Friday 27 August 2010

DK. Karume Kuzinduwa Nyumba ya Mpya ya Mayatima Zanzibar.

Dk. Karume kuzindua nyumba mpya ya Mayatima Zanzibar



Na Mwanajuma Abdi

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume leo, anatarajiwa kufungua nyumba ya kulelea watoto yatima ya kisasa Mazizini nje kidogo wa mji wa Zanzibar.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya ZAYEDESA, ambae pia ni Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Shadya Karume alisema Rais Karume ataifungua nyumba hiyo asubuhi kutokana kukamilika kwa ujenzi wake, ambapo sherehe hiyo itahudhuriwa na watoto wenyewe wa Forodhani na wageni mbali mbali.

Mama Shadya Karume alieleza nyumba ya watoto wa Yatima ya Mazizini imejengwa na Jumuiya ya ZAYEDESA, ambayo itatoa nafasi kwa watoto yatima wanaoishi nyumba ya kulelea watoto Forodhani waliokuwa chini ya udhamini ya Serikali kuhamia katika nyumba hiyo mpya.

Alifahamisha kuwa, kujengwa kwa nyumba hiyo kunatokana na nyumba ya Forodhani kuwa finyu ukilinganishwa na idadi ya watoto wanaolelewa kuongozeka.

Aidha alisema sababu nyengine ya kujengwa kwa nyumba hiyo ni Mji Mkongwe wa Zanzibar umekua zaidi katika shughuli biashara, utalii na kuongezeka kwa idadi ya watu, jambo ambalo Jumuiya ya ZAYEDESA imeona ipo haja ya kujenga nyumba nyengine itayowaweka watoto katika mazingira mazuri ya kujisomea, malaazi na kushiriki katika michezo kwa ajili ya kujenga afya kutokana nyumba ya Mazizini kuwa na eneo kubwa la kufanya shughuli hizo.

Alieleza nyumba mpya ya Mazizini itakuwa na darasa maalum la kusomea, chumba cha kompyuta na chumba cha kujifundisha ushoni kwa kutumia vyarahani kwa watoto wanaishi humo.

Mama Shadya Karume alisema kwamba, sehemu ya iliyokuwa ikitumiwa na watoto yatima Forodhani iliyochini ya Ustawi wa Jamii inatarajiwa kuwa ni Makumbusho ya Uhusiano wa Usafiri wa Bahari ya Hindi na Historia ya Zanzibar katika pwani ya Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment