Tuesday 21 June 2011

SEREKALI YATAHADHARISHWA MASLAHI YA WANAJESHI

Serikali yatahadharishwa maslahi ya wanajeshi

Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Jimbo la Mkanyageni Kisiwani Pemba Mohammed Habib Mnyaa, ameitahadharisha serikali ya Muungano kuepuka kutengeneza maandamano ya Wanajeshi kutokana na serikali kushindwa kuwalipa stahili zao askari wa vikosi vya ulinzi na usalama kwa zaidi ya miaka mitatu sasa.
Tahadhari hiyo aliitoa jana wakati akichangia bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2011/2012 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano huko Mjini Dodoma ambapo matangazo hayo yamekuwa yakirushwa moja kwa moja na Televisheni ya Taifa TBC1.
Mbunge huyo alisema inashangaza hivi sasa kuwepo kwa tatizo kubwa la taasisi hizo kutoingiziwa fedha kwa ajili ya huduma mbali mbali na kuwafanya askari kushindwa kupata stahili zao hata pale wanapoewa uhamisho
Alisema hivi sasa kuna tatizo kubwa katika kufanya malipo ya utoaji wa huduma kwa askari wa vikosi vya ulinzi huku ikifikia taasisi zao kukatiwa umeme kutokana na kuwa na madeni mengi.
Akitoa mfano mbunge huyo alisema kuna askari wa Zanzibar wamehamishiwa katika mikoa mbali mbali ya Tanzania tangu mwaka 2008, lakini jambo la kushangza hadi leo hakuna alielipwa fedha za uhamisho.
Hali hiyo alisema inaweza kusababisha hatari ya kuwaandalia askari mazingira ya kuingia barabarani na kuanzisha maandamano ya kudai haki zaobaada ya kukosa stahili zao kwa muda mrefu kunakosababishwa na serikali yao.
Alisema haitapendeza Tanzania kuona vurugu za maandamano zinaondoka kwa raia na kuhamia katika vikosi vya ulinzi jambo ambalo serikali inapaswa kuiona inachukua tahadhari za awali kuinusuru nchi na jambo hilo kwani inaweza kuleta hatari kubwa.
Wanashangaa kuona taasisi hiyo hivi sasa imekuwa inadaiwa na Shirika la Umeme TANESCO kwa Tanzania Bara na ZECO kwa Zanzibar ambapo zimeshawahi kukatiwa umeme mara kwa mara jambo ambalo ni la kushangaza kuona fedha kwa ajili ya kutumia mambo mengine zimekuwa zikiingizwa lakini tofauti katika utoaji wa huduma hazionekani na kuhoji kuna nini katika taasisi hizo.
Alisema jambo la kusikitisha kuona madeni hayo hayapo kwa wanaopewa uhamisho tuu bali pia yapo kwa askari waliostaafu ambapo hivi sasa kuna watu hawajalipwa mafao yao kwa muda mrefu.
Aidha, alisema jambo la kusikitisha kuona wanapojaribu kutoa madai yao hutakiwa kuyafuata Makao Makuu Dar- es -Salaam jambo ambalo limekuwa likiwapa usumbufu kwani inawezekana wanapojaribu kufuatiatilia kukuta kukiwa hakuna fedha za kuwalipa kwa wakati huo.
Mbunge huyo alisema anashangazwa askari hao wa Zanzibar wanapojaribu kudai kuambiwa waende Makao Makuu wakati wale walioko katika Mkoa ya Arusha na mingine hupelekewa fedha zao walipo bila ya kuitwa kufuata Makao Makuu.
Alisema haoni sababu ya askari wa Zanzibar kutakiwa kwenda Makao Makuu wakati Zanzibar, ikiwa na tawi la Benki Kuu ya Tanzania, ambapo ingelitosha taasisi hiyo kuitumia kuwapatia fedha zao.
Kutokana na adhabu hizo Mbunge huyo, aliiomba serikali kujiangalia katika taasisi hizo na kama imekuwa inaingiziwa fedha kidogo basi ibadili utaratibu wake ili kuiepusha nchi kuingia katika hatari maandamano ya askari kwani bado askari wa Tanzania ni watii kwa serikali yao.

No comments:

Post a Comment