Monday 6 December 2010

MAABARA YA JAMII KUPUNGUZA VIFO VYA WATOTO.

Maabara ya jamii kupunguza vifo vya watoto


Na Masanja Mabula, Pemba


Jumatatu 6Disemba 2010

MRADI wenye lengo la kupunguza vifo vya watoto wachanga walio na umri wa siku moja hadi siku 28 unatarajiwa kuendeshwa na maabara ya Afya ya Jamii Kisiwani Pemba ikishirikiana na Chuo Kukuu cha John Hopkins cha Marekani.

Akizungumza katika mkutano uliofanyika Wesha ukumbi wa Pemba Bahari, na kuwajumuisha viongozi wa maabara hiyo, viongozi wa Chuo Cha JHU na wataalamu wengine kutoka Zambia, Mkurungenzi wa Maabara ya Afya ya Jamii kisiwani Pemba Dk. Said Mohammed Ali alisema mradi huo utakuwa ni muda wa miaka 5.

Alisema katika utekelezaji wa mradi huo watendaji wa maabara ya afya ya jamii watakuwa wanafuatilia akinamama wanaobeba mimba hadi kufikia siku 28 tokea kujifungua kwa kuwapatia dawa kwa ajili ya kuwapaka watoto wao katika sehemu ya kitovu.

Alisema chini ya mradi huo ambao utawashirikisha wakunga wa jadi, watawapatia vitendea kazi ikiwemo dawa na simu za mikononi ambapo pia watatakiwa kuwahamiza mama wajawazito kujifungulia katika haspitali na vituo vya afya.

Mkurugenzi huyo alisema mama akijifungua katika hospitali au kituo cha afya, ataweza kupatiwa huduma za kitaalamu pale yatakapojitokeza.

Dk.Said alisema katika utafiti wa awali uliofanywa hivi karibuni na maabara hiyo, umebaini kuwepo na mwitikio mzuri kutoka kwa jamii na kwamba ana imani kuwa mradi huo utapata mafanikio makumbwa.

Mbali na kufanyika hapa kisiwani Pemba, mradi huo ambaao umefadhiliwa na kituo cha Afya na Maendeleo cha Boston University cha Marekani pia unatarajia kufanyika katika nchi ya Zambia

Katika mkutano huo pia alihudhuria Naibu Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk. Sira Ubwa Mwamboya pamoja na Mkurungezi wa Wizara hiyo Dk. Malick Juma

No comments:

Post a Comment