Thursday 4 August 2011

MARUFUKU KUINGIZA BIDHAA ZA MIGAMBA KUTOKA BARA.

Marufuku kuingiza bidhaa za mgomba kutoka Bara

Na Nafisa Madai, Maelezo
WIZARA ya Kilimo Maliasili imepiga marufuku uingizaji wa bidhaa zinazotokana mgomba ikiwemo ndizi, miche ya migomba, majani ya migomba pamoja vigogo vya mgomba kutoka Tanzania bara.
Akitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari huko ofisini kwake Mwanakwerekwe wiliya ya Magharib, Mkuu wa Kitengo cha Uhifadhi na Utibabu wa mazao Zainab Salim Abdallah, alisema marufuku ya kuingizwa kwa bidhaa hizo inafuatia kuibuka maradhi mnyauko.
Alisema maradhi hayo yanayosababishwa na bakteria yamekuwa yakiathiri migomba pamoja na mazao yake ambapo kizuizi kilichowekwa kinalenga kuiepusha Zanzibar kukumbwa na maradhi hayo.
Mkuu huyo alisema Tanzania bara imekumbwa na maradhi hayo tangu mwaka 2007, ambapo kama Idara inalazimika kuchukua hatua ya kuzuia hasa katika kipindi hicho cha mwezi wa Ramadhani kutokana na walaji ndizi kuongezeka kuliko siku za kawaida.
Zainab alisema kuwa maradhi ya mnyauko hayamuathiri mlaji wa ndizi bali athari kubwa anaweza akaipata mkulima wa migomba endapo bidhaa hiyo kwani itamsababishia hasara kubwa mkulima huyo kwa asilimia 100.
Aliwaomba Wazanzibari kutoa mashirikiano katika kutekelezwa kwa ahizo hilo ili kuepusha kusambaa kwa maradhi hayo kwa migomba ya Zanzibar.
Zainab alisema mtu yoyote atayekamata anaingiza bidhaa hiyo kutoka bara atafikishwa katika vyombo vya sheria na sheria itashika mkono wake kwa muingizaji huyo.
Alisema kitengo chake tayari kimeshakamata ndizi amabazo zimebainika na maradhi hayo kutoka bara na mipango inaandaliwa kuziangamiza ndizi hizo ili iwe fundisho kwa wengine ambao wanampango wa kuingiza ndizi Zanzibar.
Akizungumzia nzi wa matunda alisema nzi hao hivi sasa wameshamiri sana visiwani hapa na wamekuwa wakishambulia embe kwa kiasi kubwa jambo ambalo limekua likiwavunja moyo wakulima wa zao hilo.
Aidha alisema nzi hao ambao chimbulo lake Indonesia wamekua wakileta hasara kubwa kwa wakulima kwani soko limekua dogo sana ikilinganisha na hapo awali.
Hata hivyo alisema juhudi zinafanywa za kuangamizwa nzi hao za kuwawekea mitego maalum na kwasasa tayari wameanza katika wilaya ya Kusini na wamefanikiwa kwa aslimia hamsini ambapo zoezi hilo linategemewa kufanya katika mikoa yote ya Zanzibar.
Akizungumzia mende wadogo ambao nao wameshamiri kwa wingi katika visiwa vya Unguja, alisema mende hao wanaathiri sana katika makaazi ya watu kwani hushambulia nguo na vitu vyengine majumbani.
Amesema kuwa mende hao wametokea ulaya na wamekuja kutokana na vifaa vya umeme vinavyoingizwa na ambavyo vimezagaa katika Manispaa ya mji wa Zanzibar.
Aidha alisema juhudi za makusudi zinachukuliwa za kutokomeza mende hao maarufu mende wa Ulaya, na kuwaasa wale wote wanafanya biashara hiyo ya vifaa vilivyokwisha tumika kuangalia kwa makini vifaa hiyo kwani athari yake baadae inaweza kuwa kubwa zaidi.

No comments:

Post a Comment