Thursday 23 June 2011

MORO YAANDAA BONANZA KUIBUA VIPAJI VYA USANII.

Moro yaandaa bonanza kuibua vipaji vya usanii

Na Nalengo Daniel, Morogoro
KITUO cha Utamaduni wa Maendeleo ya Vijana Tanzania (KIUMAVITA), kinaandaa bonanza la kwa ajili ya kuinua vipaji vya usanii katika wilaya sita za mkoa wa Morogoro.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa kituo hicho Mohamed Ngwenje, alivitaja vipaji vitakavyovumbuliwa kuwa ni pamoja na uimbaji wa nyimbo za asili, muziki wa kizazi kipya na muziki wa Injili.
Ngwenje ambaye pia ni mratibu wa bonanza hilo, alisema kuwa uibuaji huo wa vipaji utahusisha watu wa rika zote, kwa lengo la kupata wasanii ambao watasaidiwa kurikodi katika studio inayofahamika kwa jina la 'Moro Town Records' ya mjini Morogoro.
Alisema bonanza hilo litaanzia katika wilaya ya Kilosa Juni 26 kwa kutumbuizwa na wasanii watano ambao ni Yussuf Ngwenje ambaye anatamba na kibao cha ‘moyo wangu,’ Khalifa Ramadhan, Emmanuel Ruchamuzi kutoka Uganda na wengine aliowataja kwa jina moja moja, Asia na Linda.
Alifahamisha kuwa, baadaye bonanza hilo litaendelea katika wilaya ya Ulanga, kabla kuhamia Kilombero na katika wilaya nyengine zilizobaki.
Ngwenje aliwataka vijana wanaohisi wana vipaji mbalimbali kujitokeza katika bonanza hilo ambalo litakuwa la kwanza katika mkoa wa Morogoro.
Wavu, mikono Zenj zawika Umiseta
Na Donisya Thomas
TIMU za mpira wa mikono na wavu kutoka Zanzibar kwa wanaume na wanawake zimefanikiwa kutinga nusu fainali ya michuano ya Umiseta inayoendelea kutimua vumbi Wilayani Kibaha.
Kwa upande wa mpira wa mikono vijana wa Zanzibar wametinga nusu fainali baada ya kuichakaza Kaskazini Mashariki kwa mabao 39-14.
Aidha katika mpira wa wavu, Zanzibar imezidi kutamba baada ya kuirarua bila ya huruma timu ya Ziwa kwa seti 3-1.
Mkuu wa msafara wa timu hizo za Zanzibar Mussa Abdurabi, ameliambia Zanzibar Leo kwamba kwa upande wa riadha Zanzibar haishikiki na tayari imejiongezea medali nyengine moja ya dhahabu na hivyo kufikisha medali tano, fedha mbili na shaba tano.

No comments:

Post a Comment