Tuesday 3 May 2011

MISRI YAAHIDI KUWAWEZESHA WANANCHI KIUCHUMI

Misri yaahidi kuwawezesha wananchi kiuchumi

Na Ali Mohamed, Maelezo
ZANZIBAR na Misri zimeazimia kuongeza mashirikiano zaidi katika kuwawezesha wananchi wa nchi mbili hizo kiuchumi kupitia kilimo, biashara na utalii.
Akizungumza na Waziri wa Kazi Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika katika Makao Makuu ya Wizara hiyo Mwanakwerekwe Balozi mkaazi wa Misri Zanzibar, Walid Ismail alisema maeneo hayo ni muhimu kwa mashirikiano ya kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Pamoja na nchi hiyo kuwa katika kipindi cha mpito cha kuelekea kupatikana kwa serikali yenye ridhaa ya wananchi Balozi huyo alisema Misri italeta wataalamu wa kilimo Zanzibar kutoa mafunzo ya kilimo cha kisasa.
Alisema katika sekta hiyo ya kilimo tayari nchi yake inashirikiana na Zanzibar katika mradi wa kilimo cha umwagiliaji unaendeshwa na Jeshi la Kujenga Uchumu Zanzibar (JKU).
Alisema kutokana na uhaba wa ardhi wakulima wanapaswa kulima kilimo cha kisasa kinachotumia ardhi ndogo na kuzalisha mazao mengi hivyo nchi yake itatuma timu ya wataalamu zaidi kuja kutoa mafunzo kwa wakulima wa Zanzibar.
Katika sekta ya utalii Balozi huyo mkaazi wa Zanzibar alisema Zanzibar ni kama pepo kutokana na kuwa na vivutio vingi vya utalii ambapo wananchi wengi wa Misri wanapenda kuja Zanzibar.
Alisema kikwanzo kilichopo kwa watalii wa Misri kushindwa kuja kwa wingi Zanzibar ni kukosekana kwa usafiri wa uhakika wa ndege kuja moja kwa moja katika visiwa vya Zanzibar.
Kwa upande wake Waziri wa Kazi na Uwezeshaji, Haroun Ali Suleiman alisema Zanzibar inafatilia kwa karibu matokea ya Misri na inaungana na wananchi wa nchi hiyo kuiombea kurudi katika hali yake ya kawaida.
“Kama nchi marafiki Zanzibar tunafatilia kwa karibu sana matokeo ya Misri na tunaungana na wananchi wa Misri kuwatakia mafanikio na kurudi katika hali ya kawaida”. Alifahamisha Waziri Haroun.
Alisema kihistoria nchi hizo zinafanana hivyo mashirikiano baina ya nchi mbili hizo ni kuendeleza hitoria na kuwawezesha wananchi kiuchumi na kupunguza makali ya maisha kwa wananchi.
Aidha Waziri Haroun alisema kuna umuhimu kwa watendaji wa wizara ya uwezeshaji Zanzibra kufanya ziara nchini Misri kwa lengo la kuona na kujifunza namna ya kuwawezesha wananchi kutokana na nchi hiyo kupiga hatu katika maeneo hayo hasa katika sekta ya kilimo.
Alisema kupatikana kwa ufumbuzi wa safari za ndege kutoka Misri kuja moja kwa moja Zanzibar kutaimarisha sekta ya utalii na biashara na kuimasha uchumi wa nchi mbili hizo.

No comments:

Post a Comment