Wednesday 23 February 2011

FAINAL ZA KOMBE LA CHAN SUDAN.

WAANDAAJI wa mashindano ya soka kwa mataifa ya Afrika yanayohusisha wachezaji wa ligi za ndani (CHAN) timu ya Sudan, wametupwa nje na Angola katika mchezo wa nusu fainali juzi.


Angola ilishinda kwa penelti 4-2 kwa mikwaju ya penelti baada ya miamba hiyo kumaliza dakia 120 ikitoka sare ya 1-1, katika mchezo uliokumbwa na vituko vya mashabiki wa Sudan waliokuwa wakirusha chupa uwanjani.

Sudan ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa mchezaji wake Saifeldin Ali Idris mwishoni mwa kipindi cha kwanza, kabla Angola kusawazisha katika dakika ya 70 kwa goli lililofungwa na Arsenio Cabungula.

Licha ya kuanza dakika 30 za nyongeza kwa kasi na mashambulizi ya mfululizo, Sudan ilijikuta ikicheza pungufu pale nahodha wake alipooneshwa kadi nyekundu kwa kosa la kumpiga kichwa mchezaji mmoja wa Angola na kumrushia ngumi mwengine.

Hata hivyo hakuna timu iliyoweza kuziona nyavu katika muda huo wa ziada, na kulazimisha mchezo huo uamuliwe kwa mikwaju ya penelti.

Nayo Tunisia imefauikiwa kutinga fainali baada ya kuwabwaga majirani zao Algeria kwa penelti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 katika mchezo mwengine wa nusu fainali.

Kwa matokeo hayo, mchezo wa fainali utazikutanisha Tunisia na Angola kesho, wakati wenyeji Sudan na Algeria watatangulia kucheza mechi ya kusaka mshindi wa tatu

No comments:

Post a Comment