Thursday 23 June 2011

SUWEDI AKABIDHIWA TUNZO YAKE YA MSANII BORA.

Suwedi akabidhiwa tunzo ya msanii bora

Na Mohammed Mzee,
MSANII maarufu wa taarab asilia hapa Zanzibar Iddi Suleiman Suwedi, jana alikabidhiwa tunzo yake ya mwanamuziki bora wa fani hiyo, ambayo ilitolewa katika Tamasha la Zanzibar Music Award 2011, lililofanyika Juni 10, mwaka huu katika ukumbi wa Salama, hoteli ya Bwawani.
Hafla ya makabidhiano ya tunzo hiyo ilifanyika katika klabu ya Culture kwa vile mutribu huyo hakuwepo kwenye tamasha hilo kwa kuwa alikuwa safarini nchini Ujerumani.
Katibu Mkuu wa Culture Taimour Rukuny Twaha, aliyemuwakilisha katika hafla ya Bwawani, alimkabidhi msanii huyo tunzo yake pamoja na fedha taslim shilingi 150,000.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Iddi Suwedi aliwashukuru kwa dhati waandaaji wa tamasha hilo, Zanzibar Media Corporation, inayomiliki kituo cha redio cha Zenj FM na gazeti la Nipe Habari, sambamba na wapenzi wote waliompigia kura, na kumuwezesha kuwa miongoni mwa wasanii bora mwaka huu.
Aidha aliishukuru klabu yake ya Culture kwa mchango wake mkubwa kwa kumlea hadi akafikia kuwa maarufu na kupendwa na wengi.
"Naishukuru klabu yangu ya Culture kwa kunifikisha hapa nilipo kiusanii. Kama sio klabu hii nisingefikia nafasi ya kuonekana na hatimaye kuchaguliwa kuwa mmoja wa wasanii bora," alisema mkongwe huyo wa taarab asilia, aliyepachikwa jina la ‘mpendwa na wengi’.
Hii ni mara ya pili kwa msanii huyo kuibuka na tunzo hiyo, ambapo mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2006 kupitia tamasha hilo, ambalo mwaka huu lilidhaminiwa na Kampuni ya Simu, Vodacom.

No comments:

Post a Comment