Monday 29 March 2010

Wazanzibari wachoshwa na mifarakano- Wawakilishi

Mwanajuma Abdi

WAJUMBE wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wamesema wamechoshwa na mifarakano na migogoro ya kisiasa iliyodumu kwa takrima miaka 15 tokea kuanzishwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini.

Hayo waliyasema jana, wakati wakichangia mswada wa sheria ya kuweka masharti ya kufanyika kura ya maoni kwa mara ya kwanza uliowasilishwa katika Baraza hilo na Waziri wa Nchi, Afisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma.

Walieleza kuwa Wazanzibari wamechoshwa kushuhudia migogoro na mifarakano inayoendelea siku hadi siku na iliyosababisha kuyumbisha maendeleo, sambamba na kujengeana chuki na uhasama miongoni mwa wananchi.

Akichangia Mswada huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ya Baraza hilo, Haji Omar Kheri, ambaye ni Mwakilishi wa Jimbo la Tumbatu alisema anaunga mkono mswada huo ili uwe chachu ya maendeleo na kufuta mifarakano iliyodumu tokea mwaka 1995 katika kisiwa hicho.

“Naunga mkono mswada huu mia kwa mia kwa niaba ya wananchi wa jimbo ninaloliongoza la Tumbatu ili kutumia nafasi ya demokrasia ili kuondosha mifarakano nchini”, alifahamisha Mwakilishi huyo.

Nae Said Ali Mbarouk (Gando), alionesha wasiwasi kwamba muda unaweza kutosha kwa vile Tume ya Uchaguzi imepewa dhamana ya kuendesha kura ya maoni wakati huku pia ikikabiliwa na matayarisho ya uchaguzi mkuu, sambamba inaendelea na zoezi la uandikishaji wa daftari la kudumu awamu ya pili.

Hata hivyo, alimpongeza Rais Mkapa kwa kusaini muafaka wa mwaka 2001 pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume kukutana na Katibu Kuu wa Chama cha CUF, Maalim Seif Sharif Hamad mnamo Novemba 5, mwaka jana kwa mustakabali wa maslahi ya wananchi wa visiwa hivi.

No comments:

Post a Comment