Friday 17 June 2011

BAJETI YA ZANZIBAR YAPOKEWA KWA MAONI TAFAUTI.

Bajeti ya Zanzibar yapokewa kwa maoni tafauti

Na Waandishi wetu
WADAU, wananchi na wanasiasa wametoa maoni yao kufuatia Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha Uchumi na Mipango ya Maendeleo, Omar Yussuf Mzee hapo juzi kuwasilisha bajeti ya serikali kwa mwaka 2011/2012.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha (AFP) Said Soud, alisema pamoja na serikali katika bajeti hiyo kuonesha nia ya kukuza kilimo lakini pia ilipaswa kutoa msukumo zaidi katika biashara.
Alisema kukuzwa kwa sekta hiyo kutaweza kuwepo kwa mzunguuko wa fedha na hivyo serikali kujipatia mapato makubwa sambamba na kuhakikisha inaondoa kodi kwa bidhaa za vyakula ili kuleta ahuweni ya maisha kwa wananchi.
Naye Katibu Mkuu wa TADEA, Juma Ali Khatib, alisema itakuwa jambo la busara endapo serikali itarahisisha upatikanaji wa pembejeo za kilimo pamoja na kutoa mikopo kwa wakulima wa Zanzibar.
Alisema katika watu wenye maisha ya dhiki ni wakulima hivyo kama serikali inataka kukuza uchumi sambamba na kuondosha tatizo la ajira ni vyema kilimo kikarahisishwa kwa kutolewa mikopo huku pia akielezea wakulima hao kupatiwa masoko ya uhakika.
Naye Rais wa Jumuia ya Wafanyabiashara Wenye Viwanda na Wakulima Zanzibar (Chamber of Commerce), Mbarouk Omar Mohammed, alisema bajeti ya serikali kwa kiasi kikubwa imeisahau sekta ya biashara.
“Pengine ni bajeti nzuri kwa sekta nyengine lakini ni bajeti ambayo mimi naiona haikuzingatia sana namna ya ukuzaji wa biashara hasa ikizingatiwa mazingira ya visiwa vyetu”,alisema.
Aidha alisema pamoja na kushirikishwa kwenye mchakato wa utengenezaji wa bajeti hiyo, lakini kwa kiasi kikubwa mapendekezo yao muhimu hayakuwasilisha kikamilifu.
“Tulidhani kwa kiasi waziri angetueleza namna ya kuumaliza ugonjwa wa kensa wa wafanyabiashara wa Zanzibar kutozwa kodi mara mbili, lakini hatukuelezwa na hili limekuwa tatizo ambalo halina dawa”,alisema.
Alisema urari wa utoaji wa uingizaji bidhaa visiwani (balance of trade), utaonekana mkubwa endapo vikwazo vya kufanya biashara nje ya visiwani havitapatiwa ufumbuzi.
Kwa upande wake Katibu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Zanzibar (ZATUC), Khamis Mwinyi, alisema mfumo wa utayarishaji wa bajeti ya Zanzibar una matatizo kwa sababu makundi mengi hayashirikishwi Katika uandaaji wa bajeti hiyo na wamekuwa wakilalamikia utaratibu huo mwaka hadi mwaka.
Katibu huyo alisema kwa mujibu wa sheria kifungu namba 10 ya mwaka 1986 imeweka kamati za uongozi katika kila idara pamoja na kamati za uongozi katika kila wizara za serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, lakini tatizo kubwa wizara haziwashirikishi katika uandaaji wa bajeti.
“Shirikisho letu halikushirikishwa katika uandaaji wa bajeti hii hasa katika suala la maslahi kwa wafanyakazi na kama tunavyojua wafanyakazi wetu kwa muda mrefu kilio chao kikubwa ni mishahara kutaka kuongezewa…
….bajeti imetaja kuongezwa kwa kiwango cha mishahara lakini kwa nini kuwepo na usiri mimi nadhani suala hilo liwekwe bayana ni kiwango gani cha ziada kitakachoongezwa ili wafanyakazi wenyewe wajue na hiyo ni haki yao ya msingi wao kujua” alisema Katibu huyo.
Naye mwananchi kutoka wilaya ya Kati Mwanajuma Salmin, alisema ingawa serikali inakusudia kukibadili kilimo, lakini inapaswa kuhakikisha inaangaliwa vyema hila za wafanyabiashara kupandisha bei za vyakula.
Mwanajuma alisema bidhaa kama vile mchele, unga ngano, sembe na sukari, hazigusiki madukani na kila siku zimekuwa zikibadilika bei wa kupanda juu huku vikiwepo visingizio mbali mbali ambavyo serikali ina uwezo wa kuvidhibiti.

No comments:

Post a Comment