Monday 25 April 2011

SINGIDA WAMTAKA CAG KUKAGUA HESABU HALMASHAURI.

Singida wamtaka CAG kukagua hesabu halmashauri

Na Jumbe Ismailly, Singida
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Singida kimesema kinakusudia kumwandikia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali kuomba uchunguzi maalumu (Special Ordit) wa fedha za Halmashauri ya wilaya ya Singida.
Kauli hiyo imetolewa na Mbunge wa jimbo la Singida Mashariki (CHADEMA), Tundu Lissu kwenye mkutano maalumu wa baraza la madiwani ulioandaliwa kwa ajili ya kupitisha mapendekezo ya bajeti ya mapato na matumizi ya Halmashauri hiyo kwa
mwaka 2011/2012.
Lissu alisema kwamba chama hicho kinakusudia pia kumwandikia waziri wa Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa (TAMISEMI), kumwomba afanye uchunguzi wa namna ya uendeshaji wa vikao vya Halmashauri ya wilaya ya Singida.
Kwa mujibu wa mbunge huyo kupitia tiketi ya Chadema haiwezekani na haiingii akilini kabisa bajeti ya mabilioni ya shilingi ikapitishwa ndani ya muda wa dakika 30 kama hakuna mambo ya kuficha na kama hakuna uchafau wa kuficha.
“Sasa tunataka Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu ya serikali aje afanye uchunguzi maalumu ili ajiridhishe na aturidhishe na sisi kwamba hakuna uchafu unaofichwa”,alisema Mbunge huyo kijana wa Chadema.
Lissu ambaye ni waziri Kivuli wa wizara ya Sheria na Katiba alizitaja hatua zingine watakazochukua ni pamoja na kwenda kila kijiji cha jimbo la Singida mashariki kuwaeleza wananchi juu ya maamuzi yanayo pitishwa na madiwani wao.
“Jambo la pili walipoanza kupitisha pitisha hivi tuliwasiliana na Naibu waziri wa TAMISEMI, Aggry Mwanry na akasema atampigia simu katibu tawala wa Mkoa wa Singida haraka iwezekanavyo ili aje kuzuhakiki”, alisema mbunge huyo.
Kwa upande wake Mbunge wa viti maalumu (CHADEMA) Christo Mtinda, alisema kikao hicho hakikufuata taratibu za vikao na kwamba ni kikao ambacho kilikuwa kimepangwa kivurugwe kwa makusudi.
Kwa mujibu wa Mtinda ambaye pia ofisa Mwandamizi kwenye Kurugenzi ya mafunzo ya Chama hicho alisema yeye binafsi
ameshindwa kuelewa vitu gani ambavyo vipo kwa muda ule ambao alipewa lile kabrasha lenye kuonyesha mapendekezo hayo ya bajeti ya Halmashauri.
Mbunge huyo alisema jambo lililomshangaza ni kuona Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, alionekana kuwa yeye ndiye Mwenyekiti wa Halmashauri.
Akijibu hoja za wabunge hao Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Joseph Sabore licha ya kukiri kwamba kikao hicho kilitakiwa kuijadili taarifa ya mapato na matumizi ya mwaka2010/2011, lakini alishindwa kutoa ushahidi wa namna kanuni hiyo ilivyotekelezwa kwenye kikao hicho.

No comments:

Post a Comment