Thursday 23 June 2011

TANZANIA KUANDAA MKUTANO WA SMART PARTNERSHIP.

Tanzania kuandaa mkutano wa Smart Partnership

Mwandishi Maalum, Malaysia
TANZANIA imekubali kuwa mwenyeji wa mkutano ujao wa taasisi ya kujadili maendeleo miongoni mwa nchi zinazoendelea ya Langkawi International Dialogue na Smart Partnership Movement utakaofanyika mwaka 2013 mjini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete alipokea heshima ya kuandaa mkutano huo kwa niaba ya Tanzania wakati wa sherehe ya kufunga mkutano wa mwaka huu wa taasisi hiyo uliofanyika mjini Kuala Lumpur, Malaysia chini ya jina la Langkawi International Dialogue 2011.
Tokea mwishoni mwa wiki wakati ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Rais Kikwete ulipowasili mjini Kuala Lumpur kwa ajili ya mkutano wa taasisi hiyo wa mwaka huu uliomalizika uliomalizika jana kwenye Kituo cha Mikutano ya Kimataifa cha Putrajaya (PICC), Makao Mapya ya Serikali ya Malaysia, waandalizi wa mkutano huo walikuwa wkaiishawishi Tanzania ikubali kuandaa mkutano ujao.
Awali, Rais Kikwete alionyesha kusita kukubali kuwa Tanzania iwe mwenyeji wa mkutano huo hasa kwa sababu waandalizi wa mkutano huo walikuwa wanashikilia kuwa Tanzania iandae mkutano huo mwakani, 2012.
Lakini Rais Kikwete aliwambia kuwa kwa sasa ni vigumu kwa Tanzania kukubali jukumu hiyo kwa sababu Bajeti ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha 2011/2012 imekwishakuwasilishwa Bungeni ili ipitishwe, msimamo ambao Rais Kikwete aliukubali hadharani.
Kutokana na msimamo huo wa Tanzania, waandalizi hatimaye waliomba kuwa kwa sababu Tanzania haiwezi kuandaa mkutano huo mwaka ujao kwa sababu nzuri za kibajeti, basi ukibali kuwa mwenyewe mwaka 2013, ombi ambalo Rais Kikwete amelikubali.
Rais Kikwete aliwaambia wajumbe 540 waliohudhuria mkutano wa mwaka huu wakiongozwa na wakuu wa Nchi, Serikali na mawaziri kutoka nchi 17 kuwa ni heshima kubwa kwa Tanzania kuombwa iwe mwenyeji wa mkutano huo ambao umaarufu wake umekuwa unaongezeka tokea kufanyika kwa mara ya kwanza miaka 15 iliyopita.
Kwa kawaida mikutano ya taasisi hiyo hufanyika kwa kupokezana baina ya Malaysia na nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika na nchi za Caribbean. Mkutano huo unapofanyika katika Malaysia huandaliwa chini ya jina la Langkawi International Dialogue na unapoandaliwa katika nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika hujulikana kama Southern Africa International Dialogue (SAID).
Mkutano wa mwaka huu umehudhuriwa na wakuu wa nchi na Serikali kutoka Tanzania, Zimbabwe, Lesotho na Swaziland, Makamu wa Rais kutoka Kenya na Uganda, Naibu Waziri Mkuu kutoka Namibia na wawakilishi wa viongozi wa Botswana, Cameroun, Gambia, Mozambique, Syechelles, Zambia na wenyeji Malaysia.
Mkutano huo ulikutanisha washiriki 540 kutoka katika Serikali, sekta binafsi, wasomi, taasisi zisizokuwa za kiserikali, pamoja na wawakilishi wa CPTM.

No comments:

Post a Comment