Monday 6 December 2010

NCHI ZINAZOENDELEA ZIZUIE UHARIBIFU WA MAZINGIRA.

Nchi zinazoendelea zizuie uharibu wa mazingira


Na Khatib Juma Mjaja, Denmark


Jumatatu 6 Disemba 2010


NCHI zinazoendelea zimetakiwa kutilia maanani utekelezaji wa mikakati ya kuzuia uharibifu wa mazingira, ikiwa ni sehemu ya kupunguza athari za kimazingira zinazotokea.

Akizungumza na ujumbe wa wafanyakazi wa taasisi za nchi mbali mbali,huko Makao Makuu ya Taasisi ya Mazingira kwa nchi za Ulaya, mjini Copenhagen Denmark,Meneja wa miradi ya mabadiliko ya tabia nchi kwa nchi za Ulaya na mtaalamu wa utafiti wa mazingira Dk. Hans Martin Fussel, alisema athari za kimazingira zinazojitokeza zitaongezeka endapo jitihada za makusudi hazitachukuliwa.

Alisema miongoni mwa mikakati iliyowekwa na mkutano wa kujadili mabadiliko ya tabia nchi, jijini Copenhagen mwaka 2009, ni pamoja na nchi za Ulaya kupunguza matumizi ya gesi za kemikali zinazoathiri hali ya hewa kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2020.

Aidha katika mkutano huo wa mwaka jana nchi zinazoendelea zimetakiwa kupunguza uharibifu huo kwa asilimia kati ya 20 hadi 30 ifikapo mwaka 2015.

Alisema hali ya sasa ya uharibifu wa mazingira ya anga imefikia nyuzi joto 2 huku kiwango cha kawaida kinachohitajika kuwa na uwiano wa hali ya hewa ni asilimia 0.8.

Alisema kiwango hicho cha asilimia 2 kilichopo sasa ni miongoni mwa sababu zinazopelekea majanga ya kimazingira yanayotokea kama vile, mafuriko kutokana na kuyeyuka kwa theluji milimani, vimbunga na mtandao wa barafu katika visiwa vya kijani ” Green land”.

Aidha Dk. Fussel alisema ongezeko la joto, linalosababishwa na uharibifu wa mazingira,linasababisha uzalishaji mdogo wa vyakula kwenye nchi nyingi za dunia ya tatu kukumbwa na majanga ya njaa mara kwa mara.

Dk. Fussel, alisema suala la uharibifu wa mazingira lazima lichukuliwe kwa tahadhari ya kipekee la si hivyo athari zake zitaendelea kuiathiri dunia.

No comments:

Post a Comment