Tuesday 21 June 2011

MSHINDO AWATAKA WANAFUNZI KUJIKITA MICHEZONI

Mshindo awataka wanafunzi kujikita michezoni

Na Aboud Mahmoud
WANAFUNZI nchini wameshauriwa kujenga tabia ya kujishirikisha katika michezo kwani hiyo ni sehemu muhimu katika maisha.
Ushauri huo umetolewa na Kamishna wa Michezo na Utamaduni Hamad Bakari Mshindo, kwenye sherehe ya siku ya michezo ikiwa ni shamra shamra za kutimiza miaka 20 ya kuanzishwa kijiji cha SOS.
Alisema kuwa baadhi ya wazee wamejenga dhana ya kuwa michezo ndio chanzo kikuu kinachowafanya wanafunzi wasishughulikie masomo yao jambo alilosema kuwa sio kweli.
Alieleza kuwa michezo na elimu ni miongoni mwa mambo yanayoweza kumfanya mwanafunzi ajenge ufahamu na kufaulu katika masomo yake.
"Mimi napinga dhana ambayo baadhi ya wazee wanasema kwamba michezo inawafanya wanafunzi wasisome," alisema.
Mshindo alifahamisha kuwa ili akili iweze kupumzika baada ya masomo lazima vijana wajishirikishe katika michezo.
Aidha Kamishna Mshindo aliupongeza uongozi wa kijiji cha SOS kwa kuandaa siku maalum kwa ajili ya michezo akisema hiyo ni dalili tosha ya kuwapa mafunzo wazazi kuhusu umuhimu wa michezo.
Nae Mkurugenzi wa kijiji cha SOS Suleiman Mahmoud Jabir, amesema kuwa lengo la kuandaa siku ya michezo kwa wazazi ni kuwaunganisha wazazi na wafanyakazi wa kijiji hicho kwa lengo la kukuza ushirikiano.
Katika sherehe hizo, michezo mbali mbali ilichezwa kwa kushindana baina ya wazazi na wafanyakazi wa kijiji hicho, ikiwemo mpira wa miguu, kuvuta kamba, kutembea, mbio za vijiti, kunywa soda, kupiga penalti pamoja na mpira wa pete.

No comments:

Post a Comment