Wednesday 7 April 2010

Maridhiano yafanya vikao BLW kuwa shwari- Kificho

SPIKA wa Baraza la Wawakilishi Zaznibar Pandu Amier Kificho ameweka wazi kuwa sasa kuendesha vikao vya Baraza hilo ni shwari kufuatia maridhiano kati ya Rais Karume na Maalim Seif.
 
Kificho alitoa kauli hiyo mapema wiki hii wakati alipopokea ugeni wa Kamati ya Huduma za Jamii ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania hapo Ofisini kwake Mnazimmoja mjini Zanzibar.
 
“Vikao vya Baraza sasa vinakwenda vizuri kufuatia maridhiano hayo na nashukuru kwangu inakuwa ni rahisi kuviongoza”, alisema Kificho.
 
Alisema maridhiano hayo yamefungua ukurasa mpya wa umoja na mashirikiano kati ya wajumbe wa Baraza hilo hali inayompa unafuu wa kuwaongoza vikao vya baraza hilo.

Alikiri kuwa kabala ya maridhiano hayo alikuwa na wakati mgumu wa kuongoza vikao vya wajumbe wa Baraza hilo hasa wakati wa bajeti ya mwaka kutokana na mivutano iliyokuwepo kati ya wajumbe.
 
Aidha aliwaambia wambunge hao kuwa sambamba na hali kuwa shwari ndani ya Baraza maridhiano hayo yamefungua njia zaidi ya mashirikino katika shughuli za maendeleo ya jamii.
 
Kificho alitolea mfano wa maendeleo ya elimu kuwa yamekuwa zaidi kutokana na viongozi wa chama tawala na upinzani kushirikiana na jamii katika masuala ya kuimarisha elimu.
 
Nae Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Huduma za Jamii inayoshughulikia Elimu na Afya Omar Kwang alisema sera ya uchauzi ya mwaka 2005/2010 imetekelezwa kwa asilimia kubwa na serikali zote mbili.


Na Ali Mohamed, Maelezo

No comments:

Post a Comment