATUMIKA IJENZI BUSTANI YA JAMUHURI WELESI.

148m/- zatumika ujenzi bustani ya Jamhuri


Na Halima Abdalla
4 OCTOBER 2010

KIASI cha shilingi milioni 148 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa uzio na uboreshaji wa bustani katika eneo la bustani ya Jamhuri.

Aidha shilingi milioni 48 zimetumika kwa ajili ya kununua mapembea kwa ajili ya kuchezea watoto katika kiwanja hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari Meneja Muendeshaji wa kiwanja hicho, Ali Abdalla Ali, alisema lengo la kutengeneza bustani hiyo ni kuwawezesha watoto kupata fursa ya kufurahia hazi zao za msingi kwa kushirikiriana na wenzao kwa kucheza na kuendeleza michezo ya watoto sambamba na kuimarisha bustani hiyo.

Alieleza kuwa endapo watapatiwa eneo jengine linaloweza kutumiwa kwa malengo kama hayo wako tayari kuliimarisha kwa ajili hiyo.

''Tumeamua kuwekeza katika nchi yetu si lazima kila siku wawekeze watu kutoka nje hata sisi wenyewe tunaweza kuwekeza", alisema.

Nae Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa,Rashid Juma alisema tokea kuboreshwa kwa bustani hiyo kiasi cha vijana 30 wazalendo wameajiriwa kwa shughuli za bustani katika eneo hilo.

Rashid alisema duniani kote watu wameweza kujiletea maendeleo kwa kubadilisha mandhari katika sehemu za kupumzika na wamefanikiwa kiuchumi ikiwemo kupata ajira.

Sambamba na hayo alisema Baraza la Manispaa lina mpango wa kuboresha pia bustani ya Donge, Gofu na maeneo mengine ili kuendana na wakati.

Alisema kuna maendeleo mengi yaliyofikiwa vijana ikiwa ni pamoja na kupungua wimbi la watoto kupotea tokea kujengwa kwa bustani hiyo ambapo watoto wengi wamekuwa wakifurahia kufika hapo na kucheza na wazazo wao kuwafuata baadaye kwa kuwarejesha nyumbani.

Aidha alisema kuwa maeneo ya maegesho ni sehemu nyengin muhimu ambayo inazidi kuupa mji sura ya kuvutia.

''Haya ni mambo mazuri kwa nchi yetu mafanikio mengi tunayo lakini watu hawaoni utakuta mtu anakaa pembeni na kuzungumza bustani imeharibiwa hawaoni haya mafanikio? ", alihoji.

Sambamba na hayo aliwataka wananchi kuyatunza maeneo hayo ili yaweze kudumu na kama kunawatu wengine wa ndani ya nchi wanataka kuwekeza nafasi zipo watapatiwa maeneo mengine.

WASHAURI MAPITIO SHERIA YA WANAOTESA WANYAMA.

Washauri mapitio sheria wanaotesa wanyama


Na Halima Abdalla
4 OCTOBER 2010
SERIKALI imeshauriwa kufanya mapitio ya sheria zinazohusiana na utesaji wanyama kwa nia ya kuwabana watu wanaowatesa wanyama ili iwe fundisho kwa wanaotenda vitendo hivyo.

Ushauri huo umetolewa na Katibu wa Jumuiya ya Taasisi ya Utetezi wa Haki za Wanyama na Utunzaji wa Mazingira (ZSPCA), katika mashindano ya maadhimisho siku ya wanyama duniani yaliyofanyika Kibele, Wilaya ya Kusini Unguja.

Alisema mabadiliko hayo ya kisheria ni muhimu kwa vile inaonekana sheria zilizopo sasa haziwezi kukomesha jambo hilo na badala yake kunahitajika mikakati zaidi kusaidia kuwalinda wanyama na vuguvugu la mateso linalowakumba wanyama hasa Ngombe na Punda.

Aidha, aliitaka jamii kujenga mapenzi na wanyama kwani wao ni viumbe kama binadamu na pia wana hisia kama wengine.

Sambamba na hayo, alisema Jumuiya yao imeanzishwa kwa ajili ya kutetea haki za wanyama na uharibifu wa mazingira.

Hata hivyo, pamoja na kuanzishwa kwa jumuiya hiyo, haki za wanyama bado hazijapewa msukumo mkubwa kwa vile wengi wao wanaandamwa kwa vipigo na kutwishwa mizigo mizito, kupita kiasi.

Jumuiya ya Taasisi ya Utetezi wa wanyama na Utunzaji wa Mazingira imeanzishwa mwaka 2007 ambapo kwa mara ya pili maadhimisho ya siku hiyo na kauli mbiu ya mwaka huu inasema "MAISHA BILA UKATILI KWA WANYAMA INAWEZEKANA"
WANANCHI wa Kjiji cha Mtende Mkoa wa Kusini Unguja wakiangalia ndege ndogo iliotuwa kwa dharura katika barabara ya kijiji hicho ikiwa katika shughuli zake za kufundishia wanafunzi wa kirubani, inayomilikiwa na Kampuni ya Tropicala ya Zanzibar.(Picha na Othman Maulid) 

NDEGE YATUWA KWA DHARURA KIJIJI CHA MTENDE.

