Friday 5 March 2010

UMEME KUREJEA ZANZIBAR MACHI 9

Umeme kurudi machi tisa

SHIRIKA la Umeme Zanzibar (ZECO), limesema matengenezo ya urejeshaji wa huduma ya umeme katika kisiwa cha Unguja yanatarajiwa kukamilika Machi 7, 2010 na wananchi wataipata huduma hiyo kuanzia Machi 9, 2010.
Kaimu Meneja wa Shirika la Umeme Zanzibar, Hassan Ali Mbarouk, aliyaeleza hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari katika kituo cha kupokelea umeme Fumba Wilaya ya Magharibi Unguja.
Kabla ya maelezo ya Kaimu huyo Zanzibar Leo ilishuhudia mafundi wa Kampuni ya Elmeridge Cable Services, EHT Cables ya Afrika Kusini, ambao ni washauri, Kampuni ya Nexans ya Norway ambayo ni wasimamizi wa kazi hizo wakisaidiana na wataalamu wazalendo wakiendelea na kazi katika kituo hicho.
Akitoa maelezo Kaimu huyo alisema kwa asilimia kubwa kazi za urejeshaji wa huduma ya umeme zipo katika hatua ya mwisho baada ya wataalamu hao kuanza kuunga vipande vya waya unaotoka baharini na kuingia katika kituo cha kupokelea umeme cha Fumba.
Alisema kazi hiyo imeanza jana baada ya kujitokeza tatizo katika zoezi la awali la kuunganisha waya huo kulikosababishwa na mafuta kuchafuka.
Alisema kuchafuka kwa mafuta hayo ndiko kulikosababisha kuongezeka kwa muda wa kurejesha huduma hiyo ndani ya Mwezi Februari, ambapo hapo awali ulikadiriwa kungekuwa na uwezekano katika kipindi hicho.
“Tulisema Februari 20 lakini likajitokeza tatizo la kuchelewa kufika kwa vifaa na wakati vifaa viliwasili pia muda wa pili wa ndani ya mwezi Februari haikuwezekana tena kutokana na kuchafuka kwa mafuta wakati tukiendelea na kazi” alisema Kaimu Meneja huyo.
Alisema walilazimika kujipa muda zaidi kutokana na wataalamu hao kutaka kufanya vipimo vipya kwa vile isingewezekana kutumika kwa mafuta hayo na yangeliweza kuleta athari katika kazi hiyo.
“Tumelazimika kulifanya hilo kwa vile waya huu hauhitaji kupata unyevunyevyu hata kidogo kwani ungeweza kuleta athari nyengine”, alisema Kaimu huyo.
Kutokana na hali hiyo Kaimu Meneja huyo alisema tayari hivi sasa sehemu kubwa ya matengenezo hayo yameanza kukamilika ambapo uwekaji waya unaotoka baharini katika viungo hivyo itachukua muda wa siku tatu.
Alisema baada ya kukamilisha kazi hiyo Wataalamu hao Machi 4, 2010, wanatarajiwa kwenda katika kituo cha kupokelea umeme kutoka Ubungo Dar es Salaam, cha Ras -Kiromoni kumalizia hatua za mwisho za kuunga pampu za mafuta.
Meneja huyo alisema kazi hiyo itafanywa kwa muda wa siku moja na Machi 5, 2010, wataalamu hao wataendeleza kazi katika kituo cha Fumba Wilaya ya Magaharibi Unguja kwa kukamilisha kazi ndogo ndogo.
Alisema kazi kamili za matengenezo hayo zinatarajiwa kukamilika Machi 7, 2010, na Machi 8, 2010 wataalamu hao watafanya vipimo vya mafuta yatayoambatana na kazi za majaribio katika kituo cha Ras Kiromoni, Fumba na Mtoni.
Kutokana na ratiba hiyo Kaimu Meneja huyo alisema huduma hiyo kwa upande wa wananchi inatarajiwa kurejea kuanzia asubuhi ya Machi 9, 2010 ambapo wananchi watapaswa kuanza kuchukua tahadhari ili kuepuka kutokea athari wakati huduma hiyo ikirejea.
Hata hivyo Kaimu Meneja huyo aliendelea kuwaomba radhi wananchi kutokana na kuongezeka kwa muda wa kurejeshewa huduma hiyo kulikosababishwa na matatizo ya kitaalamu.
“Tunaendelea tena kuwaomba radhi wananchi, tunajua usumbufu unaowapata lakini isingewezekana kufanya haraka kisha tukaharibikiwa zaidi ya vile jambo ambalo lingesababisha kuchukua muda zaidi tunawaomba radhi tena” alisema Kaimu Meneja huyo.
Viunganishi vilivyowekwa katika waya huo ‘Joint’ vina uzito wa tani 1.7 ikiwa ni pamoja na kubadilishiwa mfumo wa upokeaji umeme katika kituo cha Ras Kiromoni Dar es Salaam pamoja na Fumba Wilaya ya Magharibi Unguja.
Mabadiliko hayo yanakuja baada ya kuharibika kwa kifaa kilichokuwa kikitumika kupokelea umeme katika kituo cha Fumba aina ya ‘Spliter’ kuungua na kusababisha huduma ya umeme kukosekana kuanzia Disemba 10, 2009.

No comments:

Post a Comment