Monday 20 June 2011

BALOZI SEIF AFUMANIA UZEMBE HOSPITALI YA MNAZIMMOJA

Balozi Seif ‘afumania’ uzembe hospitali Mnazimmoja

• Ashitukiza usiku ashangazwa alichoshuhudia
• Akuta umeme umezimwa, mwashaji jenereta hayupo
• Alia maisha ya wagonjwa kuwekwa rehani
Na Abdulla Ali, OMPR
MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amekemea vikali tabia isiyoridhisha ya baadhi ya wahudumu wa afya katika Hospitali Kuu ya Mnazimmoja ya kuhatarisha maisha ya wananchi wenzao kwa kutowajibika ipasavyo.
Balozi Seif Iddi alitoa kauli hiyo alipofanya ziara ya ghafla usiku hospitalini hapo juzi, kufuatia shutuma na malalamiko ya wananchi juu ya vitendo visivyoridhisha hospitalini hapo na utoaji mbaya wa huduma uanofanywa na baadhi ya watendaji.
Alisikitishwa, kushangazwa na kukasirishwa na kitendo cha fundi wa jenereta kutowepo kazini wakati umeme ulipokatika na kusitisha huduma zote za hospitali hadi alipofuatwa nyumbani kwa gari la kuchukulia wagonjwa baada ya muda wa zaidi ya nusu saa.
Makamu huyo wa Pili wa Rais alisema kitendo hicho kimeonesha dharau kazini na kingeweza kusababisha vifo kwa waliokuwa wakihudumiwa kwa wakati huo.
Hata hivyo alieleza kuridhishwa kwake na baadhi ya Madaktari na wahudumu wengine kwa namna wanavyochapa kazi sambamba na jitihada za Serikali za kudumisha huduma hiyo na kuwataka waongeze bidii wakati Serikali inajitahidi kuimarisha mazingira yao.
Alisisitiza haja ya uvaaji wa sare kazini ili waonekane nadhifu na kuwatafautisha na watu wa kawaida wanaoingia bila ya mpango na kusababisha vurugu kwa wagonjwa Mawodini.
Kuhusu uimarishaji wa huduma hizo, Daktari wa zamu katika wodi mbili za Surgical, Dk. Abdulrahman Yussuf aliyekuja kwa mazoezi ya vitendo kutoka Tanzania Bara, alisema ametiwa moyo na jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) za kuimarisha huduma pamoja na za kwao na kusema yuko tayari kufanya kazi Zanzibar baada ya kuhitimu Chuo.

No comments:

Post a Comment