Thursday 23 June 2011

JK VYUO VIKUU MALAYSIA NJOONI TANZANIA.

JK: Vyuo Vikuu Malaysia njooni Tanzania

Na Mwandishi Maalum, Malaysia
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, ameiomba Serikali ya Malaysia kuvishawishi Vyuo Vikuu vya nchi hiyo kuanzisha ama kuhamishia shughuli zao, hata ikiwezekana kujenga majengo ya vyuo hivyo, katika Tanzania.
Aidha, Rais Kikwete ameiomba Serikali ya nchi hiyo kuwashawishi wawekezaji wa nchi hiyo ya Kusini Mashariki mwa Asia kuja kuwekeza katika uchumi wa Tanzania ili kusaidia utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliotangazwa majuzi na Rais Kikwete na hatimaye kuridhiwa na Bunge.
Maombi hayo ya Tanzania yamewasilishwa kwa Malaysia na Rais Kikwete mwenyewe wakati wa mkutano wake na Waziri Mkuu wa Malaysia, Dato’ Sri Mohammed Najib Tun Abdul Razak.
Viongozi hao wawili walikutana juzi kwenye Cyberview Lodge, iliyoko Cyberjaya, mjini Kuala Lumpur baada ya kushiriki mkutano wa Wakuu wa Nchi, Serikali na viongozi wa ujumbe mbali mbali waliokuwa wanashiriki katika mkutano wa mwaka huu wa taasisi ya maendeleo ya Langkawi International Dialogue (LID) 2011, uliomalizika juzi.
Katika mkutano huo, Rais Kikwete amemwomba Waziri Mkuu Razak kuwashawishi Wakuu wa vyuo vikuu na makampuni ya Malaysia kukubali kuja kuwekeza katika uchumi wa Tanzania.
Rais Kikwete amemwelezea Razak kuhusu Mpango huo wa maendeleo ambao ni sehemu ya Visheni ya Maendeleo ya 2025 inayolenga kuitoa Tanzania katika umasikini na kuifanya nchi yenye uchumi wa kati.
Rais Kikwete pia amemweleza Razak kuwa Mpango wa Maendeleo mpya wa Tanzania ni mpango mzuri na kwamba changamoto kubwa ni kuhakikisha kuwa mpango huo unatekelezwa na hivyo kuleta matunda na matokeo mazuri kwa Watanzania.

No comments:

Post a Comment