Thursday 23 June 2011

DK. SHEIN VIONGOZI CCM MSIDANYANYIKE

Dk.Shein: Viongozi CCM msidanganyike
Na Rajab Mkasaba, Pemba
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, amewaeleza viongozi wa Chama Cha Mapinduzi kuwa wasidanganyike na kauli kuwa hali ya maisha na kupanda kwa bei ya bidhaa imesababishwa na CCM, serikali iliyoko madarakani ama viongozi wake.
Dk. Shein aliyasema hayo kwa nyakati tofauti katika ziara yake ya kuzungumza na viongozi wa CCM wa Wilaya ya Mkoani na wilaya ya Chake Chake Pemba akimalizia mfululizo wa ziara zake za kuzungumza na viongozi wa CCM wa ngazi zote kuanzia ngazi za Shina, Tawi, Wadi, Jimbo, Wilaya hadi Mkoa Unguja na Pemba.
Dk. Shein aliwataka viongozi hao wajue na watoe maelezo kwa wale wasiofahamu kuwa hali ya kupanda kwa maisha inatokana na kupanda kwa bei ya bidhaa za vyakula katika soko la dunia.
Alisema kuwa viongozi wanapaswa waelewe kuwa uongozi ulioko madarakani, serikali na Chama kinachoshika hatamu hakiusiani na suala la mfumko wa bei kwani hilo ni tatizo la wote na kikubwa kinachofanywa na seikali yake hivi sasa ni kukabiliana na tatizo hilo kwa kukiimarisha kilimo.
Dk. Shein alisema kuwa serikali imo katika mikakati maalum ya kuimarisha sekta hiyo kwa kuhakikisha Mapinduzi ya Kilimo yanafikiwa kwa kuimarisha sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuongeza pembejeo na utaalamu wa kilimo kwa kuzalisha chakula kwa wingi na chengine kuweka akiba.
Alisema serikali anayoiongoza imeandaa mipango imara ya kuhakikisha sekta ya kilimo inapiga hatua ikiwa ni pamoja na kukiimarisha kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji, kilimo cha mazao kama muhogo na viazi kwa kutoa mbegu bora pamoja na kuimarisha kilimo cha matunda na mbogamboga.
Aidha Dk. Shein aliwataka viongozi waliopata nafasi za uongozi kutowakimbia wanachama na viongozi wa ngazi za chini wakiwemo viongozi wa Matawi na kusisitiza kushirikiana pamoja katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Dk. Shein alisema kuwa wakati wakitafuta nafasi za uongozi walikuwa karibu na wanachama kwa hali zote usiku na mchana, lakini analoshangazwa kuwaona viongozi hao kuwakimbia viongozi wenzao na wanachama ambao wametoa mchango mkubwa kupata uongozi wao.
Dk. Shein pia, amewataka viongozi hao kushirikiana na viongozi wa ngazi za chini kwa lengo la kuwaeleza mafanikio yaliopatikana nchini ikiwa ni pamoja na hatua zilizofikiwa katika kutekeleza Ilani ya CCM kwa muda mfupi.
Katika maelezo yake alisema kuwa tayari hatua za utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM zimeanza kuchukuliwa kwa kasi ikiwa ni pamoja na kufanya semina ya viongozi wa Serikali nzima kwa kueleza namna ya kufanya kazi ili kuwatumikia wananchi.
Dk.Shein pia, alisisitiza kuwa ajira zitaongezwa na pale patakapokuwa na ajira za serikali vijana wataajiriwa na patakapotokea fursa ya kusaidiwa ili wajiajiri wenyewe watasaidiwa kwani suala la ajira limezungumzwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Dk. Shein amemaliza ziara yake kwa kuzungumza na viongozi wa Wilaya 10 za Unguja na Pemba ambapo pia, katika mazungumzo hayo aliwaahidi kuwa wakati mwengine atakapofanya ziara zake kama hizo itakuwa ni zamu yao kuzungumza, kuuliza, kuchangia, kuhoji ana kwa ana na yeye atawasilikiza na hatimae kutoa majumuisho.
Kwa upande wa maslahi ya wafanyakazi wa sekta ya Umma, Dk. Shein alisema kuwa tayari taratibu zimepangwa katika kuhakikisha wafanyakazi za serikali wanafanyiwa makerekebisho katika mishahara yao sambamba na kuangaliwa suala zima la pencheni.
Nao viongozi wa CCM Wilaya hizo walimpongeza Dk. Shein kwa kazi kubwa anayoifanya katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi. Pia, walitoa shukurani kwa Mama Mwanamwema Shein kwa kushiriki kikamilifu katika kukiimarisha Chama Cha Mapinduzi.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai, alieleza kuwa ziara za Rais zimetoa miongozo mikubwa katika kukiimarisha chama hicho na kumuhakikishia kuwa kwa kushirikiana na viongozi wenzake wote kuanzia Shina hadi Mkoa wa Unguja na Pemba watazifanyia kazi.

No comments:

Post a Comment