Na ISSA MOHAMMED. 
3 OCTOBER 2010 JUMAPILI

NDEGE ndogo imetua barabarani kwa dharura baada ya kupata hitilafu ya mashine yake eneo la Chau nje kidogo ya kijiji cha Mtende wilaya ya kusini Unguja jana.

Akizungumza na Zanzibar leo huko Mtende Meneja Mawasiliano ya Anga Zanzibar, Said Sumry, amesema ndege hiyo ilikuwa ikitumika kwa mafunzo ya urubani.

Alifahamisha kuwa ndege hiyo inayomilikiwa na kampuni ya Tropical Air ilikuwa ikiendeshwa na rubani Keyvan Cazdat, raia wa Iran, aliyekuwa akimfundisha urubani, Abrahman Mohammed, raia wa Tanzania.

Hata hivyo, alisema rubani huyo pamoja na mwanafunzi wake wako salama, ingawa ndege imepata athari kidogo kutokana na kuingia kwenye msingi wenye mawe.

Alisema ndege hiyo iliruka katika uwanja wa ndege wa Zanzibar, Kiembesamaki nje kidogo ya mji wa Zanzibar, saa 3.44 asubuhi, na ilipofika eneo hilo saa 3.55, ilipata hitilafu ikiwa angani, ndipo rubani akaamua kutua barabarani.

Sumry alieleza ndege hiyo yenye namba 5H-TFS aina ya Piper 28-140, kwa kawaida hutumika kuwapa mazoezi marubani wanafunzi katika eneo hilo, kutokana na kutotumiwa na ndege nyingine zinapofanya safari zake za kawaida.

Tukio la ndege kutua barabarani kwa dharura ni la pili katika kipindi cha mwaka huu, ambapo mapema mwaka huu ndege ndogo kama hiyo ilitua katika barabara ya Kiwengwa mkoa wa Kaskazini Unguja.

Pia ndege ndogo ya kampuni hiyo ya Tropical Air iliwahi kuanguka baharini miaka kadhaa iliyopita karibu na kisiwa cha Chumbe, wilaya ya Kusini Unguja, ikiwa na abiria wawili ambao ni mtu na mkewe.

Katika tukio hilo, abiria hao pamoja na rubani walinusurika kifo baada ya rubani kuwavisha abiria wake vifaa maalum vya kuokoa maisha vilivyowawezesha kuelea baharini, kabla ya ndege hiyo kuanguka.

Rubani na abiria hao waliokolewa baada ya kuelea baharini kwa zaidi ya saa 12.

JOTO LA UCHAGUZI OCTOBER 31.

JOTO LA UCHAGUZI OKTOBA 31



Maziko yageuzwa mitaji ya siasa Z'bar


 Vigogo watoa mikono zaidi ya mara mbili kwa watarajiwa


 Wengine wajipitisha pitisha waonekanwe na wapiga kura

Na Khamis Haji
3 OCTOBER 2010
KATIKA hali inayoonekana ni kinyume na mila na taratibu za misiba kwa wananchi wa visiwa vyetu, baadhi ya watu wenye malengo ya kisiasa wameonekana wakiitumia mikusanyiko ya misiba kujinufaisha na kufikia malengo yao kisiasa.

Hali hiyo imebainika kushika kasi zaidi wakati huu wa harakati za uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 31 mwaka huu ambao unaonekana kuwa na ushindani mkubwa miongoni mwa wagombea.

Hivi sasa kampeni za uchaguzi huo zimepamba moto ambapo wagombea pamoja na watu wanaosaka nafasi za uteuzi kutoka kwa viongozi wanaotarajiwa kushika nyadhifa za juu katika serikali ijayo wamekuwa wakitumia kila mbinu kufanikiwa.

Uchunguzi wa gazeti hili uliofanywa kufuatia misiba mbali mbali iliyotokea wakati huu wa harakati za uchaguzi umebaini kwamba wanasiasa wamekuwa makini kufuatilia mikusanyiko hiyo ambayo hujumuisha watu mashuhuri pamoja na wapiga kura wengi.

Uchunguzi huo umegundua baadhi ya wanasiasa hao huwa na harakati kubwa zisizo za kawaida wakati wa mikusanyiko ya misiba hiyo kwa kujipitisha mbele ya viongozi watarajiwa na wapiga kura, kiasi baadhi ya wakati kuonekana kama 'vituko'.

Miongoni mwa misiba hiyo ni ile ya viongozi mashuhuri wa kisiasa, viongozi wa dini, viongozi wa michezo na watu maarufu, waliokwenda mbele ya haki katika siku za hivi karibuni, ambapo wananchi wengi waliweza kuhudhuria kwenye misiba hiyo, wakiwemo viongozi wakuu wa nchi.

