Tuesday 1 March 2011

Zanzibar yaikuna Uswissi

Zanzibar yaikuna Uswissi


Rajab Mkasaba, Ikulu

USWISSI imesema kufanikiwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye muundo wa Umoja wa Kitaifa kunatokana na juhudi zilizochukuliwa na serikali kwa kuwaelimisha mapema wananchi wake juu ya mfumo huo.

Balozi wa Uswissi nchini Tanzania, Adrian Schlapfer alisema hayo jana alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Balozi Schlapfer alitoa pongezi kwa Dk. Shein pamoja na wananchi wa Zanzibar kwa kufanikisha uchaguzi kwa amani na utulivu na hatimae kuundwa kwa Serikali ambayo imepata mafanikio kwa kuanza kazi vizuri.

Alisema hatua iliyofikiwa na Zanzibar kufanikisha Serikali hiyo na kuanza kuleta maendeleo inatokana na elimu ya kutosha iliyotolewa kwa wananchi juu ya serikali yao kabla na baada ya uchaguzi mkuu uliopita.

Balozi huyo alisema Zanzibar imejijengea heshima na sifa kubwa kitaifa na kimataifa kutokana na kufanya uchaguzi uliokuwa huru na haki.

Alisema miongoni mwa mambo yaliyochangia kufanikiwa kwa serikali ni pamoja na kuwepo kwa suala zima la utawala bora.

Katika maelezo yake hayo, Balozi Schlapfer alisema Uswissi inathamini uhusiano na ushirikiano wa kidugu uliopo kati ya nchi hiyo na Zanzibar na kuahidi kuimarisha zaidi uhusiano huo kwa manufaa ya pande zote mbili.

Alisema Uswissi itaendelea kuunga mkono miradi ya maendeleo Zanzibar na kueleza lengo la serikali yake la kuanzisha mradi maalum wa afya.

Balozi huyo alisema azma ya kuanzisha mradi huo ni kwa ajili ya kuimarisha sekta ya afya.

Akieleza juu ya sifa na haiba ya Zanzibar katika sekta ya utalii, Balozi huyo alieleza kuwa visiwa vya Zanzibar vimejaaliwa kuwa na vivutio vingi vya kitalii pamoja na ukarimu wa wananchi wake kwa wageni.

Alisema kutambulika na kukua kwa sekta ya utalii kumeweza kupanua soko la ajira ambapo baadhi ya wataalamu wa huduma za utalii kutoka nchini mwake wapo Zanzibar wakifafanya kazi katika hoteli za kitalii.

Kwa misingi hiyo alisema nchi yake ina nafasi nzuri ya kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo na kuahidi kuitangaza Zanzibar kiutalii nchini mwake.

Nae Dk. Shein kwa upande wake alimueleza Balozi huyo kuwa ushirikiano na uhusiano uliopo kati ya Zanzibar na Uswissi umeweza kutoa mchango mkubwa katika kuimarisha maendeleo nchini.

Dk. Shein alimueleza Balozi Schlapfer kuwa Uswissi imekuwa mdau mzuri wa maendeleo ya Zanzibar kwa kuweza kuunga mkono sekta mbali mbali zikiwemo elimu, kwa kutoa nafasi za masomo pamoja na sekta nyenginezo.

Alisema azma ya Uswissi ya kuanzisha mradi maalum wa sekta ya afya utaweza kusaidia juhudi za serikali katika kuimarisha sekta hiyo ambayo ni muhimu katika maendeleo ya wananachi na kufikia malengo ya Mkakati wa Kupunguza Umasikini na Kukuza Uchumi Zanzibar (MKUZA).

Dk. Shein alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Afya itahakikisha inatoa mashirikiano ya karibu zaidi kwa lengo la kuhakikisha mradi huo unafanikiwa.

Akizungumza juu ya mafanikio ya kisiasa yaliopatikana, Dk. Shein alisema amani, utulivu, mshikamano na umoja wa Wazanzibari ndio uliopelekea kufanyika uchaguzi ulio huru na haki.

