Monday 20 June 2011

UINGEREZA OUT UEFA U-21

Uingereza 'out' UEFA U-21

COPENHAGEN, Denmark
MAGOLI mawili ambayo timu ya soka ya Jamhuri ya Czech ilifunga katika dakika za mwisho za mchezo, yalitosha kuitupa nje Uingereza kwenye mashindano ya ubingwa wa Ulaya kwa vijana walio chini ya miaka 21.
Uingereza ilihitaji ushindi ili iingie nusu fainali, na ilionesha dalili za kufanikiwa baada ya Danny Welbeck kuifungia bao mnamo dakika ya 76, lililoifanya timu hiyo iongoze.
Lakini wachezaji Jan Chramosta na Tomas Pekhart walioingia baadae wakitokea benchi, walifuta ndoto za Waingereza kwa kuipachikia Czech mabao mawili ya haraka haraka katika dakika za 89 na zile za majeruhi.
Kwa ushindi huo, Czech sasa itaikabili Uswisi kesho katika mchezo wa nusu fainali.
Katika pambano hilo, kocha wa Uingereza Stuart Pearce akijaribu kusaka ushindi aliwaweka benchi wachezaji Jack Rodwell, Danny Rose na nahodha Michael Mancienne.
Aidha beki wa kati wa Manchester United Phil Jones alikabidhiwa unahodha huku Tom Cleverley akiwa miongoni mwa wanandinga walioanza sambamba na Fabrice Muamba na Scott Sinclair, Uingereza ilionekana kubadilika lakini siku haikuwa yao.
Hispania ndiyo kinara wa kundi B kwa kufikisha pointi saba, na Czech imeshika nafasi ya pili kwa kukusanya pointi sita, na kuziacha Uingereza na Ukraine zikiwa na pointi tatu na moja mtawalia.

No comments:

Post a Comment