Kwa mfano katika misiba hiyo ya wanasiasa na viongozi wa dini pamoja na misiba miwili iliyofanyika katika mtaa wa Mchangani mjini Zanzibar katika kipindi cha wiki mbili zilizopita, baadhi ya watu waliohudhuria walipigwa na mshangao kutokana na tabia waliyoiona kwa baadhi ya wanasiasa hao.

Wanasiasa hao wengi wao ni wale wanaosaka nafasi za uteuzi na wagombea wanaowania nafasi za Ubunge, Uwakilishi na Udiwani, na wamekuwa karibu na kila mtu ambaye wanahisi anaweza kuwa na mchango katika kuwawezsha kufikia malnego hayo.

Kwa upande wengine baadhi ya watu wenye matumaini ya uteuzi kutoka kwa viongozi watarajiwa wamebainika pia kuitumia kikusanyiko hiyo kwa malengo hayo, ambapo wamekuwa mstari wa mbele kusalia viongozi wakuu wa nchi na wagombea hasa wa nafasi ya Urais.

Katika msiba mmoja miongoni mwa iliyotokea katika kipindi hichi cha harakati za uchaguzi, kiongozi mmoja (jina limehifadhiwa) alionekana akiwapiga vikumbo wananchi waliohudhuria katika mkusanyiko, ili kumfikia mgombea mmoja wa Urais kumpa mkono.

Hata hivyo, mara baada ya kiongozi huyo kufanikiwa kumpa mkono mgombea huyo, hakutosheka na kutafuta nafasi nyengine, ili awe kumpa tena mkono, tukio ambalo ilizua udadisi mkubwa miongoni mwa wananchi wengi waliokuwa wakishuhudia hali hiyo ikitokea.

Baadhi ya wazee na watu mashuhuri waliohijiwa na Zanzibar Leo kuhusiana na tabia hiyo walionesha kusikitishwa na hali hiyo na kuielezea kuwa inakwenda kinyume na mila, utamaduni na taratibu za misiba hapa Zanzibar.

Walisema kwamba maziko ni kitu cha kipekee, lakini pia ni sehemu ya ibada, hivyo si vyema kuhusishwa na tamaa za madaraka ya siasa.



"Ni kweli kwenye misiba sasa tunashuhudia wanasiasa wengi, hata wale ambao katika siku zisizokuwa na uchaguzi usingewaona, lakini si katika taratibu zetu kuingiza siasa kwenye masuala ya maziko", alisema mzee Ali Abdallah wa mtaa wa Mlandege.

Baadhi ya wananchi waliozungumzia tabia hiyo walisema kwamba tabia ya kutumia mikusanyiko hiyo kwa tamaa za kisiasa ni kujisumbua bure, kwa vile wapiga kura wanaelewa vigezo vya kuchagua wagombea na sio kujipitisha mbele yao siku za uchaguzi.

Walisema kwamba hata hao viongozi wanaotarajiwa kushika nyadhifa za juu serikalini, pia wanakuwa na vigezo vyao vya uteuzi na sio tu kwasababu mtu anahudhuria sana kwenye misiba na sherehe.

Kampeni za uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31, mwaka huu hivi sasa zinaendelea kwa kasi tokea zilipoanza Septemba 10, baada ya kukamilika kwa mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) sehemu kubwa ya maandalizi ya uchaguzi huo tayari yamekamilika na kwamba vifaa kama vile karatasi za kura zinazochapishwa nchini Afrika Kusini zinaratajiwa kuwasili nchini Oktoba 26.

ZECO WALIOJENGA CHINI YA UMEME MZITO HAWATAUNGIWA.

ZECO: Waliojenga chini ya umeme mzito hawataungiwa
Na Mwanajuma Abdi
3 OCTOBER 2010 JUMAPIL.I

SHIRIKA la Umeme Zanzibar (ZECO), limesema halitowapatia huduma wananchi wataojenga katika maeneo yaliyopita njia kuu ya umeme licha ya kuwa na vibali halali vya ujenzi wa nyumba zao.

Hayo yamesemwa jana na Mwanasheria wa ZECO, Ali Hamad wakati akitoa ufafanuzi katika masuala mbali mbali yaliyoulizwa na waandishi wa habari katika semina ya siku moja, iliyoandaliwa na Shirika hilo kwa vyombo vya habari huko katika ukumbi wa Eacrotanal mjini Unguja.

Alisema kuna baadhi ya wananchi wanaojenga chini ya waya zenye umeme mzito wa 32KV (32,000 voti) na 11KV (11,000 voti) ambao wamewaonyesha vibali halisi vya ujenzi kutoka mamlaka husika.

Alieleza ZECO itaendelea na kuwanyima huduma hiyo licha ya kukosa fedha, lakini pia wanazingatia usalama wa wananchi waliojenga katika eneo hilo.

Aidha alifafanua kuwa, kwa wale wateja waliobahatika kuungiwa umeme katika maneo yaliyopita waya mkubwa watendelea kuwa nayo lakini pia wataendelea kupata madhara ya kiafya.

Alifahamisha kuwa, tayari wameshafanya vikao vya pamoja na mamlaka zinazohusika na utoaji wa viwanja, lakini bado tatizo hilo linaendelea.

