Wednesday 14 April 2010

ZEC yatangaza tarehe ya uchaguzi Mkuu Z’bar

Na Mwantanga Ame
TUME ya Uchaguzi ZEC, imetangaza kuwa uchaguzi Mkuu wa Zanzibar utafanyika Oktoba 31 mwaka huu baada ya kuvunjwa Baraza la Wawakilishi.

Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Salum Kassim Ali, ametoa tamko hilo mbele ya waandishi wa habari walIoshiriki semina kuhusu maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu, katika hoteli ya Zanzibar Beach Resort, nje kidogo ya Mji wa Zanzibar

Semina hiyo ambayo imeandaliwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar, na kufadhiliwa na Shirika la Umoja waMataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP) kwa ajili ya Wawakilishi wa asasi zinazofanya kazi na Wanawake ikiwa ni hatua ya kujadili mahitaji ya Wanawake wakati wa Uchaguzi.

Mkurugenzi huyo alisema sehemu kubwa ya maandalizi ya uchaguzi Mkuu ujao wa Zanzibar yamekamilika na uchaguzi huo umepangwa kufanyika kuanzia Oktoba 31 mwaka huu.

Katiba ya Zanzibar inaeleza kuwa Tume ya uchaguzi ndiyo yenye Mamlaka ya kuitisha uchaguzi ndani ya siku tano baada ya Baraza la Wawakilishi kuvunjwa.

Alisema uteuzi wa wagombea kupitia Tume hiyo utaanza Agosti mwaka huu baada ya vyama kumaliza kufanya uteuzi wao.

Kuhusu kampeni, Mkurugenzi huyo alisema zitanzia Oktoba 10, mwaka huu na kumalizika siku moja kabla ya uchaguzi kufanyika.

Alisema vifaa kwa ajili ya uchaguzi huo vimeanza kuagizwa na vinatarajiwa kufika nchini wakati wowote zikiwemo taa, Kompyuta na wino maalum wa kupigia kura.

Hata hivyo, alisema katika uchaguzi huo, hakuna jimbo litakalokatwa na kubakia yale yale 50 na wadi 141.


No comments:

Post a Comment