Friday 26 March 2010

Watendaji watakaochelewasha malipo kwa wadai kukiona



Na Mwantanga Ame
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema kwamba Watendaji wa Serikali wataochelewesha malipo kwa wadai wa serikali sasa watakiona baada ya sheria mpya iliyopitiwa na Baraza la Wawakilishi kutiwa saini na Rais.

Waziri wa Nchi, Afisi ya Rais anaeshughulikia Fedha na Uchumi Dk. Mwinyihaji Makame, aliyasema hayo jana wakati akitoa ufafanunuzi wa hoja mbali mbali za Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakati wakijadili mswada huo katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Alisema mswada wa sheria ya kuweka Haki na Wajibu wa Serikali katika kesi za madai na utaratibu wa mwenendo wa madai dhidi ya serikali na mambo mengineyo hauna lengo la kumkomoa mtu yeyote ila upo kwa ajili ya kuleta uwajibikaji wa utawala bora.

Waziri huyo alisema serikali imeamua kuandaa sheria hiyo kuhakikisha utawala bora unazingatiwa katika pande zote na haina nia ya kuwakomoa wananchi kwani serikali imekuwa ikipata hasara inayotokana na uzembe wa watendaji kulipa madeni .

Alisema ndani ya mswada huo kuna vipengele kadhaa vitakavyowawajibisha watendaji wa serikali ambao kwa makusudi huchelewesha kufanya malipo ya wadai jambo ambalo sasa litakuwa na kikomo kwa vile sheria hiyo imeelezea kuwawajibisha wazembe hao.

“Kuna maafisa wa serikali wamekuwa wakihangaisha watu katika kulipa madeni yao licha ya kuwa serikali inawaingizia fedha hizo, lakini hawalipi na huendekeza matakwa binafsi jambo linaloibebesha serikali mzigo mkubwa wa madeni”, alisema Waziri huyo.

No comments:

Post a Comment