Kaimu Mkaaguzi Mkuu wa Ufundi, Khalfan Salum alisema waya huo mkubwa unaathari kubwa kwa binaadamu kwani ndani yake inatoka miozi, ambayo inapenda hadi navu za ubongo.

Alisema kwamba, waya wa umeme 33KV nyumba inatakiwa ijengwe kwa masafa ya mita 50 na 11KV inatakiwa ujenzi wa makaazi yajengwe kwa mita 15 ili kujiepusha na athari ya miozi na madhara mengine ikiwemo vifo vya kuangukiwa na nguzo.

Nae, Kaimu Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme, Hassan Ali Mbarouk alisema ZECO, limeandaa mkakati wa kuwapatia huduma ya umeme wateja wapya kwa mwezi mmoja badala ya kukaa kwa muda mrefu kusubiri huduma hiyo.

Alieleza huduma hiyo wakipatiwa wateja hao watawekewa mita za TUKUZA, ambazo zimeonekana wateja wanazifurahia zaidi kuliko mita za kawaida katika kuzitumia.

Mbarouk alisema mikakati mengine ni kuzifanyia tathmini na kuzipima transfoma 500 za Unguja ili kujua uwezo wake kuwahudumia wateja, sambamba na kuondoa umeme mdogo katika baadhi ya maeneo.

Shirika la Umeme Zanzibar linawaateja 87,000 Zanzibar, ambapo kati ya hao wateja 73,000 wapo Unguja na kati ya hao 26,000 wanatumia mita za TUKUZA na Pemba mita hizo zimefikia 5,000 kwa sasa na 9,000 ni mita za kawaida.

PBZ YAAHIDI KUSAMBAZA ATM KILA KONA.

PBZ yaahidi kusambaza ATM kila kona



Na Zulekha Saleh
3 OCTOBER 2010, JUMAPILI

BENKI ya watu wa Zanzibar PBZ imesema kuwa ina mipango ya kueneza huduma ya ATM, katika maeneo yote ya Tanzania ili wateja wake waweze kuchukua fedha popote waliopo.

Katika kusambaza huduma hiyo PBZ, inatarajia kufungua vituo vyengine zaidi katika maeneo ya Mlandege kwa Unguja,Chake chake,Wete na Mkoani kwa Pemba.

Akitoa maelezo hayo Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo Juma Amour alisema wanatarajia kufungua vituo vyengine Tanzania bara ili huduma ya hiyo iweze kuenea Tanzania nzima.

''Tuna mpango wa kufungua vituo Tanzania nzima hadi Tanzania bara ili wateja wetu wote wafaidike na huduma hii'', alisema.

Aidha PBZ ina mpango wa kutoa vipeperushi ambavyo viko katika matayarisho vitakuwa vikitoa maelekezo yanayoelekeza jinsi ya kutumia huduma hiyo.

''Katika kuelekeza namna ya kutumia huduma hii tunatayarisha vipeperushi ambavyo vitakuwa vikielekeza namna ya kutumia huduma hiyo,''alifafanua.

Kadi ya SPICE inayotolewa na Benki ya watu wa Zanzibar ambayo inamuwezesha mteja wa Benki hiyo kupata huduma za ATMs zilizounganishwa na mtandao wa 'Umoja Swich'popote pale Tanzania.

Mteja yeyote wa Benki ya watu wa Zanzibar mwenye akaunti ya akiba au ya biashara anaweza kupata kadi ya SPICE kwa kiwango kidogo cha pesa.

VYOMBO VYA HABARI VIMEVICHA SAUTI ZA WANAWAKE KWENYE KAMPENI.

Vyombo vya habari vimeficha sauti za wanawake kwenye kampeni



Na Ramadhan Makame
3 OCTOBER 2010., JUMAPILI.
UTAFITI uliofanywa na taasisi ya Synovate ya kuvitathmini jinsi vyombo vya habari vinavyoripoti harakati za uchaguzi, umebainisha kuwa vyombo hivyo viko mbali na haviwapi nafasi wagombea wa kike.

Akiwasilisha matokeo ya utafiti huo kwa vyombo vya habari vya Zanzibar, Meneja wa taasisi hiyo Aggrey Oriwo alisema vyombo hivyo vimeziweka mbali sauti za wagombea wa kike ilinganishwa na wale wa kiume.

Alisema mara nyingi vyombo hivyo vimekuwa vikiwaripoti kwa kuwatambulisha wanawake kama wake wa wagombea.

"Sauti za wanawake hazipo kwenye kampeni, zinasikika wakitambulishwa kama wake wa wagombea",alisema meneja huyo.

Alisema wagombea wa kile waliosimama kwenye majimbo kuomba nafasi mbali mbali kupitia vyama tofauti hawapewi nafasi ya kujieleza wenyewe ikilinganishwa na wanaume jambo ambalo si haki.

Aidha utafiti huo wa Synovate, ulibainisha kuwa vyombo vya habari za Zanzibar kwa kiasi kikubwa vinakipendelea zaidi chama cha Mapindizi kwa kuripoti habari zake ilinganishwa na vyama vyengine.

