Monday 20 June 2011

WAPINGA KUWEPO JAA MAGOFU YA MARUHUBI

Wapinga kuwepo jaa magofu ya Maruhubi

Na Asya Hassan
WANANCHI wameilalamikia Serikali juu ya utupaji taka uliokithiri na kufanyika kwa jaa kubwa katika magofu yaliopo Maruhubi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mkaazi wa eneo hilo, Nassor Muhammed alisema kuwa eneo hilo la magofu ambalo lilikuwa ni kivutio kikubwa cha watalii hivi sasa kumekuwa hakuna haiba ya kuvutia kutokana na kukithiri kwa utupaji taka.
Aidha alisema kuwa kuwepo kwa jaa hilo kunaweza kuhatarisha afya za wakaazi wa eneo hilo kutokana na moshi mkubwa unaotoka wakati wa kuchomwa moto taka hizo na kusambaa majumbani.
Pamoja na hayo alisema kuwepo kwa jaa hilo Serikali inaweza ikapunguza pato lake la uchumi ambalo linatokana na utalii, kwani watalii hawatavutiwa na eneo hilo ambalo halina mandhari nzuri ya kuvutia na kuiomba serikali kupitia idara husika kusitisha zoezi hili utupaji taka ili eneo hilo lirudi katika hali yake ya mwanzo.
Kwa upande wake mkuu wa kitengo cha mambo ya kale Zanzibar, Abdalla Khamis Ali, alithibitisha kuwepo kwa jaa hilo na kusema kwamba eneo hilo limeruhusiwa kutupwa taka kwa muda maalum na sio eneo la kudumu kama inavyodhaniwa ili kufukia mashimo yaliyotokana na uchimbaji ovyo wa mchanga.
Alifahamisha kwamba kwa kuwa eneo hilo lina matatizo hayo kitengo chake kwa kushirikiana Idara ya mazingira walikaa kikao cha pamoja na kujadili namna gani wataweza kuyafukia mashimo hayo ndipo walipoamua kuruhusu Baraza la Manispaa kumwaga taka zake hapo ili kuzuia hali hiyo.
Mkuu huyo alifafanua kuwa kwa vile serikali ina malengo mazuri juu ya kurekebisha eneo hilo hivyo haitaishia kutupa taka tu bali ina lengo la kumwaga fusi katika eneo baada ya kukaa sawa kwa mashimo hayo.

No comments:

Post a Comment