Monday 18 July 2011

MILIONI 48 KUFANYIWA MATENGENEZO BWAWA LA MICHEZANI.

Milioni 48 kufanyiwa matengenezo bwawa Michenzani

Na Essau Msabila, DSJ
BARAZA la Manispaa la Zanzibar linatarajiwa kutumia shilingi milioni 48 kulifanyia matengenezo makubwa bwawa la Michenzani ili kulirejesha katika haiba yake.
Mkurugenzi wa Baraza hilo, Rashid Ali Juma amesema ukaguzi wa awali kuhusu ujenzi huo umekamilika kwa kiasi cha asilimia 30 ikiwa ni pamoja na kuunganisha paipu zote zinazorusha maji.
Mkurugenzi huyo alisema mambo mengine yaliyokwishafanyiwa marekebisho ya awali ni pamoja na kusafisha eneo la bwawa, kuziba paipu zilizooza na zile zinazovuja na kazi ya upakaji rangi vinavyotarajiwa kurekebishwa hivi karibuni.
Rashid alisema mazungumzo yameshafanyika kati ya Baraza na wawekezaji wa kiwanja cha kufurahishia watoto cha bustani ya Jamhuri na wale wa bustani ya Forodhani, ili kuwapatia mashine tatu maalum za kurushia maji zenye thamani ya shilingi milioni 33.
Hata hivyo, alisema pamoja na uchache wa vifaa vya kufanyia kazi, pia wanakabiliwa na tatizo la uwezo mdogo wa kielimu, lakini alisema itahakikishwa kwamba bwawa hilo linafanya kazi wakati wa sikukuu ya Idd.
Akizungumzia suala la kubandika matangazo, Rashid alisema baraza liliwaalika wafanyabiashara wa aina mbali mbali zikiwemo kampuni za simu, Zanzibar Cool pamoja na "Drop" ili watengeneze kwa kuweka matangazo yao, lakini hakuna aliyejitokeza kukubali kufanya hivyo.
Aidha, alisema kampuni pakee iliyojitokeza ni ile ya Kampuni ya simu Zanzibar, ZANTEL lakini baadae kampuni hiyo haikuendelea na majadiliano na baraza ndipo likaamua kuifanya kazi hiyo yenyewe.

No comments:

Post a Comment