Meneja huyo alisema chama hicho tawala kimejizolea asilimia 40 pekee huku vyama vilivyobaki vikigawana asilimia 60 ilioyobakia.

Utafiti huo pia ulibainisha mada zilizopewa umuhimu kwenye kampeni hizo ambapo vyombo vingi vimekuwa vikiandika habari zenye kusisitiza amani katika visiwa hivi.

Mada nyengine zilizoripotiwa kwa wingi ni pamoja na suala la elimu,afya kilimo, ajira na haki za binaadamu huku mada ya ufisadi ikiwa haijapewa umuhimu na vyombo vya Zanzibar ikilinganishwa na bara.

Matokeo ya utafiti huo yalitolewa kwenye semina ya siku moja iliyofanyia Zanzibar Beach Resort, ambapo waandishi waliuponda utafiti huo wakisema haki haikutendeka.

Waandishi hao walihoji njia zilizotumika kupatikana matokeo hayo hasa madai ya kukibeba chama cha Mapinduzi, huku vyama vya upinzani vikishindwa kutumia nafasi ya bure iliyowekwa katika vyombo vya uma.

DK. SHEIN AIVAMIA NGOME YA CUF PEMBA.

Dk. Shein aivuruga ngome ya CUF Pemba



Wana CUF Kusini Pemba wasema ndiye chaguo lao


Na Suleiman Rashid, Pemba

2 OCTOBER 2010HALI si shuwari kwa wafuasi wa CUF wa mikoa miwili ya Pemba ambao inadaiwa kuwa mvutano unaokaribia kukipasua chama hicho ambacho kiko kampenzi wa kuwania utawala wa nchi.

Habari kutoka kisiwani humo zinaeleza kuwa wafuasi wa chama hicho wa Mkoa wa Kusini na Kaskazini Pemba, wamekuwa wakivutana kila mmoja kutaka mzawa wa Mkoa huo apewe ridhaa ya kuongoza Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu.

Wafuasi wa chama hichi Mkoa wa Kusini Pemba, wanamekuwa kwenye kampeni ya kutaka mgombea wa CCM, Dk. Ali Mohammed Shein apewe ridhaa ya kuiongoza Zanzibar ambaye anatokea mkoa huo.

Kwa upande wa mkoa wa Kaskazini, wafuasi wa chama hicho nao wanavuta upande wao wakitaka kura zote apewe Seif Sharif Hamad ambaye ni mzawa wa kijiji cha Mtambwe kilioko mkoa huo.

Mvutano huo wa chini kwa chini unadaiwa kuibuka mara tu baada ya Halmashauri Kuu ya CCM kumpitisha, Dk. Ali Mohammed Shein kuwania kiti cha Urais wa Zanzibar kupitia chama hicho.

Baada ya CCM kulipitisha jina hilo wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba ambap wengi wao ni wafuasi wa CUF, wamekubwa na hisia kali na damu kuwachemka kwa kuunga mkono Dk. Shein aliyezaliwa Chokocho.

Mpasuko huo ambao upo wazi wazi ambapo huku uchaguzi mkuu ukikaribia ufa wake unazidi kuonekana ingawaje hakuna mwasiasa aliyekuwa tayari kueleza hali hiyo.

Uchunguzi uliofanywa na muandishi wa habari hizi, umegundua kuwa wananchi wa Mkoa Kusini Pemba wamekuwa hawashabikii sana huku hamasa waliyonayo huko nyuma kwa chama cha CUF ikishuka kama ilivyozoeleka.

“Ngoja nikwambie wewe angalia katika mikutano ijayo ukiacha huu wa ufunguzi hakutakuwa na watu wengi kama ulivyozea, ila usije sema nimekwambia", alisema mzee mmoja alilieeleza gazeti hili.

Kauli ya mzee huyo ilithibitika wiki iliyopita pale Maalim Seif Sharif Hamadi aliposhindwa kuzungumza na kuahirisha mkutano katika uzinduzi wa kampeni kwenye kiwanja cha Banda Taka ambapo

Baadhi ya wakaazi wa Chokocho kijiji alicho zaliwa Dk. Shen walio zungumza na Gazeti hili walisema ingawa wao niwafuasi wa Chama cha wanachi, lakini mara imewachanganya kwani damu nzito kuliko maji.

“Unajua siasa ni siasa na familia ni familia inapo bidi siasa unaweka pembeni unafinya jicho unagugumia mmm unaokoa familia” alisema moja wa mkazi wa Mkanyageni alie jitambulisha kwa jina la Malim Shali.

Alisema walivyojipanga wao rais wa awamu ya saba atakayeviongoza visiwa vya Zanzibar atatoka Chokocho jambo ambalo litakipa heshima kijiji hicho.

MAENDELEO YA CCM KWA KILA MTU --- MAMA SHEIN.

