Tuesday 12 April 2011

IFM YAZINDUWA MAFUNZO YA BIMA ZANZIBAR.

IFM yazindua mafunzo ya bima Zanzibar

Na Juma Masoud

KITIVO cha Bima na hifadhi ya jamii cha Chuo cha Usimamizi wa Fedha Tanzania (IFM), jana kimezindua programu ya mafunzo ya bima Zanzibar.

Akizindua mafunzo hayo Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Bima Tanzania Juma Juma Makame alisema hatua ya Chuo hicho kuendesha mafunzo hayo hapa Zanzibar yatapunguza gharama za kufuata mafunzo ya aina hiyo nje ya nchi.

Alisema kuendeshwa kwa mafunzo hayo hapa Zanzibar, kunakwenda sambamba na mahitaji ya huduma hiyo kutoka kwa makundi mbali mbali yanayohitaji shughuli za bima.

Alifahamisha kuwa umakini kwa wateja wa huduma hiyo ni muhimu katika kujenga uelewa juu ya huduma za bima, na kushindwa kupata uelewa wa kutosha kunaweza kusababisha wananchi kuacha kutumia huduma hiyo.

Naibu huyo alisema mafunzo hayo ya miezi mitatu yanaweza uongeza idadi ya watumishi wenye uwezo hapa Zanzibar watakaosaidia kuongezeka kwa soko la wanaojiunga na huduma ya bima inayoonekana kupungua.

Akizungumzia kuimarika kwa huduma ya kibima Tanzania, Naibu huyo alisema maamuzi ya serikali yaliyoanzisha sheria namba 18 ya mwaka 1996 iliyoanzisha kanuni kupitia notisi namba 124 ya Machi 13, mwaka 1998 ambayo ilifanyiwa marekebisho na sheria ya bima namba 10 ya 2009 yaliimarisha huduma hiyo.

Alisema Chuo cha usimamizi wa fedha Tanzania kimekuwa kituo muhimu cha mafunzo kwa kutoa mafunzo ya bima hapa nchini huku akisema kuwa Zanzibar ni miongoni mwa nchi zinazofaidika na fursa sawa katika kupata taaluma.

Alisema mafunzo hayo yatakayodumu kwa muda wa miezi mitatu hapana shaka yatatoa mwanga na kuongeza kiwango cha utendaji wa shughuli za kibima kwa wahusika.

Naye Mkuu wa Chuo hicho Prof. Godwin Mjema, alisema mafunzo hayo ambayo kwa mara ya kwanza yataendeshwa Zanzibar na kuwashirikisha wanafunzi 35 yanalenga kuleta ushirikianao baina ya shirika la bima la Tanzania Zanzibar na Chuo cha Usimamizi wa fedha hususan kitivo cha bima na uhifadhi wa jamii.

Aidha alisema pia kitatoa muongozo kwa wanafunzi kusoma na kujadiliana kutoka kwa wahadhiri wazoefu mambo mabali mbali yanayohusu taaluma ya bima ambayo aidha wamekuwa wakiitumia au wataitumia baada ya kumaliza mafunzo hayo.

Mkuu huyo alisema program hiyo itawasaidia wanafunzi wenye utashi ulio sawa katika fani ya bima yenye lengo la kuanzisha mahusiano pamoja na kubadilishana uzoefu yatakayokisaida kitivo hicho kutoa program za masoko.

Prof. Mjema alisema hicho kinaendelea kutoa mafunzo ya program mpya mbali mbali ikiwemo diploma ya juu ya bima iliyoanzishwa 1979. kufuatia mabadiliko ya kitivo hicho program nyengine kama vile kanuni za uongozi.

No comments:

Post a Comment