Tuesday 21 June 2011

DK. SHEIN AWASHANGAA WABUNGE,WAWAKILISHI WANAOWAKIMBIA WANANCHI

Dk.Shein awashangaa Wabunge, Wawakilishi wanaowakimbia wananchi

• Ahimiza mshikamano viongozi CCM, Serikali
Na Bakari Mussa, Pemba
MJUMBE wa Kamati kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa, ambae pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amewataka viongozi wa Chama hicho kushirikiana na Serikali yao kutatuwa kero za wananchi kwa kufuata Ilani ya Uchaguzi ya Chama hicho iliyoinadi wakati wa kampeni ya uchaguzi wa mwaka 2010.
Alisema CCM, itajitahidi kutekeleza ahadi ilizozitowa kupitia Ilani yake hiyo kwa vile ilizitowa kwa kujiamini na imeanza kutekeleza kwa vitendo baadhi ya ahadi hizo.
Dk. Shein, alieleza hayo ukumbi wa mikutano wa Benjamin Mkapa Wete, alipozungumza na viongozi wa CCM wa wilaya hiyo, kuanzia ngazi ya Shina hadi wilaya.
Alisema kwa kasi inayochukuliwa naCCM ya Utekelezaji wa Ilani hiyo, inategemea kumaliza utekelezaji wake kwa mujibu ilivyopangwa na Chama hicho ili kuwaondoshea kero wananchi.
Aliendelea kusema kuwa sio wakati tena wa viongozi kukaa maofisini, bali wateremke na wawe na mabadiliko waende matawini kuimarisha Chama chao na waweeleze wafuasi wao na wananchi kwa ujumla namna Serikali inavyofanya kazi na Chama cha Mapinduzi kinavyosimamia maendeleo ya wananchi bila ya kubaguwa.
Dk.Shein, alikemea mtindo wa baadhi ya Viongozi kukimbia wapiga kura wao Majimboni baada ya kuchaguliwa kwani wao ndio wanaotakiwa wawe karibu na wananchi wao ili kuelewa matatizo yao na kuyapatia ufumbuzi.
Mjumbe huyo wa Kamati kuu ya CCM Taifa, aliwataka wanaCCM, kuwa na mshikamano, umoja na maelewano miongoni mwao kwani ndio nguzo pekee itakayokiwezesha Chama kusonga mbele na daima kukiwezesha kutawala nchi hii.
“ Sio wakati wa Viongozi kukaa kimya, lazima wawe wazi na waeleze ukweli uliopo” alisema Dk. Shein.
Akizungumzia ugumu wa maisha inayoikabili Zanzibar, alisema hilo lipo lakini ukali wa maisha unaosababisha kupanda kwa gharama za maisha si la Zanzibar pekee bali ni la kidunia.
Alifahamisha kuwa Serikali haifanyi biashara imetowa uhuru kwa Wafanyabiashara wenyewe kuagiza bidhaa lakini si vyema kuwabana wananchi kibei, waangalie na bei waliyonunuwa.
Aliendelea kusema kuwa Serikali inaelewa hali hiyo, na sasa imeandaa mipango mikubwa ili Wananchi waweze kukabiliana na suala hilo na mataifa mbali mbali yanaonesha nia ya kuunga mkono juhudi hizo.
Dk, Shein, alieleza dawa ya kuwafanya wananchi waondokane na ukali wa maisha ni kukifanyia mageuzi kilimo, ili wananchi walime zaidi na kupata mazao mengi sambamba na kuwapatia pembejeo mbali mbali ikiwemo mbolea, mbegu za mazao mbali mbali.
Alisema Serikali katika msimu ujao imejipanga vyema ili iweze kukabiliana na upungufu wa chakula na kuwafanya wakulima wakipende kilimo kwa vile watakuwa wanazalisha zaidi.
“Hakuna njia ya mkato kuhusu chakula ila kwa kuboresha kilimo ili kiwe bora zaidi” alifahamisha.
Dk. Shein, aliwahakikishia viongozi na wananchi kwa ujumla kuwa ahadi zilizotolewa na CCM, katika Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2005-2010, zipo pale pale na katu haitazisahau.
“Ahadi za CCM, sio za utani kwani inatowa ahadi zinazotekelezeka “ alisema.
Alisema Serikali anayoiongoza haitambaguwa mtu wa aina yoyote kwani Serikali ni ya watu wote na kila mtu anaestahiki kupatiwa haki yake atafanyiwa hivyo, kwani yeye alikula kiapo kuwa ataongoza kwa mujibu wa Sheria.
Aliwataka wanaCCM, viongozi naWananchi kwa ujumla kuzidisha Amani, Umoja na mshikamano, iliwaishi vizuri nawaendelee kuipa heshima nchi yao .

No comments:

Post a Comment