Maendeleo ya CCM kwa kila mtu - Mama Shein



Mwandishi Maalum – Zanzibar

2 OCTOBER 2010
MKE wa Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi Mama Mwanamwema Shein, amesema amani na utulivu uliopo nchini ni matokeo ya utekelezaji wa sera nzuri za Chama cha Mapinduzi.

Mama Shein hayo alipokuwa akizungumza na kikundi cha SACCOS cha wavuvi wa Chaza wa wilaya ya mjini katika ukumbi wa EACROTENAL mjini Unguja.

Aliwaomba wanawake wa kikundi hicho kuichagua CCM katika uchaguzi mkuu ujao kwani ndio chama chenye uwezo na uhakika wa kuendeleza amani, umoja na mshikamano visiwani Zanzibar.

“Bila amani na utulivu akina mama tunahangaika…hata kazi zetu hizi za maendeleo za kuvua chaza hazifanyiki”, alisema Mama Shein.

Alitumia fursa hiyo kuwahimiza wanawake visiwani humo kujiunga kwenye vikundi ili iwe rahisi kwao kupata mikopo kwa ajili ya kuimarisha shughuli zao za kiuchumi.

Aidha, akizungumza na akina mama wa Mpendaye, mjini Unguja Mama Shein alibainisha wazi kuwa serikali ya CCM iliyoko madarakani imefanya mengi na wala haibagui katika kuwaletea maendeleo wananchi wake na hivyo kuwaomba waipigie kura CCM kwa maendeleo.

“Serikali ya CCM iliyoko madarakani imejenga barabara, maskuli, vituo vya afya, imeimarisha hospitali zetu. Watu wote wanapita kwenye barabara hizo, wanatibiwa kwenye vituo hivyo, watoto wanasoma kwenye skuli hizo. CCM haibagui, maendeleo ni kwa kila mtu…hivyo naomba mzitie kura nyingi kwa CCM,” alidokeza Mama Shein.

VIFAA VYA KURA KUWASILI MWISHONI MWA MWEZI.

Vifaa vya kura kuwasili mwishoni mwa mwezi


Na Mwantanga Ame
2 0CTOBER 2010

TUME ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), imesema vifaa vya kupigia kura kwa uchaguzi mkuu utaofanyika mwishoni mwa mwezi huu vitawasili nchini Oktoba 26.

Afisa Uhusiano wa ZEC, Idrisaa Haji Jecha alisema hayo alipokuwa akizungumza na Zanzibar Leo huko Afisini kwake Maisara mjini Zanzibar.

Alisema vifaa vyote vitakavyotumika kwenye uchaguzi mkuu zikiwemo karatasi zitawasili nchini sikui huyo vikitokea nchini Afrika Kusini ambako ndoko viliko tengenezwa.

Aidha lifahamisha kuwa kwenye vifaa hivyo pia Tume inakamilisha kupata vifaa muhimu vitavyowawezesha kupiga kura kwa watu wasioona kumudu kupiga kura wenyewe bila ya kupata msaada wa mtu mwengine.

Alisema Tume imelazimika kuchukua hatua hiyo baada ya baadhi ya wapiga kura katika Jumuiya ya Wasioona kulalamikia kuandaliwa mazingira yatayowawezesha kupiga kura bila msaada wa mtu mwengine.

Alisema ingawa Jumuiya hiyo haikuwasilisha malalamiko yao hayo rasmi kwa tume ya uchaguzi, lakini Tume imeyapokea kupitia vyombo vya habari jambo ambalo imelizingatia na kulifanyikazi.

Alisema hapo awali Tume ilishindwa kutoa tamko juu ya suala hilo kwa vile walikuwa wakisubiri kukamilika kwa mchakato wa zoezi la uchukuaji fomu ili kupata wagombea halisi kwa ajili ya kuandaa karatasi za kupigia kura.

Alisema kupatikana kwa vifaa vitakavyowawezesha watu wasioona kupiga kura itakuwa jambo la msingi ambapo walemavu hao wataweza kuwatambua wagombea hao.

Afisa huyo alisema kazi kubwa ambayo wanatarajia kuifanya baada ya kuwapatikana kwa kifaa hicho ni jinsi ya kuwapa elimu walemavu hao ili waweze kutambua namna ya kukitumia wakati uchaguzi utakapowadia.

USTAWI WA JAMII KUYAPATIA UFUMBUZI MATATIZO YA WAZEE.

Ustawi wa Jamii kuyapatia ufumbuzi matatizo ya wazee

Na Fatma Kassim, Maelezo

2 OCTOBER 2010 
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, imesema kuwa inazitambua vyema shida na matatizo yanayowakabili wazee, huku ikiyafanyiakazi bila ya kuwabagua.

Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ustawi wa Jamii, Ahmed Awadh alieleza hayo alipokuwa akizungumza na wazee katika maadhimisho ya siku ya wazee duniani yanayoadhinishwa kila ifikapo Oktoba Mosi.

Alisema matatizo yanayowakabili wazee ni mengi ambayo yamegawika katika makundi tofauti, yakiwemo yanayowakumba wafugaji, wakulima, na wastaafu mara baada ya utumishi kumalizika na serikali bado inathamini mchango wao walioutoa katika taifa.

