Wednesday 9 June 2010

Hii ndio bajeti yenu wananchi

WAZIRI wa Nchi Afisi ya Rais Anayeshughulikia Uchumi na Fedha, Dk. Mwinyihaji Makame akionyesha mkoba wenye bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 2010/2011

Jinamizi lagubika uhakiki wanachama CCJ

Na Mwanajuma Abdi
CHAMA cha Jamii (CCJ), kimezidi kukumbwa na jinamizi kwenye zoezi la uhakiki wa wanachama wake hapa Zanzibar, baada ya wanachama na wafuasi wa chama hicho Mkoa Kusini Uinguja kuingia mitini.

Chama hicho kiko kwenye hatua za kuhakikiwa wanachama wake na Afisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, ili kiweze kupata usajili wa kudumu.

Katika harakati za usajili huo, uliofanyika jana atika Mkoa wa Kusini Unguja, mwanachama mmoja tu ambae ni Naibu Katibu wa CCJ, Zanzibar, Ali Khatib ndie pekee alijitokeza kuhakikiwa na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, Rajab Mbaraka.
 
Naibu Msajili huyo aliikagua nambari ya kadi ya mwanachama huyo ambayo ilikuwa ni Na. 3910, na kubaini kuwa ni halali, baada ya kuangalia fomu zake.
 
Naibu katibu huyo wa CCJ alipotakiwa na Naibu Msajili kuwapeleka wanachama wake wakasajiliwe alikataa kata kata.

Naibu katibu huyo wa CCJ, alsiema Chama chake kimeshampelekea barua kwa Afisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, kusitisha zoezi la uhakiki huo kwa sasa hadi hapo baadae.
 
“Makao makuu ya Chama changu yaliyopo Dar es Salaam yameshaniagiza kuwa zoezi la uhakiki limesitishwa, hivyo hakuna haja ya kuendelea kufanyiwa uhakiki na ratiba zinazopangwa na Msajili ni zake mwenyewe”, alisisitiza Ali Khatib.
 
Alisema katika Mkoa wa Kusini anawanachama 231 lakini kutokana chama chake cha CCJ, kuamua kusitisha zoezi la uhakiki hajaweza kuwapa taarifa wanachama wake wala kutoa taarifa kwa Sheha na Polisi kwa vile hakuna uhakiki kwa sasa.
 
Mapema Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, Rajab Mbaraka, alionana na Mkuu wa Wilaya ya Kusini Haji Makungu Mgongo, ambapo alimwambia hana taarifa ya kufanyika kwa uhakiki wa chama CCJ jana.
 
Zoezi la uhakiki wa chama hicho ulipangwa kwa Mikoa minne kwa awamu ya kwanza lakini katika mikoa yote hiyo, wanachama wameshindwa kujitokeza, huku wale waliojitokeza wamekumbwa na utata wa uanachama wao.
 
Hata hivyo, Rajab alisema baada ya kukamilisha zoezi hilo jana wanategemea kufanya tathmini ili kuangalia kama wataendelea na zoezi hilo katika mikoa sita iliyobakia au ndio basi.

Thursday 3 June 2010

Ndiyo nazindua umeme

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Amani Abeid Karume akibonyeza kitufe kuashiria ufunguzi rasmi wa umeme wa gridi ya Taifa huko kisiwani Pemba, umeme huo umetandikwa waya kutoka Tanga hadi kisiwani humo.(Picha na Zanzibar Leo).
  

Ndiyo tumepata umeme Pemba

MKE wa Rais wa Zanzibar Shadya Karume, akiteja jambo na maofisa wa ubalozi wa Norway nchini Tanzania, ambao walihudhuria uzinduzi wa umeme kisiwani Pemba. (Picha na Zanzibar Leo).

Mawaziri wengi SMZ wapania kurudi majimboni

Na Mwantanga Ame
IKIWA zimebakia siku chache kabla ya kuanza zoezi la uchukuaji wa fomu kuwania nafasi za Ubunge, Uwakilishi na Udiwani ndani Chama cha Mapinduzi (CCM), Mawaziri kadhaa wametangaza nia ya kujitosa tena majimboni.

Vigogo hao, wameelezea nia zao katika mahojiano na gazeti hili kwa wakati tafauti na kuthibitisha kuwa watajitosa kwa mara ya kwanza kuwania majimboni katika uchaguzi Mkuu ujao huku wengine wakiwa ni wakongwe wanaoendelea kuyashika majimbo hayo.

