Friday 3 December 2010

KOCHA HUSSEIN KHERI AFARIKI DUNIA.

Hussein Kheri afariki dunia



Na Salum Vuai, Dar es Salaam
Ijumaa 3 Disamba 2010
KOCHA wa zamani wa timu ya taifa ya Kenya ‘Harambee Stars’ Hussein Kheri, amefariki dunia juzi mjini Nairobi .

Taarifa zilizopatikana kutoka katika klabu yake ya zamani aliyokuwa akiifundisha kisiwani Unguja Malindi, zimefahamisha kuwa Kheri amekufa kutokana na ugonjwa wa kisukari uliokuwa ukimsumbua kwa miaka mingi.

Mmoja wa viongozi wa klabu hiyo ambaye hakutaka kutajwa kwa kuwa sio msemaji, alifahamisha kuwa uongozi wa timu hiyo ulipokea simu kutoka Nairobi iliyoeleza kifo cha mwalimu huyo na kusema kuwa alitarajiwa kuzikwa jana huko Kenya .

Aidha alieleza kuwa marehemu alikuwa akijiandaa kwenda Zanzibar wiki hii kabla kukutwa na mauti.

Marehemu Kheri atakumbukwa kwa kuiwezesha Malindi kupata mafanikio makubwa katika soka nchini Tanzania , pamoja na kutwaa ubingwa wa visiwani mara nyingi.

Aidha aliwahi kufundisha klabu ya Moro United inayocheza ligi kuu Tanzania Bara kabla kurudi tena Malindi na hatimaye kuchukuliwa na timu ya JKU msimu uliopita.

Hata hivyo, hakuwahi kumsliza msimu huo wakati uongozi wa JKU ulipoamua kusitisha mkataba wake.

Kabla kufanya kazi ya ukocha, Kheri alikuwa beki mahiri wa Harambee Stars kwenye miaka ya sabini na awali themanini.

No comments:

Post a Comment