Tuesday 21 June 2011

WAWAKILISHI WAJINOA KWENDA ARUSHA

Wawakilishi wajinoa kwenda Arusha

Na Hamad Hija, Maelezo
TIMU ya soka ya Baraza la Wawakilishi, inatarajia kuanza mazoezi wiki hii kwa ajili ya kujiandaa na ziara ya kimichezo mkoani Arusha mwezi wa Agosti.
Kikosi cha timu hiyo kinachonolewa na kocha Juma Sumbu, kitakuwa kikifanya mazoezi hayo kwenye uwanja wa Mao Dzedong nyakati za asubuhi.
Afisa Michezo wa Baraza la Wawakilishi Dau Hamad Maulid, amesema ziara hiyo ni ya kawaida ambapo kila mwaka kikao cha bajeti kinapomalizika, huwa inakwenda Kilimanjaro ikiwa wageni wa rafiki zao Wazee Sports ya huko.
“Huo ni utamaduni tuliojiwekewa kila tunapomaliza kikao cha bajeti huwatembelea ndugu zetu wa Wazee Sports, kwa lengo la kuimarisha umoja wetu”, alisema.
Dau amesema kabla ya safari hiyo, wanatarajia kucheza mechi kadhaa za kirafiki ili kujipima nguvu na baadhi ya timu za hapa nchini.
Alizitaja timu walizopanga kupambana nazo kuwa ni Unguja Ukuu, Kiwengwa na Makunduchi.
Miongoni mwa wanandinga wanaotegemewa na waheshimiwa hao wa baraza la kutunga sheria ni Hamza Hassan Juma, Ali Abdulla na Issa Gavu pamoja na mlinda mlango Hashim Jaku.
Mbali na timu hiyo ya soka, timu hiyo pia kutakuwa na timu ya netiboli, kuvuta kamba na mbio za magunia, ambapo msafara wake unatarajiwa kuongozwa na Spika wa baraza hilo Pandu Ameir Kificho.

No comments:

Post a Comment