Wa kwanza kuthibitisha kuingia kwenye mchakato huo ni Waziri wa Nchi Afisi ya Rais anayeshughulikia Fedha na Uchumi, Dk. Mwinyihaji Makame ambaye alieleza wazi kuwa anajitayarisha kutetea Jimbo analoliongoza hivi sasa la Dimani.

Waziri Mwinyihaji, ameliambia gazeti hili kwamba atahakikisha anachukua fomu kwa ajili ya kuomba tena ridhaa za wananchi wa Jimbo hilo bila ya wasiwasi.

Alisema anafanya hivyo akiamini kuwa wapo wanachama wengine wa CCM pia wameweka nia kama hiyo lakini bado kwake haijawa kikwazo kwa sababu kila mtu ana haki hiyo.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Afisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma, ambaye ni Mwakilishi wa Kwamtipura, alieleza kuwa nia ya kutaka kuwania nafasi ya Uwakilishi katika Jimbo hilo bado anayo kwa vile umri unamruhusu kufanya hivyo.

Alisema bado ana ushirikiano mkubwa na wananchi wa Jimbo hilo huku kukiwa na mambo ambayo yanamhitaji kuyafanyia kazi hapo baadae.
 
Alisema kujitokeza kwa idadi yoyote ya wananchi watakaoingia kwenye Jimbo hilo, hakumpi ugumu kwa vile hakuna mwenye hatimiliki ya Jimbo na hilo ni jambo wazi katika kucheza na demokrasia, akiamini kuwa kipindi chake amekitumia vizuri.
 
Kuhusu mchakato wa upigaji kura za maoni, ambao utafanyika wakati yeye akiwa bado na majukumu mengi serikalini, Waziri Hamza alisema hilo ni linaweza kumpa uzito kwa vile muda uliotangazwa na Chama chake kuanza kwa mchakato huo utaingiliana na shughuli za Bajeti ya Zanzibar.
 
“Nimo katika kujipanga kwani katika kipindi hichi kutakuwa na mambo mengi ambayo yatanihitaji niyafanye likiwemo la kupiga kura ya maoni ya CCM, kufanya kampeni zangu, kushiriki mikutano ya bajeti, na kura ya maoni ya Tume ya Uchaguzi” alisema Waziri huyo.
 
Katika hatua nyengine, Waziri wa Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto, Asha Abdalla Juma, akizungumza na mwandishi wa habari hizi, alisema yeye bado anatafakari kama ajitokeze kuwania nafasi katika Jimbo alilozaliwa la Dimani au la.
 
Waziri Asha alisema ameamua kuchukua hatua hiyo kwa kile alichosema wasiwasi wa kuwepo uwezekano wa kupatikana kwa asilimia ndogo ya wagombea wanawake kwa vile bado anaona nguvu ya wanaume katika uchaguzi ujao ipo juu.

Alisema licha ya CCM kutoa ofa ya kuwataka wanawake kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi za uongozi katika majimbo, bado huenda wanawake wasipewe.

Waziri huyo alifahamisha kwa vile tayari kuna wanawake wengi ambao wameanza kuonesha nia ya kutaka kuwania katika majimbo ni vyema Chama kikahakikisha kinatimiza ahadi yake.
 
Hata hivyo, Waziri huyo aliwataka wanawake kutovunjika moyo na badala yake wajitokeze kwa wingi kuchukua fomu katika majimbo yao.

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Mazingira, Burhani Sadat Haji, alishatangaza mapema nia yake ya kuwania Jimbo la Kikwajuni akisema bado uwezo wa kulitumikia anao.

Kiongozi mwengine ambaye alishawahi kuelezea nia ya kutaka kuwania Jimbo ni Naibu Waziri Kiongozi na waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna kwa kuetetea Jimbo lake la Donge baada ya kuelezea nia hiyo mbele ya wananchi wa Jimbo hilo.

Licha ya baadhi ya viongozi kuelezea nia hizo hadharani, bado wapo ambao hawajajitokeza kutoa kauli hizo kwa maelezo mbali mbali na huenda idadi ya wanachama wenye nia kama hiyo ikaongezeka kadri muda unavyokwenda mbele.
 
