Tuesday 3 May 2011

ASHIKILIWA NA NYARA ZA SERIKALI

Ashikiliwa na nyara za serikali

Na Nalengo Daniel, Morogoro
JESHI la polisi mkoni hapa linamshikilia Sudy Pazi (26) mkazi wa jijini Dar es salaam kwa tuhuma za kuingia ndani ya hifadhi ya Mikumi na kukutwa na nyara za serikali zenye thamani ya shilingi milioni 9.6.
Akizungumza na waandishi wa habari kamanda wa polisi mkoni hapa Adolphina Chialo alizitaja nyara hizo kuwa ni vipande 8 vya meno ya Tembo vyenye uzito wa kilo 10.3 , vyenye thamani ya shilingi milioni 9.5, mikia miwili ya tembo na ngozi paka mwitu vyenye thamani ya shilingi 168,000.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Aprili 30 mwaka huu saa 4:30 asubuhi na kwamba mtu huyo alikamatwa na askari wa hifadhi ya wanyamapori Aloyce Munka (63) aliyekuwa doria ndani ya hifadhi hiyo.
Alisema kuwa askari huyo alimkamata mtuhumiwa ndani ya hifadhi hiyo katika eneo la Magogoni tarafa ya Mvuha wilaya ya Morogoro vijijini na kwamba uchunguzi unaendelea na kwamba atafikishwa mahakamani wakati wowote baada ya uchunguzi kukamilika.
Katika tukio jingine watu wawili wanashikiliwa na polisi mkoni hapa kwa tuhuma za kumiliki shamba la bangi lenye ukubwa wa hekari moja.
Kamanda Chialo aliwataja watu hao kuwa ni Hamisi Charasa(45 na Juma Charasa (20) wote wakazi wa kijiji cha Ihombwe kata na Tarafa ya Mikumi Wilayani Kilosa.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Aprili 30 mwaka huu saa 1:30 asubuhi katika kitongoji cha Minazini Kijiji cha Ihombwe tarafa na kata ya Mikumi.
Alisema kuwa askari mwenye cheo cha Inspekta Munuo akiwa na askari wenzake waliteketeza shamba la watuhumiwa hao kwa moto lilokuwa na miche ya bangi iliyokuwa tayari kwa kuvunwa.
Hata hivyo kamanda huyo alisema kuwa watuhumiwa wote wanashikiliwa na polisi na kwamba watafikishwa mahakamani wakati wowote mara baada ya uchunguzi kukamilika.

No comments:

Post a Comment