Thursday 23 June 2011

SERIKALI KUFANIKISHA MAPINDUZI YA KILIMO-- MANSOOR

Serikali kufanikisha mapinduzi ya kilimo – Mansoor

Na Khamis Ali
WAZIRI wa Kilimo na Maliasili, Mansoor Yussuf Himid amewataka wakulima kutarajia mabadilko katika sekta ya kilimo kwani bajeti ijayo itaruhusu kutokea kwa mapinduzi ya kilimo.
Waziri Mansoor aliyasema hayo wakati akizungumza na wakulima wa zao la muhogo baada ya kufanya ziara katika kijiji cha Machui wilaya ya Unguja.
Alisema serikali hivi sasa imo katika matayarisho makubwa ya kukabiliana na matatizo yanayoikabili sekta ya kilimo na inakusudia kuyafanyia kazi katika mwaka mpya wa bajeti ili wakulima waweze kupata nafuu hasa katika upatikanaji wa zana za kilimo.
Alisema serikali ya awamu ya saba inayoongozwa na Dk. Ali Mohamed Shein, imedhamiria kuleta mapinduzi ya kilimo kupitia ilani yake na Wizara yake itahakikisha inatimiza nia hiyo.
Alisema serikali inachokusudia kukifanya hivi sasa ni kuendesha utafiti wa zaidi kwa kuviangalia vyakula vyote vya mizizi ambapo hatua itayoweza kukuza kilimo pamoja na wakulima.
Waziri huyo aliwataka wakulima hao kuona wanaongeza juhudi na kutokata tamaa kutokana na gharama zinazowapata katika ununuzi wa pembejeo ambapo serikali tayari imeshazingatia mahitaji yao.
Waziri huyo alisema mazingatio hayo yamo katika bajeti ijayo ya Wizara hiyo ambapo itaweza kuongeza upatikanaji wa matrekta, mbolea ili kuwafanya kulima kwa wakati na vifaa muhimu vya kilimo ikiwemo miundombinu.
Nao wakulima wa kijiji hicho wameeleza hatua yao ya kufurahishwa na ziara ya Waziri huyo kwa kuweza kuyatambua mahitaji yao kabla bajeti ya wizara hiyo kuanza kusomwa.
Mkulima Suleiman John, alimweleza Waziri huyo kuwa hapo awali walikuwa wakikabilwa na tatizo kubwa na mbegu asili baada ya kupata ugonjwa wa kansa ya muhogo lakini hivi sasa tayari tatizo hilo wameweza kukabiliana nalo baada ya kuanzisha mbegu mpya nne ambazo zilifanyiwa utafiti na kuonekana kufaa kwa eneo lao.
Akizitaja mbegu hizo alisema ni pamoja na ya Mahonda, Machui, Kama na Kizimbani ambazo zimeweza kutoa kiasi kikubwa cha zao la muhogo lakini hivi sasa wamekuwa wakikabiliwa na tatizo la masoko.
Alisema katika mbegu hizo, mbegu ya Machui imeonekana kufanya vizuri zaidi kutokana na kukubaliana na ardhi ya sehemu hiyo ambapo hivi sasa wanaitumia wakulima wengi.
Ziara hiyo pia ilimshirikisha Mkurugenzi wa Idara ya Kilimo Mberik Rashid na Mkurugenzi wa Utafiti Haji Hamid na maofisa wengine wa wizara hiyo.

No comments:

Post a Comment