Thursday 23 June 2011

MAGENDO YA KARAFUU YAIKOSESHA ZANZIBAR DOLA MILIONI 16

Magendo ya karafuu yaikosesha Zanzibar dola milioni 16

• SMZ yapanga mkakati kudhibiti bei
• Yasisitiza mafuta kutolewa kwenye muungano
Na Ramadhan Makame
SERIKALI katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, imepoteza kiasi cha dola za Marekani milioni 16, kutokana na vitendo vya usafirishaji nje kwa magendo zao la karafuu.
Waziri wa Biashara Viwanda na Masoko, Nassor Ahmed Mazrui alilieleza Baraza la Wawakilishi lililopo Mbweni nje kidogo ya mji wa Zanzibar alipokuwa akichangia bajeti ya serikali ya mwaka 2011/2012.
Waziri huyo alisema vitendo vya usafirishaji magendo karafuu nje ya Zanzibar vimekuwa na athari kubwa kwa uchumi wa Zanzibar kutoka na kuikosesha mapato serikali.
Mazrui alisema usafirishaji magendo wa zao la karafuu limeifaya nchi ya Kenya kuwa muuzaji mashuhuri wa zao la karafuu kwa zaidi ya tani 2,000 katika soko la dunia huku ikizingatiwa kuwa katika nchi hiyo hakuna mikarafuu inayolimwa.
“Nawasihi sana, tuache kuuza karafuu kwa magendo, zao la karafuu litumike kuwanufaishana wananchi wa Zanzibar. Serikali itapandisha bei nzuri sana na ni lengo letu kukifufua kilimo cha karafuu”, alisema waziri huyo.
Akizungumzia suala la Zanzibar kuwa bandari huru, alisema kuna kampuni imeajiriwa kulifanyia utafiti la kuifanya Zanzibar kuwa ni miongoni mwa eneo tengefu kiuchumi.
Alisema baada ya ripoti kukamilika itawasilishwa katika baraza la wawakilishi kupata michango ya viongozi hao na kuifanya Zanzibar kuwa nchi itakayokuwa uchumi wake unakuwa kwa kasi kubwa.
Akizungumzia juu ya tatizo la upandaji ovyo wa bei za vyakula alisema upo mpango ambao utahakikisha uwekaji wa bei za bidhaa muhimu za vyakula unashirikisha baina ya serikali na wafanyabishara.
Kwa upande wake Waziri wa Ardhi Makazi Maji na Nishati, Ali Juma Shamuhuna alisema serikali ya awamu ya saba imesimama pale pale kwa kusema kuwa mafuta na gesi asili lazima yatolewe katika orodha ya mambo ya Muungano.
Waziri huyo alisema shindikizo la kutaka kuiondoa rasilimali hiyo katika mamlaka ya Muungano lazima lifikishwe Bungeni kwa ajili ya kuondolewa kwani suala la uchumi si katika mambo ya Muungano.
Alisema katika visiwa vyote vya Unguja na Pemba kUna akiba kubwa ya gesi asilia na wala hakuna ubishi wa kufanywa utafiti wa mafuta kwani yapo ya kutosha.
Naye Fatma Abdulhabib Ferej alisema kutokana na serikali kutopandisha kodi, ni vyema msisitizo na mkazo ukawekwa katika kudhibiti mvujo wa mapato, wigo wa kuongezwa ukusanyaji mapato, kuondosha misamaha ya kodi pamoja na kupunguza matumizi ya serikali.
Aidha waziri huyo alionesha kuridhishwa kutokana na bajeti hiyo kutoa vipaumbele zaidi katika sekta za jamii ikiwemo afya, elimu na maji huku akisema kuwa hizo ndizo kero zinazowakabili Wazanzibari.
Bajeti hiyo ilitarajiwa kupitishwa jana jioni baada ya kuchangiwa na wajumbe kadhaa za Baraza hilo na waziri wa Nchi Ofisi Rais Fedha Uchumi na Mipango ya Maendeleo kufanya majumuisho.

No comments:

Post a Comment