Tuesday 3 May 2011

CAG AVIJIA JUU VYOMBO VYA HABARI

CAG avijia juu vyombo vya habari

Na Kunze Mswanyama
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Uttoh, amekanusha tuhuma zilizoelekezwa kwake na kwa Shirika la Umeme nchini (TANESCO) juu ya matumizi mabaya ya fedha za umma hasa malipo ya shilingi bilioni moja kwa kampuni ya Dowans zilitolewa na baadhi ya vyombo vya habari mapema wiki iliyopita.
CAG Uttoh alisema kuwa katika ripoti yake aliyoipeleka kwa Rais Dk. Jakaya Kikwete mapema mwishoni mwa Machi haina kipengele chochote kinachosema kuwa "Tanesco kuna ufisadi mpya na pia vyama vya siasa pia kuna ufisadi,hakuna kifungu hata kimoja nilichokiandika katika ripoti yangu kinachosema hivyo",alisema.
"Katika uwasilishaji wa ripoti zangu kumetokea mapungufu katika ufafanuzi na uchambuzi wa ripoti hizi. Baadhi ya vyombo vya habari vimeripoti baadhi ya taarifa potofu za shirika la umeme nchini na vyama mbalimbali vya siasa, nawaomba waandishi muwe mnaitafuta ofisi yangu ili kujua baadhi ya ripoti zinazohitaji ufafanuzi".
"Ninapenda ieleweke wazi kuwa katika taarifa zangu za ukaguzi hakuna sehemu yeyote niliyotumia neno kashfa mpya au ufisadi kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.Habari zilizoandikwa si tu kwamba si sahihi lakini pia hazipo kabisa katika taarifa za mwaka ulioishia Juni 30,2010",alisema CAG.
Alisema baadhi ya taarifa zisizokuwa sahihi kuwa ni pamoja na ile ya Tanesco kuilipa Dowans dola 1.2 milioni badala ya 120,000 za kusafirishia mitambo hiyo kuja nchini.Pia matumizi hayo yanakadiriwa kufikia shilingi bilioni 1.4 kwamba ziliingizwa katika akaunti ya Dowans kimakosa.
Pia,hadi sasa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali amesema Tanesco imeshindwa kumpelekea ripoti ya matumizi ya fedha hizo alizoziita kuwa za ufisadi pia kwamba waliokatiwa umeme na shirika hilo bado wanatumia ilhali wanadaiwa bili ya dola 65,000 habari hizo zote si za kweli.
Kwa upande wa vyama vya siasa alisema kuwa yeye kama Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu hajakagua hesabu za vyama hivyo ila anavisihi kupeleka taarifa zao za mapato na matumizi kwa Msajili ili nae azipeleke kwake ili kuwepo na uwazi kwa matumizi ya fedha za umma hasa kwa vyama vile ambavyo vilipata ruzuku ya serikali ili kuendeshea uchaguzi uliopita wa mwaka 2010.
Taarifa hiyo ilisema kuwa ,"vyama vya CUF na NCCR-Mageuzi vimetumia vibaya fedha hiyo hilo sio sahihi kwa kuwa bado sijakagua hesabu zao",alisema Uttoh.
Baadhi ya vyombo vya habari hapa nchini (siyo hili), kwa muda wa wiki moja iliyopita vimekuwa vikiripoti habari za ufisadi hasa kutokana na ripoti ya CAG jambo lililofanya taasisi hiyo kubwa na nyeti nchini katika dhana nzima ya utawala bora, kuwaita waandishi wa habari na kukana kutoa taarifa hizo.

No comments:

Post a Comment