Tuesday 21 June 2011

ZANZIBAR OCEAN, SIMBA KUNDI MOJA KAGAME.

Zanzibar Ocean, Simba kundi moja Kagame
Itafungua dimba na Wasomali Ettcel
Na Kunze Mswanyama, Dar es Salaam
WAWAKILISHI wa Zanzibar kwenye michuano ya Kombe la Kagame timu ya Zanzibar Ocean View, wamepangwa katika kundi A pamoja na wekundu wa Msimbazi Simba ya Tanzania Bara.
Katibu wa Shirikisho la Soka Tanzania 'TFF' Angetile Osiah, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa timu zote zinazoshiriki mashindano hayo yanayotarajiwa kuanza Juni 26, mwaka huu, zimepangwa katika makundi matatu.
Osieh alisema mbali na timu hizo za Zanzibar na Tanzania Bara, kundi A pia litakuwa na timu ya Ettcel ya Somalia na Vital’O kutoka Burundi, ambapo kundi B linaundwa na timu za Yanga, El Mirrekh ya Sudan, Bunamuaya kutoka Uganda na Elmaan ya Somalia.
Kundi C linajumuisha timu za APR ya Rwanda, Ports FC ya Djibout, Saint George ya Ethiopia na mabingwa wa Kenya Ulinzi.
Kwa mujibu wa Osieh, siku ya ufunguzi wa mashindano hayo yanayodhaminiwa na kampuni ya bia ya TBL, Zanzibar Ocean View itashuka uwanja wa taifa kumenyana na Ettcel ya Somalia wakati wa saa 8:00 mchana, huku Simba ikiivaa Vitalo mnamo saa 10:00 jioni uwanjani hapo.
Katibu huyo wa TFF alieleza kuwa mbali na uwanja wa taifa wa Dar es Salaam, ngarambe hizo pia zitakuwa zikirindima katika dimba la Jamhuri mkoani Morogoro.
Timu ya Yanga imeweza kushirikishwa katika mashindano hayo baada ya kulilipa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) deni la dola 35,000 za Kimarekani ilizokuwa ikidaiwa baada ya kugomea mchezo wa kutafuta ushindi wa tatu dhidi ya Simba katika mashindano kama hayo mjini Dar es Salaam.
Michuano hiyo inafanyika kufuatia wasiwasi wa kukosa mdhamini, baada ya kuokolewa na kampuni ya TBL iliyokubali kuibeba na kuikabidhi TFF shilingi milioni 300 juzi.
Bingwa wa mashindano hayo atanyakua dola 30,000 huku washindi wa pili na wa tatu wakizoa dola 20,000 na 10,000 mtawalia, ambazo hutolewa na Rais wa Rwanda Paul Kagame.
Awali mashindano hayo yalikuwa yafanyike Zanzibar, na baadae kuhamishiwa Sudan kwa sababu tafauti, lakini yakahamishiwa Dar es Salaam kutokana na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yanayoendelea nchini humo.

No comments:

Post a Comment