Monday 20 June 2011

MRADI KUMOSHA BAKORA WAFANIKIWA.

‘Komesha bakora’ wafanikiwa

Na Hamad Hija, Maelezo Zanzibar
MRADI wa majaribio wa mwaka mmoja kuhamasisha kutumia adhabu mbadala maskulini na kuacha kutumia bakora ulioanza Julai 2010 utamalizika Juni 2011 ukiwa umefanikiwa kwa kiasi kubwa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, ofisini kwake Mazizini mjini Zanzibar mratibu wa mradi huo Safia Ali Rijaali, alisema mradi huo unaoendeshwa kwa pamoja kati ya Wizara ya elimu na na shirika linaloshughulikia watoto SAVE THE CHILDREN kupata maendeleo makubwa karibu asilimia 70 za malengo yake yamefikiwa.
Amesema Mradi huo uliolenga kupunguza matumizi ya bakora na walimu kutumia njia nyengine kwa kiasi umezaa matunda kwa vile matumizi ya akora yameanza kupunguwa.
Kwa awamu ya kwanza ya majaribio ya mradi huo umezishirikisha skuli 10 za msingi za unguja na Pemba, ambapo kwa upande wa Unguja zilihusishwa skuli za Kisiwandui kwa Wilaya ya mjini na Wilaya ya Magharibi skuli ya Regezamwendo.
Kaskazini ‘A’ ni skuli ya Kinyasini na Kaskazini ‘B’ skuli ya Fujoni na Wilaya ya Kati ni Marumbi, ambapo Kusini ni Kitogani, Pemba ni Chake Chake skuli ya Pondeani, Wete ni Minungwini, Micheweni skuli ya Wingwi na Mkoani ni skuli ya Ng’ombeni, ambazo zimefaidika na mradi huo.
Aidha Mratibu huyo alisema mradi kama huo haukufikia malengo kwa kuwa muda ni mdogo sana, ambao ulihitaji angalau miaka miwili ama mitatu.
Mradi huo ambao umetumia 71 milioni, awamu hii ya kwanza ukiwa unalenga zaidi kupunguza adhabu ya bakora na kutumika adhabu nyengine ambazo hamuathiri mwanafunzi ili kujenga mahusiano mazuri kwa walimu na wanafunzi pamoja na wazee wenye watoto.
Mratibu alisema mradi kwa kiasi ni mgumu kwani kumtowa mtu katika mazoea ya kutenda jambo na kumuondoa kwa muda mdogo inakuwa vigumu kwa kiasi fulani, lakini pamoja na hayo kwa kiasi kikubwa umefanikiwa.
Akifafanua njia wanazotumia kutowa elimu ya kuhamasisha kutumia adhabu mbadala kwa wanafunzi maskulini, mratibu huyo alisema njia zinazotumika katika kufikisha ujumbe huo ni pamoja na kutumia vyombo vya habari kama vile Redio, magazeti na vipindi vya televisheni.

No comments:

Post a Comment