Monday 23 August 2010

WAWAKILISHI MADIWANI WASUASUA KUREJESHA FOMU ZA UTEUZI

Wawakilishi, madiwani wasuasua kurejesha fomu za uteuzi



Na Mwanajuma Abdi

JUMLA ya wagombea 53 wa nafasi za Uwakilishi na wagombea 90 wa Udiwani wamejitokeza katika majimbo ya Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, kuchukua fomu za kuwania nafasi hizo kupitia vyama mbali mbali vya siasa.

Idadi hiyo imepatikana hadi jana ambapo gazeti hili lilitembeleza Afisi zaTume ya Uchaguzi ya Wilaya ya Mjini iliyopo Maisara na ya Wilaya ya Magharibi huko Mwanakwerekwe.

Kati ya wagombea hao wa Uwakilishi waliochukua fomu ni 11 ndio waliorejesha fomu huku kati ya maombi 90 ya madiwani kukiwa na idadi ya fomu 19 zilizorejeshwa.

Msimamizi Msaidizi wa Tume ya Uchaguzi Wilaya Mjini, Mohammed Ali Abdallah aliwataja waliorejesha fomu hizo ambao wote ni wagombea kupitia tiketi ya CCM, Nassor Salum Ali (Jazeera) wa jimbo la Rahaleo, Suleiman Othman Nyanga (Jang'ombe), Mahmoud Mohammed Mussa (Kikwajuni), Ali Salum Haji (Kwahani), Salmin Awadh Salmin (Magomeni) na Fatma Said Mbarouk (Amani).

Aidha alisema kwa upande wa Udiwani wagombea waliochukuwa ni 50 kati ya hao wagombea 12 wamerejesha fomu hizo ni Ameir Makungu Makame (CCM), anayegombea Wadi ya Rahaleo, Bikwao Hamad Khamis (CHADEMA) Wadi ya Jang'ombe, Abdallah Ali Chum (CCM) Wadi ya Amani na Saleh Fasih Mzee (CCM) Wadi ya Jang'ombe.

Alieleza wagombea wengine wa Udiwani ni Khamis Mabrouk Khamis (CCM), Wadi ya Mlandege, Khatib Abdurhman Khatib (CCM) Wadi ya Miembeni, Mahabubu Juma Issa (CCM) Wadi ya Kikwajuni, Zubeir Juma Salum (CCM) Wadi ya Meya, Asha Ali Abeid (CCM) Wadi ya Nyerere, Juma Ngwali Juma (CCM) Chumbuni, Machano Mwadini Omar (CCM) Kwahani na Awena Abdallah Mkubwa (CCM) Wadi ya Mikunguni.

Nae Msaidizi Afisa wa Uchaguzi wa Wilaya ya Magharibi, Khamis Mussa Khamis alisema wagombea waliochukuwa fomu za kuwania nafasi za Uwakilishi walikuwa ni 28 kati ya hao watano ndio waliorejesha fomu hadi jana mchana.

Aliwataja wagombe hao ni Thuwaybah Kissasi (CCM) jimbo la Fuoni, Ali Abdalla Ali (CCM) Mfenesini, Asha Mohammed Hilal (CCM) Magogoni, Khamis Jabir Makame (CCM) Mtoni na Mansoor Yussuf Himid wa Kiembesamaki.

Maalim Khamis aliwataja waliochukuwa fomu za Udiwani ni 40 kati ya hao wagombea saba wamesharejesha fomu zao katika Afisi hiyo.

Aliwataja walioresha fomu hizo ni pamoja na Mahammed Haji Kitete (CCM) Wadi ya Mwanakwerekwe, Nyange Haji Haji (CCM) Wadi ya Mbuzini, Amina Ali Mohammed wa CCM (Bububu), Msim Seif Abdulla Wadi ya Mfenesini (CCM), Bernard Lutoba Kanungu wa CCM Wadi ya Tomondo, Hamza Khamis Juma (CCM) Wadi ya Mwanyanya na Mwatima Talib Said (CCM) Wadi ya Magogoni.

Wakati huo huo, wagombea wa Udiwani kupitia CCM, Msimu Seif Abdallah (Wadi ya Mfenesini), Bernard Lutoba (Tomondo) na Nyange Haji (Mbuzini) walirejesha fomu jana, katika Wilaya ya Magharibi, ambapo Maalim Khamis alizipokea na kuwaambia waende katika Afisi hiyo, Septemba pili mwaka huu saa 10:00 jioni ili kuangalia kama hawajawekewa pingamizi au kama wanataka kuweka pingamizi kwa wagombea wengine.

Katika Wilaya ya Kati Unguja, Afisa wa Uchaguzi, Maalim Mussa Ali Juma alifahamisha kuwa, katika Wilaya hiyo wagombea tisa wamejitokeza kuchukua fomu za kuwania Uwakilishi kutoka vyama mbali mbali vikiwemo cha CCM, CUF, Jahazi Asilia, TLP, CHADEMA, ambapo hadi mchana wa jana hakuna aliyerejesha fomu.

Aidha kwa upande wa nafasi za Udiwani waliochukuwa fomu za kuwania wadi mbali mbali walikuwa 25, ambapo pia hakuna aliyerejesha fomu hadi jana mchana.

No comments:

Post a Comment