Alieleza kikubwa kinachohitajiwa na Wazanzibari hivi sasa ni maendeleo, hivyo juhudi za pamoja zitaendelea kuchukuliwa kwa kuhakikisha Zanzibar inapata maendeleo zaidi.

Dk. Shein alitoa pongezi kwa nchi kwa mashirikiano yake pamoja na misaada inayotoa kwa Zanzibar pamoja na kutoa shukurani zake kwa nchi hiyo kwa kushiriki vyema katika uangalizi wa uchaguzi mkuu uliopita.

Alisema hatua hiyo imeitia moyo Zanzibar na kuweza kujitambua kuwa ina nafasi katika kujiletea maedneleo endelevu na kuendeleza amani na utulivu uliopo.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo Zanzibar ni sehemu moja wapo ya uwekezaji hivyo inawakaribisha waekezaji kutoka nchini humo kuja kuekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii, uvuvi na sekta nyengine muhimu

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo haja ya kuimarisha uhusiano wa kielimu kwa vyuo vikuu vya nchini humo na vile vya Zanzibar kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA).

Rais Kikwete ziarani Ufaransa

Rais Kikwete ziarani Ufaransa



Na Mwandishi maalum, Dar

RAIS wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete ameondoka nchini jana kuelekea Paris, Ufaransa kushiriki mkutano wa Kimataifa wa Tasnia ya Uziduaji yaani Global Extractive Industries Transparency Initiative –EITI.

Katika mkutano huo Rais Kikwete atatoa mada juu ya umuhimu wa shughuli za uziduaji na uwazi katika mapato ya madini.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Kurugenzi ya mawasiliano Ikulu,mkutano huo wa siku mbili unaonza leo una malengo ya kuongeza uwazi na uwajibikaji katika mapato yatokanayo na uchimbaji madini, mafuta na gesi asilia.

Tanzania iliomba na kupewa uanachama wa muda wa EITI tangu mwaka 2009.

Hata hivyo, itaweza kupata uanachama kamili baada ya kuwa imekamilisha na kutimiza vigezo vya kuwa mwanachama kamili na kuweka misingi ya utoaji taarifa hizo muhimu kwa umma juu ya malipo ya kodi kutoka makampuni mbalimbali yaliyopo nchini.

Lengo kuu la kujiunga na EITI ni kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia kwa kutangaza hadharani malipo yanayotokana na rasilimali zake kwa manufaa ya wananchi.

Utaratibu huo utaweka uwazi na kuondoa usiri ambao unaweza kuwa mwanya wa kuficha mapato halisi ya makampuni husika.

Baada ya kumaliza mkutano huo, Rais Kikwete ataelekea Nouakchott, Mauritania kwa ajili ya kikao cha Marais wa Afrika wanaotafuta suluhisho la mgogoro wa kisiasa wa Ivory Coast.

Akiwa Mauritania, Rais Kikwete atajiunga na marais wa Mauritania, Afrika Kusini, Burkina Faso, Chad, Nigeria na Equatorial Guinea pamoja na wawakilishi wa Jumuia ya Uchumi ya Afrika Magharibi (ECOWAS), Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AU) Balozi Jean Ping na Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa (UN).

Katika kikao hicho, viongozi hao watafikia uamuzi wa AU kuhusu mzozo huo na kupendekeza namna gani ya kuutatua mzozo huo ulioripuka baada uchaguzi mkuu wa mwezi Novemba mwaka uliopita.

Matokeo yake, nchi hiyo imegawanyika katika sehemu mbili, moja ikimuunga mkono aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Alassane Quattara na nyingine ikimuunga mkono Rais aliyekomadarakani Laurent Gbagbo.

Kila mmoja kati ya wanasiasa hao amejitangaza kuwa rais na kila mmoja ameunda na kutangaza serikali katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Wiki iliyopita, viongozi hao wa Afrika walikutana mjini Nouakchott na baadaye wakaenda Abidjan, Ivory Coast ambako walikutana na viongozi hao wawili nchini humo katika jaribio la kutafuta suluhisho la mzozo huo.