Wanaotajwa ni pamoja na Waziri wa Maji, Ujenzi Nishati na Ardhi, Mansoor Yussuf Himid, anaelishikilia Jimbo la Kiembe Samaki, Waziri wa Utalii, Biashara na Uwekezaji, Samia Suluhu Hassan kwa tiketi za Wanawake Wilaya ya Kusini.

Wakati kundi hilo la Mawaziri likijitayarisha tayari pia kuna kundi la Makatibu Wakuu na Wakurugenzi ndani ya serikali ya SMZ nao huenda wakajitokeza kuwania baadhi ya majimbo katika uchaguzi Mkuu ujao.

Mkurugenzi wa Idara ya Maafa Zanzibar, Waride Bakari Jabu, amelihakikishia gazeti hili katika mahojiano maalum kuwa nia ya kuwania nafasi ya Ubunge katika Jimbo la Kiembe Samaki katika uchaguzi Mkuu ujao anayo na wakati wowote atatangaza rasmi.

Waride alisema ameamua kuchukua uamuzi huo ikiwa ni sehemu ya demokrasia yake huku Chama cha Mapinduzi kikiwa kimesisitiza wanawake wajitokeze kuwania nafasi za uongozi katika Majimbo.

Licha ya Mkurugenzi huyo pia wapo Makatibu Wakuu kadhaa ambao watajitokeza katika kuwania nafasi za kuomba kuteuliwa majimboni.

Makatibu Wakuu hao wengi wao wanatajwa wana nia ya kuomba kuteuliwa katika Majimbo ya Vijijini kwa Unguja na Pemba.
 
Watachukua hatua hio baada kutekeleza sheria ya uchaguzi, ya mwaka 1984 kifungu cha 45(1) (a) kinachoeleza kuwa endapo uchaguzi Mkuu umepangwa kufanyika siku ya uteuzi kwa Jimbo lolote haitakuwa chini ya siku tano au zaidi ya siku ishirini na tano baada ya kuvunjwa Baraza la Wawakilishi.

Kutokana na kifungu hicho cha sheria tayari Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imetangaza ratiba ya uteuzi wa kwa nafasi za wagombea wa Urais, Uwakilishi na Udiwani kazi ambayo inatarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 3, 2010 na uchaguzi kufanyika Oktoba 31, mwaka huu.

Tume hiyo imefahamisha zoezi la uchukuaji wa fomu kwa nafasi ya urais wa Zanzibar litaanza Septemba 10, 2010 na Septemba 15 ni kwa ajili ya wagombea nafasi za Uwakilishi na Udiwani.

Mambo ya umeme Pemba


Umeme ufungue milango uwekezaji Pemba

Na Mwandishi Wetu, Pemba
KUPATIKANA kwa umeme wa uhakika kisiwani Pemba, kufungue milango ya uwekezaji kisiwani humo katika sekta mbali mbali ikiwemo viwanda vidogo vidogo na viwanda vya kati, pamoja na kuwataka wazalendo kujitokeza kuwekeza badala ya kuwaachia wageni peke yao.

Hayo yalielezwa jana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume, alipohutubia wananchi katika uzinduzi wa Mradi wa umeme wa uhakika Zanzibar, uwanja wa Gombani kisiwani Pemba jana.

Alieleza kukamilika Mradi huo ni kukamilisha malengo ya Mapinduzi ya Januari 1964 ya Zanzibar na ilani ya uchaguzi ya CCM ya 2000-2010, zinazoeleza wazi umuhimu wa kuwajengea mazingira mazuri ya maendeleo wananchi wake, ili waweze kufaidika na rasilimali za nchini kwao.
 
Alisema Zanzibar imepiga hatua kubwa ikilinganishwa na nchi nyingi za Afrika, ambapo imefikia asilimia 82 ya wananchi wake mijini na vijijini wanapata umeme wa uhakika na inatarajia kufikia asilimia 90 mwaka 2012.

Alisema umeme huo utasaidia kurahisisha upatikanaji wa elimu bora kwa watoto, kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa miundombinu ya sekta hiyo kuimarika.

Aliwataka wananchi wa Zanzibar kujiamini na kutumia uwezo wao wa hali na mali, kwani wakijiamini watafikia maendeleo makubwa zaidi.
 
