Friday 23 April 2010

Mgombea Urais Z'bar kuweka dhamana milioni 3 ZEC

Na Issa Mohammed
TUME ya Uchaguzi Zanzibar imepandisha kima cha fedha za dhamana kwa watakaogombea nafasi ya urais,uwakilishi na udiwani katika uchaguzi Mkuu ujao.

Kwa mujibu wa taarifa ya Tume hiyo kwa vyombo vya habari, mgombea urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu atatakiwa kuweka dhamana ya fedha shilingi milioni tatu badala ya shilingi milioni moja.

Taarifa hiyo imefahamisha kwamba mgombea uwakilishi atatakiwa kuweka dhana ya shilingi laki tatu badala ya shilingi hamsini elfu wakati mgombea udiwani ataweka dhamana ya shilingi hamsini elfu badala ya shilingi elfu kumi na tano.

Tume hiyo imesema kwamba maandalizi ya uchaguzi huo yanaendelea vizuri na kwamba imo katika jitihada za kuhakikisha kuwa ratiba ya kazi zote zilizopangwa kwa ajili ya uchaguzi huo zinakwenda kama ilivyokusudiwa.

Aidha, Tume hiyo imetangaza tarehe za kuchukuwa fomu kwa wagombea watakaowania nafasi ya urais, uwakilishi na udiwani katika

uchaguzi huo utakaokuwa wa tatu chini ya mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini.

Tume katika taarifa hiyo, imefahamisha kuwa uchukuwaji fomu za kugombea urais utaanza Agost 10 hadi 30, wakati uchukuaji fomu za uwakilishi na udiwani utaanza tarehe Agosti 15 hadi 30 Augosti.

Kwa upande wa kampeni za uchaguzi, tume imesema shuhuli hizo zitaanza Septemba 10 hadi 30 na kuwa siku ya kupiga kura itakuwa tarehe 31 Oktoba.

No comments:

Post a Comment