Thursday 23 June 2011

JAMII YAHIMIZWA KUWATUNZA YATIMA, WZEE.

Jamii yahimizwa kuwatunza yatima, wazee

Na Mwantanga Ame
JAMII imeshauriwa kujenga utamaduni wa kuwapenda kwa kuwatunza watoto yatima na wazee ikiwa ni hatua ya msingi itayoweza kufuata misingi ya maadili ya marehemu Mzee Karume.
Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mama Asha Seif Iddi, aliyasema hayo jana baada ya kuwakabidhi televisheni tatu Wizara ya Ustawi wa Jamii na maendeleo ya Wanawake na Watoto kwa ajili ya Watoto yatima wa Mazizini, Wazee wa Sebleni na Welezo ambapo kwa kila moja ina thamani ya shilingi milioni 1.5.
Sherehe ya makabishiano hayo ilifanyika Makao Makuu ya Wizara hiyo huko Vuga Mjini Zanzibar ambapo Mama Asha aliwataka viongozi wa Wizara hiyo kuona wanaendeleza maadili ya Rais wa kwanza wa Zanzibar Mzee Abeid Amani Karume kuwapenda watoto na wazee.
Alisema Rais Karume aliyapenda makundi hayo kwa kuona nao wanakuwa katika hali nzuri ya kimaisha na ndio maana baada ya Zanzibar kuwa huru aliamua kuanzisha nyumba za wazee pamoja na nyumba za watoto yatima.
Alisema kutokana na kuthamini utamaduni huo ndio maana serikali zote zimeamua kuona makundi hayo yanaendelea kupatiwa matunzo bora ya maisha na haitakuwa busara kuacha kuendeleza maadili hayo.
Alifahamisha kuwa serikali ya awamu ya saba itahakikisha inaendeleza maadili hayo ya Mzee Karume kwa kuwajali Wazee pamoja na watoto yatima kila pale inapoona haja ya kuwa nao pamoja.
Hata hivyo Mama Asha, aliwataka viongozi wa Wizara hiyo kuona wanawapa umuhimu wazee pale inapojitokeza kutaka kupatiwa msaada wa fedha kutokana na baadhi yao hujitokeza maofisini kuhitaji msaada baada ya kukabiliwa na hali ngumu ya maisha.
“Kuna watu wanaweza kuwajia kuwaomba hata 500 ya nauli baada ya kwenda hospitali sasa msije mkawadharau kuwapa msaada wasaidieni kwani ukitoa moja Mungu atakupa nyengine tuwaenzini wazee” alisema Mama Asha.
Aidha, Mama Asha, aliwataka viongozi na wafanyakazi wa Wizara hiyo, kumpa ushirikiano mzuri Katibu Mkuu mpya kwa kuona kuwa wote ni wamoja kwa vile Wizara hiyo inatarajiwa kuwa kiungo kizuri cha kuwaunganisha wanawake kote nchini.
Nae Waziri wa Wizara hiyo, Zainab Omar Mohammed, akitoa shukrani zake, alisema msaada huo utawawezesha walengwa kujenga upeo wao bora kwa kupata habari matukio na taarifa za maeneo mbali mbali duniani na ndani ya nchi.
Waziri huyo aliahidi kuwa msaada huo unawafikia walengwa ili waweze kuwaelimisha walengwa waliokusudiwa yakiwemo makundi hayo.
Waziri huyo alitoa wito kwa jamii kuiga mfano huo wa kutoa misaada yao kwa hali na mali kwani bado kutoa sio kama wanacho bali kuyasaidia makundi hayo ili nayo yawe katika hali nzuri za kimaisha.
Wakati huo huo, Mama Asha alikabidhi msaada kama huo ikiwemo na mashine ya DVD, kwa kituo cha Polisi cha Mfenesini na kuwataka askari hao kukitumia chombo hicho kuweza kufuatilia mambo mbali mbali duniani ikiwa ni hatua itayowasaidia kupata mbinu mpya za kukabiliana na wahalifu.
Alisema amelazimika kuwapatia msaada huo kwa vile muda mwingi hutakiwa kuwa macho kutimiza wajibu wao na kuwapo kwa vitu hivyo vitawasaidia kutekeleza vyema wajibu wao.
Msaada umetolewa na kwa pamoja na Mke wa Rais wa Zanzibar, Mama Mwanamwema Shein, ambapo kesho Mama Asha anatarajiwa kuwakabidhi wazee wa kisiwani Pemba.

No comments:

Post a Comment