Tuesday 28 June 2011

BALOZI SEIF ATAKA VIONGOZI WASHIRIKI KUTEKELEZA ILANI YA CCM

Balozi Seif ataka viongozi washiriki kutekeleza ilani ya CCM

Na Mwantanga Ame
AHADI ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwatunza wazee, imeanza kutekelezwa kwa vitendo na baadhi ya Wawakilishi, kwa kujitolea kuwapatia misaada wastaafu waliokuwa wakitumikia serikali wa Jamhuri ya Muungano.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alipokea misaada hiyo jana baada ya Mwakilishi wa Jimbo la Rahaleo, Nassor Salum Ali ‘Al-Jazira’, Mbunge wa Jimbo hilo Abdalla Juma Mabodi na mfanyabiashara Amani Makungu kuwasaidia shilingi 700,000 kwa ajili ya wazee hao.
Makabidhiano hayo yalifanyika jana kati ya Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi na Mwakilishi wa Jimbo la Rahaleo, Nassor Salum, katika Chumba cha Maalum cha Wageni mashuhuri ndani ya ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Mwakilishi huyo alisema wameamua kutoa fedha hizo ikiwa ni hatua ya kuunga mkono jitihada za serikali katika kuitekeleza ilani ya CCM ambayo imeahidi kuwatunza Wazee pamoja na makundi mengine.
Alisema wazee wastaafu ni moja ya hazina muhimu kwa taifa na suala la kuwapa matunzo ni moja ya jambo linalohitajika kuzingatiwa na jamii yote.
Kutokana na umuhimu huo, alisema ndio maana Chama cha Mapinduzi katika ilani yake kimeamua kwa makusdi kuhakikisha inawapa kipaumbele wazee kwa kuwapatia matunzo bora.
Alisema hatua hiyo ya serikali ni sehemu ya kuendeleza malengo ya chama cha A.S.P ambacho kimeahidi kuwapa makaazi mema wazee pamoja na kuwatunza.
Nae Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi, alisema serikali inafarajika kuona viongozi wake wamekuwa wakishiriki kuitekeleza vyema ilani ya CCM katika suala zima la kuwatunza wazee kwani ni moja ya mambo ya msingi iliyoahidi katika kampeni zake.
Alisema serikali itahakikisha utekelezaji wa ilani unaenda sambamba kwa kuwashirikisha wazee katika shughuli mbali mbali zikiwemo za maendeleo ikiwa ni moja ya hatua muhimu ya kuwafanya kujisikia kuitumikia nchi yao.
Alisema mchango wa Wazee ni muhimu katika maendeleo ya Zanzibar kutokana na ndio uliosababisha kulifanya taifa hili kuwa huru hivi sasa na haiwezekani wazee kuachwa nyuma.
Alisema ingawa kuna changamoto nyingi za maisha zinazowakabili wazee lakini serikali itahakikisha inapambana nazo na kuitaka jamii kuona nayo inashiriki kuwapatia misaada wazee ili wawe katika maisha mazuri.
Balozi Seif, aliahidi kutimiza ahadi yake ya kuwapatia wazee hao shilingi milioni 1,000,000 ikiwa ni mchango wake kwa Wazee wastaafu wa Muungano.
Mapema mwezi uliopita wazee hao walikabidhiwa boti moja na mashine kwa ajili ya kufanya shughuli zao za maendeleo pamoja na charahani na Mfanyabiashara Mohammed Raza, sherehe ambayo ilifanyika katika viwanja vya bahari ya Kizingo na kuendeshwa harambee iliyochangisha shilingi milioni nne za ahadi na fedha halisi shilingi 400,000.

No comments:

Post a Comment