Alifahamisha kuwa juhudi zaidi zinafanywa ili kuhakikisha kundi hilo katika jamii yanasaidiwa ili yaweze kuondokana na matatizo yao.

Aidha alisema kutokana na umuhimu wa wazee serikali inatoa kipaumbele masuala mazima ya kuwapatia hifadhi ikiwamo makaazi bora sambamba na huduma muhimu.

Nao wazee hao wamesema kutokana na kupanda maisha na mahitaji yanaongezeka wameomba kuongezewa posho lao la mwezi kufikia 50,000 pamoja na kupatiwa huduma muhimu.

Mapema Mwenyekiti wa kamati ya ufundi wa jumuiya ya wastaafu Zanzibar (JUWAZA), Aboud Talib alisema wazee wana mengi wanayoyahitaji yakiwemo huduma za afya, makaazi bora pamoja na kupewa posho ambalo litatua matatizo yao.

TAMWA YALAANI UDHALILISHAJI WAGOMBEA WANAWAKE.

TAMWA yalaani udhalilishwaji wagombea wanawake


Na Muandishi Wetu
2 october 2010

WAGOMBEA wanaume ambao wanatoa lugha za matusi kwa wagombea wanawake majimboni, wanadhihirisha kutokuwa na hoja wala sera za maendeleo na hivyo wanastahiki kunyimwa kura.

Hivi karibuni baadhi ya wanaume ambao wanaona wagombea wanawake ni tishio kwao, wamekuwa wakiwaundia mbinu chafu ikiwa ni pamoja na kuwakejeli na kuwadhalilisha kwa matusi.

Wanawake kadhaa wanaogombea Ubunge majimboni wamelalamika kuwa baadhi ya wanaume wapinzani wao wamekuwa wakiwatukana na kuwakejeli baada ya kubaini kuwa wagombea hao wanawakake wanakubalika zaidi yao.

Miongoni mwa majimbo ambayo wagombea wanaume wamelalamikiwa kutumia lugha za matusi dhidi ya wagombea wanawake ni pamoja na jimbo la Kawe, Dar es Salaam na Kwimba mkoani Mwanza.

Sheria ya kanuni ya adhabu ya mwaka 2002, kifungu cha 89 kifungu kidogo cha kwanza (a) kinasema kuwa mtu yeyote akitoa lugha ya matusi kwa mtu mwingine ni kosa na adhabu yake ni miezi sita jela.

Kutokana na hali hiyo Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), kimewaonya wanaogombea uongozi mwaka huu kupitia vyama vyote vya siasa, na kueleza kuwa Watanzania wameelimika na zama za kuwanyanyasa wanawake na kuwanyima haki ya kuwa viongozi zimepitwa na wakati.

Katika taarifa ya Chama hicho iliyoasaini na Mkurugenzi Mtendaji Ananilea Nkya, ilieleza kuwa wagombea wanaume ambao bado wana mitazamo potofu dhidi ya wanawake, wajitoe kwenye uchaguzi kwani Watanzania wamechoka kuvumilia udhalilishwaji wa wanawake.

Nkya alisema Watanzania wanachohitaji ni mtu mwenye sifa za uongozi awe mwanamke au mwanaume bila kujali ameoa au kuolewa kutokana kuwepo watu wengi waliooa na kuolewa lakini hawana uadilifu katika ndoa zao.

Jumla ya wanawake 190 wanagombea Ubunge Majimboni mwaka huu wakiwepo 25 CHADEMA, 24 CCM, 15 NCCR Mageuzi, CUF 14 , UDP 14, UPDP 14, TADEA 12, DP 11 na UMD 10. Waliobaki wanagombea kupitia vyama vya NLD, NRA, SAU, TLP, Jahazi Asilia, Makini, Chausta, APPT-Maendeleo na AFP. Kadhalika wanawake 557 wanagombea udiwani majimboni.
BAADA ya kuimarika kwa Bandari ya Malindi mjini Zanzibar meli kubwa za mizingo za kubebea makontena zikifunga katika bandari hiyo(Picha na Abdalla Masangu)

Sunday 3 October 2010

DANGURO JENGINE LAVUMBULIWA MALINDI.

Danguro jengine lavumbuliwa Malindi

Na Waandishi Wetu
1 october 2010.
WIKI chache baada ya uchunguzi wa Zanzibar Leo kubaini kuuzwa chakula mchana wa Ramadhani eneo liliyopo pembezoni ya soko la samaki Malindi mjini hapa, kadhia nyengine mpya ya ufuska imeibuka katika eneo hilo.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa eneo hilo ambapo kuna banda linalomilikiwa na shirika moja limegeuzwa kuwa danguro.

Kwa mujibu wa vyanzo mbali mbali vya habari vilivyohojiwa na gazeti hili vimeeleza kuwa danguro hilo linaendeshwa na mtu mmoja anayejulikana kwa jina maarufu Jiti.

