Saturday 21 August 2010

MASHINDANO KUHIFADHISHA KURAN KUFIKIA KILELE LEO.

Mashindano kuhifadhi Kuran kufikia kilele leo



Na Aboud Mahmoud

KAIMU Kadhi Mkuu wa Zanzibar,Sheikh Khamis Haji anatarajiwa kuwa mgeni rasmin katika mashindano ya kimataifa ya kuhifadhi kuran yanayotarajiwa kufanyika katika Msikiti wa Afraa Bint Issa Kidongo Chekundu.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Amir wa maswala ya uenezi, Maalim Mustafa Basha,zinasema kuwa Kaimu Kadhi huyo anatarajiwa kushiriki katika mashindano hayo ambayo yatakuwa ni ya siku ya mwisho na kushindaniwa juzuu 30 tu.

Maalim Mustafa alisema kuwa mashindano hayo
Kwa wanaume na kwa upande wa wanafunzi wa kike, wanatarajia kufunga mashindano hayo leo katika ukumbi wa Salama Bwawani.

Aidha, alizitaja nchi zitakazoshiriki katika mashindano hayo ni pamoja na wenyeji Zanzibar,Tanzania Bara, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Msumbiji na Visiwa vya Comoro.

Alieleza kuwa mashindano hayo yataendeshwa kwa njia ya kuhifadhi usomaji wa kuran pamoja na njia ya Tashjii Tahkik.

Mashindano ya kuhifadhi Kuran yaliendelea juzi katika msikiti Sahaba Mtoni, Kidato na wanawake yalifanyika katika ukumbi wa Haile Selassie ambapo mashindano hayo yalikwenda kwa njia ya Tashjii tahkik.

Katika mashindano wanafunzi kutoka visiwani Zanzibar walikuwa wakiendelea kuwa mbele katika mashindano hayo .

Kwa upande wa wanaume mashindano hayo yalikua ni kuanzia juzuu 5,10,15,20na 25 ambapo mshindi wa juzuu 30 alikuwa ni Ali Khamis aliepata alama 100 mshindi wa pili Ali Salum aliepata alama 99.95 na Ali Ahmad alipata alama 69.65.

Mshindi wa kwanza juzuu 25 alikuwa ni Nabil Masoud aliepata alama 93.00 wakati mshindi wa pili alikuwa Abdulawal Khamis aliepata alama 70.65 .

Kwa upande wa juzuu 20 mshindi alikuwa ni Abdulaziz Abdullah alipata alama 100, Jaffar Hajji alipata alama 86.00 na Muhidin Suleiman alipata alama 77.99.

Kwa upande wa wanawake mwanafunzi Husna alipata alama 100 na kuwa mshindi wa juzuu 30 huku mwanafunzi Mariama Mohammed alikuwa mshindi wa juzuu 25 kwa kupata alama 100,Juzuu 15 alikuwa Sabah Abdullah na Zulfa Abdullah alikuwa mshindi wa juzuu tano.

Wananfunzi hao walioshinda walizawadiwa fedha taslim pamoja na vitu mbali mbali ikiwemo tv.

No comments:

Post a Comment