Dk. Bilal akutana na ujumbe kamati ya Bunge la Afrika Mashariki

Dk. Bilal akutana na ujumbe kamati ya Bunge la Afrika Mashariki



Mwandishi Maalum, Dar


MAKAMU wa Rais Dk. Mohammed Gharib Bilal amesema Bunge la Afrika Mashariki lina wajibu wa kuhakikisha kuwa ndoto ya wananchi wa ukanda huo ya kutaka kuundwa kwa Shirikisho la Afrika Mashariki inatimizwa.

Dk. Bilal ameyasema hayo jana alipokutana na mazungumzo Kamati ya Uongozi ya Bunge la Afrika Mashariki ikiongozwa na Spika wa Bunge hilo ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati Abdirahin Abdi ilipomtembelea Ikulu, Jijini Dar es salaam.

Dk. Bilal aliuambia ujumbe wa kamati hiyo kuwa shirikisho litakapoundwa wananchi watakuwa na uhuru zaidi wa kuwekeza popote pale katika nchi hizo kutokana na ukweli kwamba bado watakuwa wamewekeza ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki.

“Kama utawekeza Rwanda, Tanzania, Burundi utakuwa umewekeza kwenye ukanda wa Afrika Mashariki. Hivyo hivyo kwa Kenya na Uganda,” alisema na kuongeza “lazima mjenge matumaini kuwa mtafanikiwa. EU ilichukua miaka mingi lakini mwishowe shirikisho limeundwa.”

Akizungumza kwa niaba ya kamati, Spika Abdi alielezea umuhimu wa kuwa na mfumo unaolingana wa elimu ya juu kwa nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hali ambayo itasaidia kuwawezesha wahitimu kuwa na elimu yenye ubora na viwango vinavyofanana na hivyo kuwa rahisi kwao kupata ajira.

Akizungumzia hoja hiyo Makamu wa Rais alisema iwapo kutakuwa na muundo unaokubalika kikanuni ni jambo jema kwa vile kuwa na mfumo unaolingana utawawezesha wanafunzi wanapohama kutoka nchi moja kwenda nyingine kuendelea na masomo yao kama kawaida chini ya kanuni na taratibu zilizopo.

“Tukiwa na muundo unaokubalika kikanuni, haitaleta shida kwa wanafunzi wa elimu ya juu wanapohama kutoka nchi moja kwenda nyingine. Kwa mfano mwanafunzi anaweza kusoma mwaka wa kwanza Dar es salaam, mwaka wa pili akaendelea Nairobi na mwaka wa tatu labda Rwanda. Inakubalika na hakuna atakayelaumu kiwango cha elimu,” alidokeza Dk. Bilal

Kamati hiyo ilifika Ikulu kwa lengo la kumwelezea Makamu wa Rais jinsi inavyoendesha shughuli zake katika kuhakikisha nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zinapiga hatua zaidi ya kimaendeleo.

Spika wa Bunge hilo alitumia fursa hiyo pia kuipongeza serikali na wananchi wa Tanzania kwa kufanya uchaguzi mkuu wa mwaka jana kwa amani na utulivu na pia kutoa pole kufuatia janga la miripuko ya mabomu ya hivi karibuni iliyotokea katika kambi ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) 511 KJ Gombo la Mboto, Dar es salaam.

NGOs nyingi hazijasajiliwa

NGOs nyingi hazijasajiliwa

Na Kauthar Abdalla


UCHUNGUZI unaonesha Jumuiya nyingi za vijana (NGOs) ama hazijasajiliwa au hazina hesabu za benki hali ambayo inazifanya zishindwe kuendesha shughuli zao na kufaidika na miradi inayotolewa na taasisi mbali mbali.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, katika ukumbi wa Salama hoteli ya Bwawani, vijana wengi wamesema Jumuiya zao hazijasajiliwa kutokana na kile walichokieleza kuwepo kwa urasimu katika taasisi zinazohusika na masuala ya usajili wa NGOs.

Amesema hali hiyo inazifanya NGOs kufanya kazi bila ya kuwa na miradi mikubwa kwa kuwa masharti ya kupata fedha pamoja na mambo mengine yanazitaka Jumuiya kuwa na cheti cha usajili na hesabu ya benki.

Aidha tatizo jengine ambalo linazikabili NGOs nyingi ni kutokuwa na ripoti za fedha za mwaka zilizofanyiwa ukaguzi, lakini pia matumizi mengi yamekuwa yakifanywa bila ya kuwepo stakabadhi halali.

Akizungumza na vijana katika mkutano maalum wa kuwafahamisha jinsi ya kuandika michanganuo ya kuomba fedha, Katibu Mkuu Wizara ya Ustawi wa Jamii, Maendeleo ya Wanawake na Watoto, Rahma Mshangama, amewataka vijana kuandika miradi itakayokidhi vigenzo vinavyotakiwa na wafadhili ili waweze kuingiziwa fedha.

Alisema vijana wafanye upembuzi yakinifu wa kuandika miradi bora ambayo itajikita katika kulikomboa kundi la vijana na ambayo itakuwa na ushawishi wakati itakapopitiwa na wafadhili.

Alisema lengo la mfuko wa vijana ambao umeanzishwa hivi karibuni ni kulikomboa kundi kubwa la vijana, ambalo limekuwa likikabiliwa na umaskini, ukosefu wa ajira, utumiaji wa dawa za kulevya na maambukizi ya virusi vya ukimwi.

Alisema vijana wanapaswa kufahamu kwamba michanganuo itakayokidhi vigenzo ikiwa ni pamoja na akaunti za benki, cheti cha usajili na ripoti ya matumizi ya fedha iliyofanyiwa ukaguzi ndiyo itakayopatiwa msaada wa fedha hizo.

Mkutano huo uliwashirikisha mamia ya vijana kutoka maeneo yote ya Unguja na mwengine kama huo utafanyika kisiwani Pemba.

Februari 20, serikali ya Norway ilitangaza kuupatia mfuko wa vijana Zanzibar msaada wa dola za Marekani 100,000 ambazo ni sawa na shilingi milioni 144 ili kusaidia ukombozi wa kundi hilo.

Fedha hizo zitatolewa kwa zile NGOs za vijana zitakazowasilisha miradi itakayokidhi vigenzo chini ya usimamizi wa Shirika la Makazi la Umoja wa Mataifa, UN-HABITAT.

Kiwango cha chini cha ufadhili kwa Jumuiya hizo ni dola za Marekani 5,000 na kiwango cha juu ni dola 30,000 ambazo zitatolewa mara moja kwa mwaka.

Wanafunzi wa kike wasimamishwa masomo kwa kuweka nywele dawa

Wanafunzi wa kike wasimamishwa masomo kwa kuweka nywele dawa

Na Ismail Mwinyi

WANAFUNZI wa darasa la saba na kitado cha pili katika skuli ya Kijitoupele wilaya ya Magharibi Unguja, wamesimamishwa masomo baada ya kukutwa na makosa ya kutia dawa nywele na kujitia vipodozi usoni.

Hatua hiyo imekuja kufuatia mzazi mmoja wa mwanafunzi kuwa na wasiwasi kwa mtoto wake kutokana na mabadiliko aliyokuwa nayo.

Akizungumza na gazeti hili, Msaidizi wa Mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo, Makame Hana Ali, alisema hivi sasa wanafanya upekuzi kwa wanafunzi wa kike kwa sababu wanafunzi hano ni wakorofi zaidi.

Alisema wamewarudisha nyumbani wanafunzi hao kwa ajili ya kuwaeleza wazazi wao ili waje kulizungumza suala hilo kwa pamoja na walimu na kulipatia ufumbuzi unaofaa.

Hana alisema wanafunzi waliorejesha nyumbani 20 ambao wote wanahusika na kufanya makosa hayo kinyume na utaratibu wa skuli.

Alisema opereshini hiyo ni ya kudumu na ambayo itafanyika kila baada ya mienzi sita ambapo wanafunzi wa kike watafanyiwa ukaguzi ili kuhakikisha makosa hayo yanatoweka kabisa katika skuli hiyo.