Friday 6 May 2011

MWANAHIJA KUCHEZESHAA PAMBANO LA ANGOLA , ZIMBABWE

 Mwanahija kuchezesha pambano la Angola, Zimbabwe

Na Donisya Thomas
SHIRIKISHO la Soka Afrika (Caf), limemteua muamuzi pekee wa kike kutoka Zanzibar, Mwanahija Fumu, kupuliza firimbi katika pambano la michuano ya All African Games kwa vijana chini uya umri wa miaka 23.
Mwanahija, atakuwa muamuzi wa kati katika mchezo huo utakaowakutanisha vijana kutoka Angola na Zimbabwe ambao umepangwa kufanyika Aprili 10 mwaka huu jijini Harare, Zimbabwe.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi,Katibu Msaidizi wa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA), Masoud Attai, alisema, chama chake kimeupokea uteuzi huo kwa heshima kubwa.
Attai, alisema, ZFA imefarijika kutokana na mwamuzi huo kuonekana na Caf na kwamba uteuzi huo mbali ya kuwa ni sifa kwa chama hicho, lakini pia ni kwa wadau wa soka nchini.
Alisema, tayari chama chake kimeshaandika barua ya kumuombea ruhusa mwamuzi huyo ambae ni mwajiriwa wa Jeshi la kujenga Uchumi ( JKU) na kumruhusu bila kinyongo.
“ Tumefurahi kwa mwamuzi wetu kuchaguliwa na Caf katika mchezo huo wa vijana huko Zimbabwe", alisema, Attai.
"Ni sifa kubwa kwetu ukizingatia huyu ni mwamuzi mwanamke na Caf imemuamini jukumu hilo zito kwa kuthamini uwezo wake”, alisema, Attai.

No comments:

Post a Comment