Sunday 17 July 2011

WAHADHIRI WAIKIMBIA SUZA KWENDA KUSOMESHA DODOMA.

Wahadhiri waikimbia SUZA kwenda kusomesha Dodoma

Na Halima Abdalla
WIZARA ya elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, imetakiwa kuchukua hatua ili kuwafanya wahadhiri kutokimbia kufanya kazi katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).
Akichangia akichangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ya mwaka 2011/2012, Mwakilishi wa Mji Mkongwe, Ismail Jusa Ladhu, alisema inasikitisha kuona wahadhiri waliobobea katika fani muhimu walio katika kiwango cha Udaktari wa falsafa (PHD) kukikimbia chuo hicho na kwenda kusomesha Chu Kikuu cha Dododoma.
Jusa alisema hali hiyo inatia shaka kwa wahadhiri wanaosomea PHD hivi sasa nao hawatorudi kutokana na kutokuwepo maslahi mazuri chuoni hapo.
Aidha Wizara hiyo imeshauriwa kuweka muda wa masomo ya ziada nyakati za jioni katika maskuli ili kuepusha wanafunzi kwenda kusoma masomo hayo vichochoroni au skuli za binafsi.
Ushauri huo umetolewa na Omar Ali Sheikh (Chake Chake) katika kikao cha Baraza la Wawakilishi alipokuwa Alisema masomo hayo ya ziada yakipelekwa maskulini itasaidia katika maskuli kujipatia pesa ikiwemo walimu kujipatia posho za kuweza kusaidia kujikimu na maisha.
Aidha alisema tatizo la walimu kukimbia katika vyuo vikuuu lina sababishwa na mishahara midogo wanayolipwa aliishauri Serikali kuwaongezea wataalamu mishahara ili kuzuia kuondoka.
Akichangia Bajeti hiyo Ashura Sharif Ali (Nafasi za wanawake) aliishauri Wizara ya Elimu kufanya juhudi japo kwa kutafuta wafadhili kuwapatia posho japo la sabuni walimu wa vyuo vya madrasa ili kuwapa nguvu ya kufundisha walimu hao.
Alisema elimu ya madrasa ndio ya mwanzo anapoanzia mtoto kupatia elimu ya akhera hivyo inahitaji kusukumwa.
Nae Subeit Khamis Faki (Micheweni) aliishauri Wizara elimu kuwapunguzia michango walimu kwani mishahara yao walimu haiwatoshi hivyo alimtaka Waziri wa Elimu kukaa pamoja na kuzingatia jinsi gani ya kuwapunguzia walimu mzigo huo.
Aidha waliishauri Wizara ya Elimu kuacha kuwa changisha wanafunzi karatasi za mitihani kipindi cha mitihani ikifika kwani kunarejesha nyuma maendeleo ya wanafunzi maskulini.
Sambamba na hayo aliishauri Serikali kuwalipa walimu fedha zao za kusimamia mitihani kwa wakati muafaka wanapomaliza kusimamia mitihani hiyo kwani Serikali imekuwa ikiwacheleweshea walimu fedha zao wanapomaliza kusimamia mitihani .
Kwa upande wake Abdalla Muhammed Ali (Mkoani) aliishauri Serikali ifanye jitihada ya kuongeza walimu kwani waliopo hawatoshi kwani Zanzibar kuna skuli 700 na kwa sasa Serikali ina mpango kuajiri walimu 800 aliishauri Serikali kuongeza idadi hiyo kwani hitoshi na kwa sasa Zanzibar inakabiliwa na uhaba wa walimu.
Alisema kuna walimu wengi hawajaajiriwa mpaka sasa ambao wanafika mikumbo minne ambayo imemaliza vyuoni hivyo aliishauri Serikali kuongeza idadi ya walimu ki wa kuwaajiri ili kupunguza tatizo la walimu maskulini.

No comments:

Post a Comment