Monday 29 March 2010

UNICEF kuendeleza program kuchapuza huduma Z'bar

Na Rajab Mkasaba, Ikulu

SHIRIKA la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia maendeleo watoto (UNICEF) limeeleza azma yake ya kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wakiwemo akinamama na watoto.

Mwakilishi Mkaazi wa UNICEF anayemaliza muda wake Heimo Laakkonen, aliyasema hayo Ikulu mjini Zanzibar alipozungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Amani Abeid Karume jana.

Laakkonea alimueleza Rais Karume kuwa UNICEF inajivunia hatua za maendeleo zilizofikiwa Zanzibar hasa katika uimarishaji wa huduma za jamii zikiwemo za afya.

Alieleza kuwa kutokana na hatua hiyo UNICEF itaendelea kuiunga mkono Zanzibar kwa kuendeleza programu mbali mbali ambazo zitaongeza kasi za huduma ya afya kwa watoto hapa nchini.

Aidha Laakkonea alieleza kuwa uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya UNICEF na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ni mkubwa ambao umemsaidia katika utendaji wake wa kazi katika kipindi chote alichofanya kazi nchini Tanzania.

Rais Karume kwa upande wake alitoa shukurani kwa niaba ya wananchi wa Zanzibar kutokana na ushirikiano na misaada mbali mbali inayotolewa na UNICEF.

Alisema UNICEF imekuwa mstari wa mbele kusaidia uimarishaji wa huduma za kijamii zikiwemo huduma za afya kwa watoto na akina mama.

No comments:

Post a Comment