Sunday 19 December 2010

UINGEREZA YARIDHIASHWA NA MAELEWANO ZANZIBAR.

Uingereza yaridhishwa na maelewano Zanzibar

Na Ali Mohamed, Maelezo
Jumatatu 20 Disemba 2010
UINGEREZA imeelezea kuridhishwa na hali ya maelewano, mashirikiano na maendeleo ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliyo katika mfumo wa Umoja wa Kitaifa iliyoundwa na Dk. Ali Mohamed Shein.

Uingereza imewekwa bayana hali hiyo kupitia Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Deane Coner baada ya chakula cha mchana huko Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Alisema hatua iliyofikiwa na Zanzibar inaonesha ishara njema kwa wananchi wa Zanzibar ya kushirikiana na kulisukuma gurudumu la maendeleo ya nchi kwa maslahi ya wananchi wote.

Kwa niaba ya nchi yake Balozi huyo alisema Uingereza itazidisha mashirikiano na Zanzibar na kuisadia katika miradi mbali mbali ya maendeleo.

Aidha aliitakia Zanzibar mafanikio mema katika maelewano na mashirikino na kutoa wito kwa viongozi na wananchi kudumisha zaidi hali hiyo kwa maslahi ya nchi yao.

Deane Coner, alifika katika kijiji hicho cha Makunduchi kwa ajili ya kufungua wodi ya wazazi katika hospitali ya Makunduchi iliyojengwa na taasisi isiyo ya kiserikali ya Uingereza (HIPZ).

Akimfahamisha mchakato uliopitiwa na Zanzibar hadi kufika hatua hiyo ya kuundwa kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mfumo wa Umoja wa Kitaifa, Mwenyekiti Mstaafu wa Baraza la Wawakilishi Ali Mzee alimwambia Kamishna huyo kuwa uamuzi huo ulikuwa ni wa Wazanzibari wote bila kujali itikadi za kisiasa.

Nae Waziri wa Kazi, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika Haroun Ali Suleiman, ambae ndie aliyekuwa mwenyeji wa Kamishna huyo katika chakula hicho cha mchana alisema anaamini kuwa serikali iliyoundwa ya Umoja wa Kitaifa itaivusha Zanzibar kuelekea katika maendeleo makubwa.

No comments:

Post a Comment