Bwana huyo amekuwa akiendesha shughuli za matendo machafu katika eneo hilo ambapo amekuwa akichukua makahaba maarufu wa kiume kutoka sehemu mbali mbali hapa nchini.

Baadhi ya wafanyabiashara wa samaki walilieleza gazeti hili kuwa wamechoshwa na vitendo hivyo vilivyo kinyume na maadili vinavyofanywa na mtu huyo ambaye amekuwa tishio.

"Tumefurahi sana leo mmekuja kuzitafuta habari hizi, hili eneo lina habari nzito unaliona hilo banda hapo, hilo si banda bali ni danguro la makahaba wa kiume wanaoingizwa na kufanya vitendo vichafu",alieleza mmoja kati ya wafanyabiashara katika eneo hilo.

Alifahamisha kuwa baadhi ya watu wanaokuja kufanywa mambo hayo kwenye danguro hilo, hutolewa nje ya Zanzibar.

Mmoja wa maofisa wa shirika hilo ambaye hakutaka jina lake litajwe alithibitisha kuwepo kwa vitendo hivyo kwa muda mrefu sasa.

"Mbona haya mambo yapo zamani watu wote wanajua, cha kushangaza hata baadhi ya askari polisi katika vituo vya karibu wanajua kinachoendelea kwenye banda hilo", alisema Afisa huyo.

Afisa huyo alishindwa kutoa maelezo zaidi juu ya kadhia ya matendo machafu yanayoendelea kwenye eneo hilo, akisema kuwa yeye si msemaji na haelewi kama Shirika lake limempa eneo hilo Jiti.

Aidha katika eneo jengine lililopo karibu na eneo hilo ambalo linajulikana kwa jina maarufu la Kwamapaka ambako nako kuna mabanda nako kunaendeshwa biashara ya ngono kwa madada poa.

Mbali ya shughuli hizo za ngono pia eneo hilo limekuwa likifanyika biashara haramu ya dawa za kulevya.

Sheha wa Shehia ya Malindi, Himid Omari alilithibitishia gazeti hili kuwa anazo habari za kuendelea kwa matendo hayo machafu kwenye shehia yake.

Saturday 2 October 2010

WANAHABARI KUWENI MAKINI KUFANIKISHAUCHAGUZI -- JAJI MSHIBE

Wanahabari kuweni makini kufanikisha uchaguzi – Jaji Mshibe

Na Ramadhan Makame, 1 Oktoba 2010

HUKU Taifa likikaribia kuingia katika uchaguzi mkuu, waandishi wa habari wametakiwa kuwa makini kuiepusha nchi kuingia kwenye machafuko.

Jaji wa Mahakama Kuu wa Zanzibar, Mshibe Ali Bakari alieleza hayo katika hoteli ya Zanzibar Beach Resort alipokuwa akifungua kongamano la siku moja lililoelezea dhima ya vyombo hivyo katika uchaguzi.

Jaji Mshibe alisema endapo vyombo vya habari na waandishi wa habari watateleza na kuruhusu kufanya makosa vinaweza kuiweka nchi katika hali mbaya ya mifarakano na ghasia.

Mshibe alisema kalamu za waandishi zikitumika vyema zitaweza kufanikisha kuiepusha nchi kuingia kwenye machafuko ambapo yakitokea yataweza kumuathiri kila mtu.

“Machafuko yanapotokea hayachagui kila mtu ataathirika hata wewe mwenyewe uliyeandika habari hiyo nawe utakwenda na mafuriko”,alisema Jaji Mshibe.

Aidha alisema kinachohitajika kwa waandishi na vyombo vyao katika kipindi hichi kuacha kuripoti mambo yenye maslahi yao binafsi sambamba na kulipendelea kundi fulani.

“Nchi imepita katika kipindi kigumu, jamani andikeni mambo yanayohusu watu sio mambo yenu binafsi ambayo yanaweza kuiweka nchi katika pahali pabaya”.

Akitoa mada katika semina hiyo, Mhadhiri wa Chuo cha Uandishi wa Habari IJMC, Ayoub Rioba alisema vyombo vya habari vina wajibu wa kuandika habari za usawa, kutompendelea mtu sambamba na kuzichambua habari mbali mbali ambazo zitasaidia uelewa kwa wananchi.

Naye Mwandishi wa habari kutoka nchini Afrika Kusini Wellington Radu, akielezea uzoefu wa kuripoti habari za uchaguzi, alisema vyombo vya habari nchini humo wakati wa uchafuzi hutoa taaluma ambayo huwawezesha wananchi kufahamu mambo mbali mbali juu ya uchaguzi.

Wakichangia kwenye semina hiyo waandishi wa habari Zanzibar, walitaja vikwazo kadhaa wanavyokabiliana navyo wakati wa kuripoti masuala ya uchaguzi.

Semina hiyo ya siku moja imeandaliwa na MISA-Tan na kufadhiliwa na shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Washiriki katika mkutano huo walikuwa ni pamoja na waandishi wa habari waandamaizi, wahariri, wamiliki wa vyombo vya habari, viongozi wa vyama vya siasa na taasisi zisizo za kiserikali.