Tuesday 26 April 2011

WENYE MAHITAJI MAALUM WANA HAKI KUPEWA ELIMU - MKURUGENZI

Wenye mahitaji maalum wana haki ya kupewa elimu - Mkurugenzi

Na Luluwa Salum, Pemba
WALIMU wanaofundisha skuli zenye vituo vya elimu mjumuisho wametakiwa kutowabagua watoto wenye mahitaji maalumu na kuhakikisha wanawapatia elimu sawa na watoto wengine.
Akizindua vituo vya Elimu mjumuisho katika skuli za Kangani na Michenzani Pemba, Mkurugengezi Idara ya Elimu Msingi Zanzibar, Uledi Juma Wadi, alisema Elimu ni haki ya kila mtu, hivyo kuna ulazima wa kupatiwa bila ya ubaguzi wowote.
Mkurugenzi huyo alisema watu wenye mahitaji maalumu ni sawa na binaadamu wengine wa kawaida hivyo suala la kupewa alimu ni haki yao ya msingi miongoni mwa haki za binaadamu.
Alisema serikali imeona umuhimu wa kuwepo vituo hivyo katika skuli mbali mbali za Zanzibar, ikiwa lengo ni kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata elimu.
Aliwataka wazazi na walezi kutowafungia ndani watoto wao wenye ulemavu na kuwafichua wale wote wenye watoto walio na mahitaji maalum ambao wanapinga agizo la serikali la kuwapeleka skuli.
Alifahamisha kuwa mashirikiano kati ya wazazi na walimu ndio chachu ya mafanikio na kuwataka walimu wanaofundisha katika skuli zilizo na vituo vya elimu mjumuisho kuwa na hekma na busara wakati wanapofundisha na kuepukana na kutoa adhabu nzito.
Aidha aliwata Walimu kujiendeleza kimasomo na kutoridhika na elimu waliyonayo na endaopo zitatokea nafasi za kusoma masomo ya elimu mjumuisho basi wasizikatae nafasi hizo kwa dhana ya kuwa ni mzigo kubwa kufundisha walemavu.
Kwa upande wao walimu wanaofundisha katika skuli hizo wameahidi kutoa elimu sawa kwa watoto wote bila ya kujali tofauti zao na kuiomba serikali kuwapatia nyenzo za kufundishia sambamba na kuhakikisha nafasi za masomo zinazotolewa zinawafikia walegwa.

No comments:

Post a Comment