Dk. Karume aliishukuru Serikali ya Norway kwa kutoa msaada mkubwa uliofanikisha kukamilika Mradi huo.
 
Norway imetoa dola milioni 71 kufadhili Mradi huo, ambao umebadilisha historia ya kisiwa hicho na Zanzibar kwa jumla kwa upande wa nishati ya umeme, ambapo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ilichangia dola milioni 10 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT), ilichangia dola milioni 5.
 
Aidha alizishukuru kampuni za NEXAN za Norway ambayo ndiyo iliyojenga mradi huo, kampuni ya ADC ya Sweden kwa kusaidia vifaa vya mradi huu, pamoja na kutengeneza hitilafu za kukatika umeme kisiwani Unguja, pamoja Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mkuu wa Mkoa wa Tanga na Mkuu wa wilaya ya Tanga.

Akizungumzia uchaguzi mkuu wa Oktoba 2010, Rais Karume aliwataka wananchi kuungana na kwenda katika uchaguzi kwa kuimarisha umoja, amani na utulivu, ili kujenga Zanzibar yenye amani na maendeleo.

Aliwapongeza wananchi wote wa Zanzibar kwa mchango wao wa dola milioni 10 kufanikisha Mradi huo, pamoja na ndugu zao wa Tanzania Bara kwa kuchangia dola milioni tano na kuutaja Mkoa wa Tanga kutokana na kutoa ushirikiano mkubwa kwa vile umeme huo umeunganisha kutokea huko.

Akitoa salamu za nchi yake, Balozi wa Norway nchini Tanzania, John Lomoy, alisema kuzinduliwa kwa Mradi huo ni kielelezo cha uhusiano mwema na ushirikiano baina ya nchi yake na Zanzibar na Tanzania kwa jumla.

Akizungumza kwa kiswahili alisema maamuzi ya wananchi wa Norway kusaidia Mradi huo ni kuelewa umuhimu wake kwa wananchi wa Zanzibar,
 
Mbali ya hotuba sherehe hizo ambazo wananchi walifurika katika uwanja wa Gombani, zilipambwa kwa utenzi na ngoma za utamaduni.

Akitoa taarifa za kitaalamu kuhusiana na Mradi huo, Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Ujenzi Nishati na Ardhi, Mwalimu Ali Mwalimu, alisema kabla ya umeme huo wa uhakika Pemba ilikuwa ikipata umeme kwa kutumia majenereta.

Alisema Mradi huo utaokoa mamilioni ya fedha za dizeli na matengenezo ya zilizokuwa zikitumika kwa majenereta ya kuzalisha umeme Pemba.

Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi, Mansoor Yusuf Himid, alisema kuwezekana kwa Mradi huo kumetokana na juhudi na ujasiri mkubwa wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume, aliyelifungia kibwebwe suala la umeme wa Pemba.

"Nataka niwahakikishie wananchi wenzangu kwamba bila ya uongozi imara wa Rais Karume, Mradi huo usingefikia mafanikio yaliyopo sasa" alisisitiza Mansoor.

Aidha alimtaja Meneja Mradi wa umeme Vijijini Zanzibar kutoka Norway, Rodrigue, ambae kwa kushirikiana na Rais ndiyo waliobuni na kusimamia Mradi huo kwa nguvu zao zote hadi kukamilika kwake.

Aidha alisema Mradi huo ni wa kipekee kwani waya wake umetandikwa katika kina kirefu zaidi cha maji cha Kilomita moja ya kina cha maji cha bahari na umbali wa Kilomita 78 kutoka Tanga hadi Pemba na pia Norway haijawahi kufadhili Mradi kama huo barabi Afrika na kuwa wa kipekee kwa kutumia teknolojia ya kisasa zaidi kwa Afrika na duniani ni wa kipekee.

Mbali ya umeme pia waya huo uliotandikwa chini ya bahari unatoa huduma ya mawasiliano kupitia 'fibre' maalum, hivyo kuifanya Pemba kupiga hatua kimawasiliano kama dunia za mwanzo' First world'.

Sherehe hizo pia zimehudhuriwa na Mke wa Rais Mama Shadya Karume, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Ali Mohammed Shein, Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna, Mawaziri viongozi wastaafu, Ujumbe kutoka Norway, Mawaziri na viongozi wa Serikali na vyama vya siasa.