Monday 29 March 2010

Jela miaka saba kwa kubaka mototo wa miaka mitatu

Na Omar Hassan, Pemba
MAHAKAMA ya Mkoa wa Chake Chake, Pemba imemuhukumu kutumikia chuo cha mafunzo Muhammed Maganga Sebastian (25) mkaazi wa Vikunguni Chake Pemba kwa muda wa miaka saba baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka na kumsababishia maumivu mtoto wa miaka mitatu.

Akitoa hukumu hiyo Hakimu Haji Omar wa mahakama hiyo, alisema kuwa ametoa hukumu hiyo baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakamani, pia iwe fundisho kwa mshtakiwa na watu wengine wenye tabia ya kuwaingilia watoto.

Mapema akisomewa shitaka lake na mwendesha mashtaka wa Serikali Ali Bilali, alidai kuwa Aprili 14 mwaka 2009 saa 1:30 asubuhi huko Magome Vikunguni, Wilaya ya Chake chake, Mkoa wa Kusini Pemba, mshtakiwa Mohammed Maganga alimuingilia kwa nguvu mtoto wa miaka mitatu, jina linahifadhiwa.

Mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo kinyume na kifungu 125 (1) (2) (e) na 126 (1) cha sheria namba 6 ya mwaka 2004 sheria za Zanzibar.

Kesi hiyo imeanza kutajwa katika Mahakama ya Chake chake April 23 mwaka jana na kutolewa hukumu hiyo juzi.

No comments:

Post a Comment