Tuesday 3 May 2011

MANISPAA, ILO KUSHIRIKIANA KUZOA TAKA

Manispaa, ILO kushirikiana kuzoa taka

Na Halima Abdalla
BARAZA la Manispaa Zanzibar kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani (ILO) limeandaa mradi wa kuzoa taka na kusafisha michirizi ya maji machafu ambao utawashirikisha vikundi binafsi vya usafi vilivyopo kwenye shehia.
Akizungumza na mwandishi wetu huko ofisini kwake Mkuu wa Huduma za jamii kutoka Baraza hilo Rajab Salum Rajab alisema tayari mtaalamu wa shirika hilo ameshafanya ziara ya kuangalia vikundi hivyo na kuangalia hali ya mazingira ya Zanzibar.
Rajab alisema lengo la mpango huo ni kuweza kuwapatia ajira ya kazi ndogo ndogo za usafi kwa kila shehia kwa vijana na akina mama ili kuwasaidia kupata ajira na kuondokana na masikini.
Alisema kuwa vikundi hivyo vitakuwa vinashughulika kwa kutoa huduma za ukusanyaji taka katika maeneo ya majumbani, kusafisha michirizi ya maji machafu ili kupunguza malalamiko ya kutopata huduma za uzoaji wa taka na usafishaji katika maeneo ya Manispaa ya Zanzibar.
Alifahamisha kuwa mpango huo utakapoanza itabidi wananchi wachangie gharama ili kusaidia upatikanaji wa fedha za kuwasaidia watu hao.
''Mpango huo wa usafishaji katika shehia utasimamiwa na Diwani na Sheha pamoja na wakuu wa vikundi hivyo,''alisema Rajab.
Alieleza kuwa tayari wameshafanya mafunzo kwa wanavikundi hivyo kuhusiana na mradi huo na pia watatoa vifaa vya vitendea kazi pamoja na kufanya ziara ya kujifunza kuona wenzetu wanafanya nini kuhusiana na hilo.
Mradi huo wa uzoaji wa taka kwa shehia mbali mbali za Manispaa ya Zanzibar umefadhiliwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO).

No comments:

Post a Comment